Home » » ZANZIBAR ISAIDIWE KUBORESHA HUDUMA ZA KIFEDHA

ZANZIBAR ISAIDIWE KUBORESHA HUDUMA ZA KIFEDHA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Zanzibar ndiyo mkoa wa kwanza wenye idadi ndogo ya watu wanaopata huduma za kifedha, licha ya kuwa na mitandao ya simu kama ile iliyopo bara.
Ripoti ya hivi karibuni iliyotolewa na Mfuko wa Kuendeleza Huduma za Fedha Tanzania (FSDT) inaonyesha kuwa Zanzibar inashika mkia licha ya Tanzania kuongoza duniani kwa kutumia simu kujipatia huduma za kifedha.
Idadi ya wanaotumia benki imeongezeka kutoka asilimia 9.1 mwaka 2009 mpaka asilimia 13.9 mwaka 2013.
Aidha, asilimia 73.2 ya watu hao wamekuwa wakipata huduma za kifedha zinazojumuisha bima, vyama vya kuweka na kukopa na kutuma na kupokea fedha kupitia taasisi nyingine mbalimbali zilizoanzisha huduma za kutoa huduma za fedha.
Ongezeko hili la wanaopata huduma hizi linaonekana zaidi kwa watu wa bara pekee kwani, kwa Zanzibar, takriban asilimia 50 hawapati huduma hizi.
Huko, asilimia 11.5 ya watu wamekuwa wakitumia benki wakati asilimia 25.5 wamekuwa wakipata huduma hizo kupitia simu na asilimia 17.1 wanatumia huduma nyinginezo za fedha.
Hali ni tofauti na Mkoa wa Kilimanjaro unaoongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watu wapatao huduma za kifedha ikifuatiwa na Dar es Salaam.
Mkoa wa Kilimanjaro una asilimia 93.8 ya watu wanaopata huduma za fedha ukilinganisha na asilimia 54.1 kwa Zanzibar. Asilimia 16.8, zaidi ya wastani wa Taifa, wanapata huduma za benki huko Kilimanjaro.
Mojawapo ya sababu za hali kuwa mbaya kwa Zanzibar ni taarifa kwamba wengi hawajishughulishi na uzalishaji.
Hii inaweza ikawa sababu ya wao kutopata huduma hizi kutokana na ukweli kwamba hawana uwezo wa kumudu gharama hizo.
Wakati Tanzania sasa ikiwa na matawi ya benki yanayofikia 50 kote nchini na watumiaji wa simu wapatao milioni 28, kuna haja ya watu wa visiwani kubadilika na kuondokana na mfumo huo wa maisha.
Mitandao ya simu iliyopo, bara ipo Zanzibar pia, jambo linalotoa fursa sawa kwa wote.
Licha ya kwamba ripoti hiyo inaonyesha watu wengi wanahifadhi fedha zao nyumbani, bado wanatuma na kupokea fedha kwa kutumia njia tofauti na hata kufanya malipo pia kwa njia hizo, mfano m-pesa, airtel money, tigo pesa na hata easy pesa.
Pamoja na sababu nyingi za Watanzania wengi kutotumia huduma hizi, bado kuna kila haja ya kubadilika na kutoishi kijima kwani uchumi wa nchi hii unakua na mwingiliano na mataifa mengine unaongezeka.
Kutokuwa na fedha za kutosha, umbali wa kufuata huduma na gharama kubwa za huduma hizo kumekuwa kukielezewa kuwa ni kikwazo kwa watu wengi kumudu huduma hizo wakati wa zoezi la ukusanyaji wa taarifa za utafiti huo.
Wakati taasisi za fedha zikishauriwa kuangalia gharama za huduma zao, wananchi hawana budi kubadilika ili kuendana na mfumo mpya wa dunia unaohamia ulimwengu wa malipo kwa njia ya mtandao (cashless economy). Kampuni ya simu nazo, kwa kuwa ni rahisi kutumia simu, ni vyema zikaiona fursa hii na kuitumia.
Elimu ya huduma hizo ni tatizo kubwa kwa wananchi wengi hasa tukizingatia kuwa theluthi moja ya Watanzania wote hawajui kusoma wala kuandika kama ilivyobainishwa hivi karibuni na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO).
Kimsingi kuna kila sababu kwa Tanzania kuangalia namna gani inaweza kufanya ili kuharakisha maendeleo nchini hasa katika sekta hii ya fedha.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa