Home » » VUAI: ATOA MAAGIZO MAZITO KWA KAMATI YA SIASA MKOA WA KASKZN UNGUJA

VUAI: ATOA MAAGIZO MAZITO KWA KAMATI YA SIASA MKOA WA KASKZN UNGUJA


Na Is-haka Omar, Zanzibar.

WAJUMBE wa Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Kaskazini Unguja Kichama wametakiwa kutumia vikao halali kama inavyoelekezwa na Katiba na Kanuni za Chama kwa kuwahoji na kuwachukulia hatua mwafaka baadhi ya viongozi na wanachama wanaokwenda kinyume na misingi ya Chama Cha Mapinduzi.

 Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai na  Kamati ya siasa ya Mkoa huo katika kikao cha kuongeza ufanisi wa kiutenda huko Mahonda Unguja, alisema viongozi hao wanatakiwa kuwa na uthubutu wa kufichua wale wote wanaokwenda kinyume na matakwa ya Chama.

Vuai aliwakumbusha viongozi hao kuwa wana mamlaka ya kuwachukulia hatua za kuwaita , kuwahoji na kuwapa fursa ya kujitetea katika vikao halali vya chama viongozi na wanachama wanaotuhumiwa kufanya vitendo vinavyokwenda kinyume na Katiba ya CCM au maelekezo ya chama.

 “Kamati ya siasa ya Mkoa nyinyi ni ngazi ya juu kabisa ndani ya Mkoa kichama, hivyo mnawajibu wa kuchukua maamuzi ya kuwaita baadhi ya watu mnaowashuku kukisaliti chama katika vikao stahiki na kuwahoji na kuwapa nafasi ya kujitetea kabla ya kuwaadhibu.”, alisema Vuai.

 Vuai alisisitiza kuwa hatua za  kuwashughulikia Wanachama wa Chama hicho wanaotuhumiwa kwenda kinyume na maadili ya Chama ni lazima kuhakikisha hakuna Mwanaccm anayechukuliwa hatua kwa kuonewa au kudhalilishwa.

 Alikemea tabia za baadhi ya Wana CCM kuitana  wasaliti bila ya kuwa na ushahidi wa kutosha katika kuthibitisha tuhuma hizo, kwani zinaweza kukwamisha utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja na maendeleo ya Chama kwa ujumla.

“ Viongozi lazima muwe makini tunapoletewa kesi fanyeni utafti kwanza  kwani kuna tuhuma zingine zinatokana na chuki binafsi hivyo watu wanaona njia ya kumaliza visasi vyao ni kuwatuhumu wenzao kuwa ni wasaliti, wakati mwingine tuhuma hizo zinakuwa hazina ukweli.”, alisisitiza Vuai na kuongeza kuwa CCM ni chama kinachosimama katika misingi ya ukweli na hakiwezi kufanya uonevu kwa watu wasiokuwa na hatia.

Naibu Katibu Mkuu huyo aliitaka Kamati hiyo kuendelea kujenga mazingira rafiki ya kuwa karibu na viongozi wao wa ngazi za chini pamoja na wanachama wote kwa lengo la kujua kwa undani changamoto zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao.

 Alieleza kwamba misingi ya Demokrasia, nidhamu na uwazi uliojengeka  ndani na nje  ya chama hicho vinatakiwa kulindwa na kuenziwa na kila kiongozi anayekabidhiwa dhamana za kiutendaji au uongozi.

Alieleza kuwa kazi iliyopo mbele ya chama ni kujiandaa kwa mambo mbali mbali yakiwemo Uchaguzi wa ndani wa CCM wa mwaka 2017, kwa ajili ya kupata viongozi makini watakaobeba jukumu la kusimamia maandalizi ya Uchaguzi Mkuu ujao na kuhakikisha Chama hicho kinapata ushindi wa kihistoria.

Alisema wanachama wanaokusudia kuwania nafasi mbali mbali za uongozi wa Chama na Jumuiya zake , lazima wawe Wanaccm safi ambao hawana rekodi mbaya ya utumishi wao  ndani ya chama au serikalini hata katika nafasi zozote ya uongozi walizowahi kutumikia hapo nyuma.

Pamoja na hayo aliwashauri viongozi kuwa mabalozi wazuri  kwa kuwasihi wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo zinazofanywa na serikali pamoja na kulinda amani na utulivu wa nchi.

Hata hivyo aliipongeza Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Kaskazini Unguja, kwa juhudi zao katika  kuimarisha Chama pamoja na kusimamia kwa vitendo  utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa