Home » » JUMUIYA YA WAZAZI CCM YALIA NA KUKITHIRI KWA UDHALILISHAJI WA KIJINSIA.

JUMUIYA YA WAZAZI CCM YALIA NA KUKITHIRI KWA UDHALILISHAJI WA KIJINSIA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na Is-haka Omar, Zanzibar.

JUMUIYA ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imekishauri Chama hicho kuiambia serikali iongeze nguvu katika kusimamia na kudhibiti vitendo vya udhalilishaji wa Kijinsia  wanavyofanyiwa Watoto na Wanawake ili watu wanaobainika kuhusika na matukio hayo wahukumiwe kisheria kwa mujibu wa ukubwa wa matukio wanayofanya.

Ushauri huo umetolewa na Katibu msaidizi idara ya Organazesheni ya Jumuiya hiyo, Simba Haji Mcha wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa kazi za jumuiya katika mwendelezo wa ziara ya Idara ya Organazesheni Afisi kuu ya CCM Zanzibar  iliyofanyika katika Afisi za Jumuiya hiyo Kikwajuni Mjini hapa.

Katibu huyo alivitaja vitendo kuwa ni pamoja na ubakaji, kulawiti, kunajisi na kupigwa na kutelekezwa kwa watoto na wanawake na kudai kuwa ni aibu kubwa kwa nchi ya Zanzibar yenye historia na sifa nzuri juu ya maadili na utamaduni wake mbele ya mataifa mengine.

Alisema Wananchi wamechoshwa na kufanyika kwa matukio hayo kila mara huku wahusika wa vitendo hivyo viovu hawachukuliwi hatua zinazostahiki kwa visingizio vya kutokamilika kwa ushahidi ama kupatiwa adhabu ndogo isiyolingana na ukubwa wa tukio husika.

Alieleza kwamba sio tu vitendo hivyo vinatia aibu nchi peke yake bali vinachangia kuharibu sifa za Chama na serikali kwa ujumla hivyo  taasisi husika waongeze juhudi katika kutafuta ufumbuzi wa kudumu juu ya kutatua tatizo hilo.

Katika taarifa hiyo, Katibu Simba alisema majukumu waliyopewa watekeleze kikanuni kuwa ni kusimamia suala la elimu, malezi, utamaduni, mazingira na uchumi mambo aliyoyaeleza kuwa  yanayotekelezwa kwa ufanisi mkubwa kwa lengo la kujenga jamii itakayoweza kukabiliana na kutatua changamoto mbali mbali za kimaisha.

“ Hali ya kisiasa ndani ya Jumuiya yetu ipo licha ya kuwepo na changamoto kadhaa zinazotafutiwa ufumbuzi kupitia vikao maalum vya afisi yetu kwa kufanya tathimini maelekezo ya utekelezaji wa majukumu ya jumuiya na mambo yote ya kuwahimiza watendaji wa mikoa na wilaya kusimamia jumuiya kwa mujibu wa kanuni na maelekezo yanayotoka chamani na  makao makuu jumuiya yetu.”, alifafanua Simba.

Alisema katika kusimamia elimu kwa watoto ili wawe na misingi imara ya kitaaluma  jumuiya inamiliki na kusimamia Vituo vya Chekechea pamoja na shule mbili za Sekondari na ufundi za Dole Unguja na Dodeani iliyopo Pemba, ambazo wanafunzi wake wamekuwa wakifaulu kwa kiwango kizuri.

Ameeleza kuwa kwa upande wa suala la malezi na utamaduni jumuiya imekuwa karibu na Wazazi na Walezi katika kuhamasisha na kuelekezana juu ya umuhimu wa malezi bora na athari ya mporomoko wa maadili katika jamii.

Pamoja na hayo alifafanua kuwa  jumuiya hiyo katika suala la kusimamia Mazingira imekuwa kuhamasisha upandaji wa miti na   kupiga vita vitendo vya uharibifu wa Mazingira vikiwemo uchimbaji wa mchanga holela na kukata miti ovyo hali inayosababisha ongezeko la athari za tabia nchi.

Akizungumza  Katibu wa Kamati Maalum ya Idara ya Organazesheni Afisi Kuu Zanzibar, Haji Mkema alieleza kuridhishwa kwake na utendaji na usimamizi wa majukumu mbali mbali ya kiutengaji na kiuongozi yaliyotekelezwa na jumuiya hiyo.

Aliikumbusha jumuiya hiyo kuwa ndio chombo kinachobeba na kulea wanachama wa rika mbalimbali hivyo wanatakiwa kutambua kuwa uhai wa Chama na jumuiya unaanzia kwa wanachama wenyewe.

Alisema lengo la ziara hiyo ni kukutana na Viongozi na Watendaji wa jumuiya hiyo ili kuwashukru, kubadilishana mawazo na kuona hali halisi ya utekelezaji wa shughuli za jumuiya na chama kwa ujumla.

“ Nyinyi ndio Wazazi na Walezi wetu na  hao Akina Baba, Akina Mama, Vijana na Watoto wote wapo chini ya malezi yenu hivyo mnatakiwa kuendelea kuwa mfano bora wa kusimamia kwa vitendo maslahi ya CCM ili tuendee kushinda kila uchaguzi na kushika dola”., alisema Mkema.

Aliitaka jumuiya hiyo kuhakikisha takwimu za wanachama wa jumuiya zinakuwa sahihi na zenye uhalisia ili kuwa na idadi halisi za wanachama halali watakaosimamia kazi na majukumu ya jumuiya na chama bila ya kuchoka.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo Zanzibar, Nagma Murtaza Giga aliipongeza Afisi kuu CCM kwa ushirikiano wao mzuri na jumuiya hiyo hatua inayoongeza kasi za kiutendaji kwa lengo la kufanikisha kikamilifu majukumu ya kisiasa ndani na nje ya Chama.

Giga alikiomba Chama kusaidia kutatua Changamoto zinazoikabili jumuiya hiyo katika suala la uendeshaji wa miradi ya jumuiya iliyopo Zanzibar, kwa lengo la kuhakisha wanatekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 inayohimiza falsafa ya siasa na uchumi ndani ya Chama na Jumuiya.

Aidha aliwapongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano Dkt.  John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kasi ya usimamizi mzuri wa shughuli za kiutendaji  ndani ya chama na katika serikali wanazoziongoza ambazo zimezaa matunda yanayowanufaisha wananchi.

Kwa upande wao Watendaji na Viongozi mbali mbali wa jumuiya hiyo wanaofanyia kazi Zanzibar, kwa nyakati tofauti wamekiomba Chama vitendo vya udanganyifu na rushwa katika Uchaguzi wa Chama na jumuiya unaorajiwa kufanyika mwaka 2017, ili kupata viongozi makini na wenye maadili mema.

Aidha  wamelalamikia suala la kuchelewa kwa utekelezaji wa baadhi ya mambo yanayojadiliwa katika vikao vya jumuiya hiyo ambayo hawapati mrejesho wake kwa wakati kutoka Makao Makuu ya Jumuiya, jambo linalochangia kukwama kwa baadhi ya shughuli za kitaasisi.

Wakati huo huo, Katibu Mkema alitembelea na kukagua miradi ya jumuiya hiyo ambayo ni Shule ya Sekondari na Ufundi pamoja na Chekechea zilizopo  katika Kijiji Cha Dole na kuona shughuli za uendeshaji wa miradi hiyo.
                                                                     

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa