Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Jeshi la Polisi Zanzibar, limesema kazi ya kuchunguza kompyuta
mpakato ya waziri wa zamani wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, (SMZ),
Mansoor Yussuf Himid, aliyefunguliwa mashtaka matatu yakiwamo ya
kukamatwa na silaha ya moto na risasi 407, imekamilika.
Hata hivyo, limesema kuwa hakuna kitu kibaya kilichokutwa ndani yake.
Akizungumza na Mwananchi Jumamosi jana, Naibu
Mkurugenzi wa Upelelezi na Makosa ya Jinai Zanzibar, Kamishna Msaidizi
wa Polisi (DDCI), Salum Msangi, alisema kuwa kazi ya kuchunguza kompyuta
hiyo imefanyika kwa umakini mkubwa na wataalamu wa mawasiliano ya
mitandao wa jeshi hilo.
“Hakuna kitu kibaya tulichofanikiwa kukamata baada ya kukamilika kwa uchunguzi wake,”alisema DDCI Msangi.
Hata hivyo, alisema kwamba baada ya kuifungua na
kufanya upekuzi katika mfumo wa mtandao wa mawasiliano wa kompyuta hiyo
hakuna kitu chochote cha jinai walichogundua zaidi ya mawasiliano yake
binafsi.
Akifafanua zaidi alisema kwamba kazi ya mwisho
inayoendelea kufanywa na maofisa wa upelelezi ni kukamilisha ushahidi
katika kesi ya msingi na wakati wowote Mansoor atarejeshewa kompyuta
yake.
Kompyuta hiyo ilichukuliwa na polisi kwa uchunguzi
baada ya Mansoor kupekuliwa nyumbani kwake Chukwani Agosti 2 mwaka huu,
ambapo alipatikana na silaha ya moto na risasi 407, kinyume na Sheria
ya Silaha na Risasi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hata hivyo, DDCI Msangi alisema kwamba upelelezi
wa kesi bado haujakamilika, licha ya mshtakiwa kufikishwa mahakamani na
kusomewa mashtaka matatu.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa tena Agosti 28 mwaka huu.
Waziri huyo wa zamani yupo nje kwa kwa dhamana ya
masharti ya kutosafiri nje ya Zanzibar bila ya ruhusa ya mahakama,
kusalimisha hati ya kusafiria, pamoja na wadhamini wawili kwa bodi ya
shilingi milioni tano kila mmoja na fedha taslimu shilingi milioni tatu
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment