RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Zanzibar imeweza kupata mafanikio
makubwa ya maendeleo lakini yamekuwa yakivizwa kutokana na kutokuwepo kwa takwimu
sahihi na zinazokwenda na wakati.
Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika
ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, MnaziMmoja Mjini Zanzibar wakati
akifungua Semina ya siku moja kwa Viongozi na Watendaji wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu Umuhimu wa Takwimu na Matumizi yake.
Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema
kuwa hakuna sababu ya kuyabeza maendeleo
makubwa yaliopatikana hapa nchini lakini kuna kila sababu ya kutatua changamoto
ya kutokuwepo kwa takwimu sahihi katika taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar.
Dk. Shein ambaye pia, alikuwa
Mwenyekitiwa Semina hiyo, alisema kuwa kutokana na hali hiyo ndio maana akaona
haja ya kuandaliwa mafunzo hayo ambayo yatasaidia kwa kiasi kikubwa kufikia
malengo yaliokusudiwa ambapo mwishoni yatakuja na maazimio ambayo hatimae
yatafanyiwa kazi.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa hakuna
jambo lolote la maendeleo linaloweza kufanyika na kufanikiwa bila ya kuwepo kwa
takwimu sahihi na ufanyaji tafiti huku akisisitiza kuwa upatikanaji wa takwimu
sahihi na kwa wakati ni msingi muhimu katika kupanga na kutekeleza mipango yote
ya maendeleo.
Kwa maelezo ya Dk. Shein alieleza kuwa juhudi
mbali mbali zimechukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutatua
changamoto hiyo ikiwa ni pamoja na kuunda Idara ya Sera na Utafiti, Sheria ya
Takwimu lakini bado changamoto hizo zimekuwepo, hivyo aliwataka washiriki wa Semina
hiyo kufuatilia kwa makini mafunzo hayo na hatimae kufanyiwa kazi ipasavyo.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa
kwa upande wa Takwimu Zanzibar imekuwa ikifanya vizuri na kutumia fursa hiyo
kutoa pongezi kwa Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa
pongezi kwa Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Abdulhamid Yahya Mzee,Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Ofisi ya Mtakwimu
Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana pamoja katika
kuandaa Semina hiyo.
Dk. Shein pia, alivutia na juhudi za
makusudi zilizochukuliwa na uongozi huo kwa
kuanza kutekeleza vizuri maagizo yake tisa aliyoyatoa siku ya tarehe 6 Januari
mwaka huu, wakati alipoweka jiwe la msingi kwenye jengo jipya la Ofisi ya
Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huko Mazizini Mjini
Zanzibar, na kusisitiza kuwa hiyo ndio kasi anayoitaka.
Nae Waziri wa Fedha na Mipango Dk. Khalid
Salum Mohammed alisema kuwa Semina hiyo yametokana na agizo lake alilolitoa
siku hiyo katika ufunguzi wa jengo jipya la Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Aidha, Dk. Khalid alisema kuwa mbali ya
agizo hilo pia, tayari wameshaanza kuyafanyia kazi maagizo mengine kati ya
maagizo tisa aliyoyatoa Rais likiwemo ujenzi wa Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa
Serikali huko Pemba ambapo tayari mchakato wake unaendelea na jengo hilo
linatarajiwa kujengwa huko Gombani katika jengo jipya la ghorofa la Wizara ya
Fedha na Mipango.
Pia, Dk. Khalid aliongezea kuwa katika
agizo la mafunzo kwa wafanyakazi wa Ofisi hiyo ya Mtakwimu Mkuu, tayari zoezi
hilo linaendelea na wafanyakazi wawili wamepatiwa nafasi za masomo maalum juu
ya kada hiyo ya takwimu na kwa kila mwaka kwa miaka mitatu ijayo mpango huo
utaendelezwa.
Katika mafunzo hayo mada mbali mbali
ziliwasilishwa zikiwemo Muhtasari wa Majukumu ya Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa
Serikali katika upatikanaji wa Takwimu na utekelezaji wake, Umuhimu wa Takwimu,
Hatua za uzalishaji na Matumizi yake, Takwimu za Sekta ya Kilimo, Takwimu za
Sekta ya Viwanda na Takwimu za sekta za Huduma.
Akitoa mada juu ya Muhtasari wa Majukumu
ya Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali katika upatikanaji wa Takwimu na
utekelezaji wake Bi Mayasa Mahfoudh Mwinyi alisema kuwa Ofisi hiyo ina jukumu
kubwa la kusimamia kikamilifu upatikanaji wa takwimu bora nchini.
Kwa maana kwamba takwimu zinazotolewa zinatakiwa
zikidhi vigezo vilivyowekwa vikiwemo usahihi, kukidhi vigezo katika ngazi
husika ziwe zinalingana na zinatolewa kwa wakati ili kukidhi haja ya watumiaji
wa takwimu hizo yakiwemo maitaji ya Taifa.
Sambamba na hayo, Bi Mayasa alisema kuwa
Ofisi hiyo imeweza kuwajengea uwezo kitaalamu wafanyakazi wake ili waweze
kutekeleza majuku yao kwa ufanisi zaidi ambapo jumla ya wafanyakazi 30
wamepatiwa mafunzo katika ngazi ya Shahada na Shahada ya Uzamili ndani ya
kipindi cha miaka 10 na wafanyakazi 150 wa Ofisi hiyo ambao wamepata mafunzo
mafupi mafupi.
Viongozi mbali mbali walihudhuria katika Semina
hiyo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi SeifAli Idd pamoja na
viongozi wengine na watendaji wa Serikali.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
0 comments:
Post a Comment