Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Ujio wa beki mpya wa Simba, Mrundi Butoyi
Hussein umewagawa viongozi wa Simba katika makundi mawili yanayopingana
juu ya usajili wake, ingawa kocha Patrick Phiri amesema aachiwe kazi
hiyo aifanye mwenyewe.
Butoyi yupo visiwani hapa akifanya majaribio,
ambapo viongozi wengi hasa kutoka kundi lenye ushawishi mkubwa la
Friends of Simba wakihitaji beki huyo asajiliwe huku wakitaka Mkenya
Donald Mosoti aondolewe katika kikosi chao kama alivyoomba hapo awali
kuvunja mkataba wake.
Hata hivyo, Phiri amekuwa mgumu wa kutoa uamuzi
wake juu ya wachezaji wake hao wawili Mosoti na Butoyi ingawa ni lazima
mmoja wao aondoke kwani sheria za usajili wa wachezaji wa kigeni
zinahitaji kila timu iwe na wachezaji watano tu wa kigeni.
Tayari Simba ina wachezaji wake watano wa kigeni
ambao ni Mganda Joseph Owino, Mkenya Raphael Kiongera, Warundi Amissi
Tambwe na Pierre Kwizera pamoja na Mosoti mwenye mkataba wa mwaka mmoja
na nusu kwani alisajiliwa dirisha dogo msimu uliopita.
Kazi ya kumsaka beki huyo kutoka timu ya Telecom
ya Djibouti ilifanywa na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Zacharia Hans
Poppe aliyefunga safari mpaka Kigali yalikokuwa yakifanyika mashindano
ya Kombe la Kagame baada ya Kamati hiyo kujadili na kukubaliana kwa
pamoja kuwa atafutwe beki mwingine haraka ili Mosoti aruhusiwe.
Jana Jumapili Simba ilicheza mechi yake ya
kirafiki dhidi ya Kilimani City, mechi iliyochezwa Uwanja wa Amaan na
kuhudhuriwa na baadhi ya viongozi wa Simba kwa lengo la kuangalia
kiwango cha Butoyi.
“Tutamsikiliza kocha (Phiri) anasemaje, lakini
tumeangalia kwa umakini uamuzi wa Mosoti wa kutaka kuondoka, si hilo tu
hata kiwango chake ndio maana tunataka kufanya marekebisho kabla ligi
haijaanza, hivyo uwezekano wa kumsajili Butoyi ni mkubwa ili kumpa
nafasi Mosoti ya kwenda anakotaka,” alisema kiongozi mmoja wa Friends of
Simba, hata hivyo baadhi ya wajumbe wa kamati ya usajili na kamati ya
utendaji ya Simba walipinga uamuzi huo kwa madai kuwa Mosoti anatakiwa
kupewa muda mpaka wakati wa dirisha dogo.
Mosoti aliliambia gazeti hili kuwa,“Kama
nilivyosema awali kuwa nilizungumza na viongozi wangu juu ya kuondoka,
lakini pia sioni kama kutakuwa na tatizo nikiondoka kwani wachezaji
waliopo Simba ni wazuri na wataisadia Simba kwa kiasi kikubwa tu.”
Kuhusu mkanganyiko wa wachezaji hao wawili, kocha
Phiri alisema, “Baada ya mechi kadhaa ndipo nitakuwa na jambo lolote la
kuzungumzia kuhusiana na wachezaji hao, kwani kwa muda niliokaa nao
mazoezini wote ni wazuri ila siwezi kuwapima kwa njia ya mazoezi pekee.”
Wakati huohuo, kiungo mpya wa Simba Mrundi, Pierre
Kwizera amesema kila nafasi katika kikosi chao kuna changamoto ya
kupata namba kwani timu ina wachezaji wengi ambao ni wazuri.
Kwizera alisema tangu kocha Phiri ametua Simba
kumekuwapo na mabadiliko makubwa katika kikosi chao kwani wachezaji
wanaonyesha viwango vya juu mazoezini.
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment