Home » » TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuwaunga mkono Wawekezaji wa ndani na nje ya Zanzibar kwa lengo la kukuza na kuuimarisha uchumi sambamba na maendeleo ya Zanzibar.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, huko katika kwianda cha Sukari Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja, mara baada ya kufanya ziara ya kukitembelea kiwanda hicho na kuangalia ukarabati mkubwa wa majengo pamoja na mitambo yake unaoendelea kufanywa na wawekezaji wa Kampuni ya Shanta Sugar Holding Lmtd kutoka nchini India.

Katika maelezo yake Dk. Shein aliueleza uongozi wa Kampuni hiyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini juhudi kubwa zilizochukuliwa na wawekezaji hao zikiwemo za kuanza awamu mpya ya kiwanda hicho kwa kutumia compyuta na digital katika uzalishaji wa sukari na bidhaa nyengine zinazotokana na miwa.

Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuwaunga mkono wawekezaji wa kiwanda hicho kwani mkakati maalum umewekwa na Serikali kwa kukiimarisha kiwanda hicho kwa kutambua kuwa hakuna nchi yoyote duniani inayoweza kuimrika bila ya waekezaji.

“Wawekezaji ni lazima wasaidiwe ili  waweze kuekeza vizuri”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo  kusisitiza haja ya kuimarisha uhusiano mwema kati ya wawekezaji na Serikali ili na wao wapate faida na biashara izidi kuwa nzuri huku akieleza matumaini yake kuwa wananchi watapata nafuu kubwa ya bidhaa hiyo mara uzalishaji utakapoanza kiwandani hapo.

Dk. Shein aliwapongeza wawekezaji hao kwa kuekeza Dola milioni 30 kwa hatua za mwanzo sambamba na juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na uongozi wa kiwanda hicho za kuongeza Dola nyengine milioni 11.5 za Kimarekani katika kukiimarisha kiwanda hicho ambacho kitakuwa na mitambo ya kisasa na uzalishaji bora wa sukari na bidhaa nyegine zitokazo na miwa.

Dk. Shein alisema kuwa juhudi za  wawekezaji hao zimemtia moyo mkubwa ikiwa ni pamoja na azma yao ya kutoa ajira kwa vijana zipatazo 200 katika sehemu za kiwandani na 500 mashambani na kuendelea zaidi ajira hizo kwa kadri uzalishaji utakavyoimarika.

Pia, Dk. Shein alifarajika kwa maelezo aliyoyapata kutoka kwa uongozi wa Kampuni hiyo wa kueleza kuwa watazalisha umeme wao wenyewe ambao watatumia kiwandani hapo na mwengine kuweza hata kuliuzia Shirika la Umeme la Zanzibar ZECO ili kuweza kuwasambazia wananchi vijijini.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwahakikishia wawekezaji hao kuwa maombi yao waliyoyatoa kwake yakiwemo kuongezewa heka 3500 za ziada, maghala ya kuhifadhia biadhaa zao pamoja na nyumba za wafanyakazi ambayo yote hayo kwa mujibu wa maelezo ya Dk. Shein yatafanyiwa kazi kwa taratibu maalum za serikali.

Dk. Shein aliwapongeza wawekezaji hao kwa kazi kubwa walizofanya pamoja na hatua kubwa iliyofikiwa katika uimarishaji wa kiwanda hicho licha ya changamoto kadhaa zilizojitokeza ambazo zinaendelea kupatiwa ufumbuzi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitoa rai kwa wawekezaji hao kuitumia vyema mbolea watakayoitoa kiwandani hapo kwa kuanzisha kilimo cha mboga mboga sambamba na kuwasaidia wakuma wadogo wadogo ili na wao waweze kuzalisha mbogamboga na kuweza kusaidia maendeleo ya Zanzibar

Mapema Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Omar Yussuf Mzee alieleza kuwa Mradi  wa kiwanda hicho ni muhimu sana kwani utaimarisha uchumi wa Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa unaunganisha sekta ya Kilimo hapa nchini.

Mzee alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake ya Fedha iliona ipo haja kubwa ya kuunga mkono Mradi huo kwani utasaidia sana uchumi na maendeleo ya Zanzibar kwani ni mradi wa Kitaifa na utachangia sana taifa.

Akieleza faida nyengine muhimu mbali ya uzalishaji wa sukari kutoka kiwandani hapo, Waziri Mzee alisema kuwa kiwanda hicho kitasaidia suala zima la ajira, umeme, mbolea na kueleza kuwa katika uzalishaji wa kiwanda hicho hakuna kitakachotupwa.

Nae Mwenyekiti wa Kampuni hiyo ya uwekezaji Bwana Mahesh Patel alimueleza Dk. Shein hatua mbali mbali zilizofikiwa na kiwanda hicho katika ukarabati wake mkubwa unaoendelea huku akimuahidi kuwa kiwanda hicho kitanza kuzalisha  sukari mwezi wa Januari mwakani.

 Mwenyekiti huyo alimueleza Dk. Shein miongoni mwa juhudi za ujenzi na ukarabati uliofanyika ikiwa ni pamoja na ujenzi hodhi la kubwa la maji ambalo litasambaza maji mashambani, azma ya sukari  itakayozalishwa kiwandani hapo kuwa na kuwa na  nembo maalum‘Brand’ ya Zanzibar, unafuu wa bei ya bidhaa hiyo kwa wananchi wa Zanzibar na mambo mengineyo.

Aidha, Mwenyekiti huyo alieleza kuwa hatua hizo zilizoanza mwaka jana zimefikia pazuri  na kutumia fursa hiyo kueleza kuwa uzalishaji wa kiwanda hicho utasaidia uchumi wa Zanzibar sambamba na kuweka historia nzuri ya Zanzibar katika biashara na uwekezaji huku akitoa pongezi kwa Serikali hasa Wizara yake ya Fedha kwa mashirikiano mazuri wanayoyapata. 

Akitoa maelezo ya utangulizi Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maeneo Huru na Vitega Uchumi Zanzibar  (ZIPA) Salum Khamis Nassor, alisema kuwa ujenzi na ukarabati mkubwa unaoendelea kufanywa na waekezaji hao hasa ikizingatiwa kuwa zaidi ya mitambo yenye asilimia 80 kiwandani hapo ni chakavu ambayo itabadilishwa upya una umuhimu mkubwa katika uchumi wa Zanzibar.

Alisema kuwa hatua hiyo imefikiwa ili haja ya kiuchumi iweze kutimia hapa Zanzibar na kueleza kuwa muda si mrefu matunda ya kiwanda hicho yataanza kuonekana

Kambla ya mazungumzo hayo Dk. Shein alitembelea kiwanda hicho katika maeneo yote na kuangalia hatua za ujenzi zinazoendelea pamoja na uwekaji wa mitambo mipya, miundombinu ya maji, umeme  pamoja na shughuli nyenginezo za kiwanda na kupata maelezo kutoka kwa viongozi wa kiwanda hicho.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
 

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa