Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Wakazi wa Zanzibar wakiitikia salamu wakati Katibu Mkuu wa Chama Cha
Mapinduzi(CCM), Abdulrahman Kinana alipokuwa akihutubia katika Viwanja
vya Kibandamaiti jana.
Mnadhimu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), Salmin Awadh
Salmin amesema wawakilishi wa CCM wanajiandaa kuwasilisha hoja binafsi
kwenye Baraza hilo ili kuwapa nafasi wananchi waulizwe iwapo wanataka
kuendelea na Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), au la.
Akihutubia mkutano wa hadhara wa chama hicho
ulioongozwa na Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana kwenye Viwanja vya
Kibandamaiti, Unguja jana, Salmin alisema wajumbe hao wamefikia hatua
hiyo kwa kuwa wanaona kwamba lengo na matumaini ya kuundwa kwake
yamefutika na hayana dalili njema katika siku za usoni.
Alisema ni vyema wananchi wakaulizwa kama bado wana hamu na mfumo huo au ule wa zamani urejeshwe.
“Kitendo cha viongozi tuliounda nao umoja wa
kitaifa kupinga Muungano na Mapinduzi ya Zanzibar hakivumiliki, tunaona
ipo haja kila upande ubaki na msimamo wake kuliko kujenga urafiki wa
mashaka,” alisema Salmin ambaye ni Mwakilishi wa Magomeni CCM.
Alimwomba Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein
kuunga mkono hoja hiyo itakapowasilishwa ili kutoa nafasi mpya ya
kidemokrasia kwa wananchi wake kujua kama wanataka mfumo wa sasa au wa
zamani.
Wazo hilo liliungwa mkono na Katibu wa Itikadi na
Uenezi wa CCM, Nape Nnauye ambaye alisema ni jambo muhimu kuitishwa kura
ya maoni ili wananchi wapate nafasi ya kuulizwa kama wanataka mfumo wa
Serikali iliyopo au la kabla ya kufanyika Uchaguzi Mkuu mwakani.
Kinana amshukia Maalim
Awali, Kinana alisema kwa miaka 20 tangu
kuanzishwa mfumo wa vyama vingi, Katibu Mkuu wa CUF, Seif Shariff Hamad
amekuwa akiwayumbisha Wazanzibari kutokana na tabia yake ya kubadilisha
ajenda za kisiasa na kutikisa misingi ya umoja wa kitaifa nchini.
Alisema tabia ya kiongozi huyo imekuwa haifahamiki
na haijulikani anatafuta jambo gani licha ya kuwa Makamu wa Kwanza wa
Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyoundwa mwaka 2010 na CCM na
CUF.
Alisema kwa msingi huo, tabia ya kiongozi huyo
mbali na kuonekana kutaka kuzorotesha misingi ya umoja wa kitaifa pia
imekuwa ikichafua siasa za Zanzibar na Muungano na kuwataka wananchi
kuwa macho hasa katika mjadala wa Katiba unaoendelea nchini.
“Tabia ya Maalim Seif haifahamiki, ni bingwa wa
kubadilisha ajenda za kisiasa mara kwa mara akiwayumbisha wananchi.
Tokea kuanzisha vyama vingi, ameshabadili ajenda zaidi ya 20, amewaacha
wananchi hawajui washike lipi na waamini jambo gani,” alisema.
Alisema Rasimu ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya
Muungano lazima ipatikane kwa njia ya amani na isiwe kichocheo cha watu
kung’oana macho au kutoana ngeu na kwamba mabadiliko ya katiba si
mwarobaini wa maendeleo akisema mataifa mengi yamewahi kuandika katiba
mpya na bado kuna kero za wananchi.
Aliwataka wabunge na wawakilishi wa CCM kukaa pamoja na kutafakari kwa kina jinsi ya kuondosha kero zinazolalamikiwa na wananchi wa Zanzibar na kuipa Zanzibar nafasi pana ili ijiimarishe kiuchumi.
Chanzo;Mwananchi
Aliwataka wabunge na wawakilishi wa CCM kukaa pamoja na kutafakari kwa kina jinsi ya kuondosha kero zinazolalamikiwa na wananchi wa Zanzibar na kuipa Zanzibar nafasi pana ili ijiimarishe kiuchumi.
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment