Home » » BANDARI YACHANUA LIGI KUU YA GRAND MALT ZENJI

BANDARI YACHANUA LIGI KUU YA GRAND MALT ZENJI



na Mwandishi wetu, Zanzibar
LIGI Kuu ya soka ya Grand Malt ya visiwani hapa, iliendelea juzi kwa timu ya Bandari kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mundu kwenye Uwanja wa Amaan.
Katika mchezo huo uliokuwa na ushindani pande zote mbili karibu muda wote, ilikuwa ni dakika ya 42, Bandari walipofanikiwa kupata bao pekee kupitia kwa mshambuliaji wake, Hissam Hamis.
Hata hivyo, washambuliaji wa Mundu hawakuwa makini, kutokana na kupoteza nafasi kadhaa walizotengeneza na kuishia kupiga mashuti pembeni ya lango na kusababisha wapoteze pointi tatu muhimu kwenye ligi hiyo.
Katika mchezo mwingine uliofanyika Pemba, kwenye dimba la Gombani, mabingwa wa zamani wa ligi hiyo, Jamhuri, waligawana pointi na Mtende ambayo imepanda daraja msimu huu, baada ya dakika 90 kumalizika wakiwa sare ya bao 1-1.
Ligi hiyo ilitarajiwa kuendelea tena jana jioni, kwa kuzikutanisha timu za Malindi na Chuoni kwenye Uwanja wa Amaan, wakati huko Pemba, Chipukizi watawakaribisha maafande wa Mafunzo Uwanja wa Gombani na leo jioni, Dume itavaana na Mtende huku usiku Falcon watachuana na Mafunzo.
Kampuni ya Bia Tanzania kupitia kinywaji chake kisicho na kilevi cha Grand Malt, ndio wadhamini wakuu wa ligi hiyo inayoshirikisha timu 12 kutoka Unguja na Pemba.
Mshindi wa kwanza wa ligi hiyo ataiwakilisha Zanzibar katika mashindano ya Klabu Bingwa Afrika pamoja na michuano ya Kombe la Kagame huku mshindi wa pili atapeperusha bendera ya Zanzibar kwenye mashindano ya Kombe la Shirikisho (CAF).
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa