Home » » BALOZI SEIF AFUNGUA KINGAMANO LA VIJANA WA CCM WA VYUO VIKUU KATIKA KUADHIMISHA MIAKA 39 YA KUZALIWA KWA CCM

BALOZI SEIF AFUNGUA KINGAMANO LA VIJANA WA CCM WA VYUO VIKUU KATIKA KUADHIMISHA MIAKA 39 YA KUZALIWA KWA CCM

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
  Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi akisalimiana na Mwenyekiti wa Vijana wa CCM wa Vyuo Vikuu Zanzibar kwa ajili ya kulifungua kongamano la CCM kutimia miaka 39 hapo Bwawani Hoteli Mjini Zanzibar.
Balozi Seif pamoja na Viongozi wengine wa ngazi ya Juu ya CCM na shirikisho la Vyuo Vikuu Tanzania wakifuatilia mambo yaliyokuwa yakiendelea kwenye kongamano la kuadhimisha miaka 39 ya CCM ndani ya ukumbi wa Salama Bwawani.
Baadhi ya Vijana wa Chama cha Mapinduzi walioshiriki Kongamano ya maadhimisho ya kutimia miaka 39 ya Chama cha Mapinduzi.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Balozi Seif Ali Iddi akilifungua Kongamano ya maadhimisho ya kutimia miaka 39 ya Chama cha Mapinduzi. Picha na – OMPR – ZNZ.
       
NA Othman Khamis Ame, OMPR 
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba kazi kubwa iliyopo mbele kwa Vijana wa CCM wa Vyuo Vikuu ni kutafakari na kulipatia ufumbuzi tatizo la kupungua kwa ushindi wa Chama hicho ikilinganishwa na chaguzi nyengine zilizopita nyuma. 
Alisema Vijana hao wanapaswa kuelewa kazi kubwa ya chama cha siasa ni kushinda uchaguzi ili kushika Dola kama inavyoelezwa katika Katiba na kanuni za Chama cha Mapinduzi. 
Akilifungua Kongamano la Vijana wa CCM wa vyuo Vikuu kuadhimisha miaka 39 tangu kuzaliwa kwa CCM hapo katika Ukumbi wa Salama Bwawani Mjini Zanzibar Balozi Seif alisema Viongozi pamoja na Wanachama wa CCM wanataka kuona Chama kinaendelea kubakia kuwa kimbilio la Wanawake. 
Alisema Chama chochote kitakachojenga tabia ya kudharau kundi la Wanawake ambalo ndio kubwa katika Jamii hakitokuwa na nafasi ya kushinda uchaguzi kwa sasa na hata hapo baadaye. 
“ Wanawake ni zaidi ya nusu ya Watanzania. Sasa ukilidharau kundi hili maana yake umejidharau mwenyewe na dhambi hiyo kubwa ambapo isifikie wakati akatafutwa mchawi wa kulaumiw a”. Alisema Balozi Seif. 
Balozi Seif alilitaja kundi jengine kubwa la Vijana ambalo chama cha Siasa kinapaswa kuwa na Sera na mfumo bora utakaowavutia Vijana wengi ili kujitengenezea mazingira mazuri ya kushinda uchaguzi na huo ndio mtazamo wa Chama cha Mapinduzi. 
Alisema Chama kinategemea kazi hiyo ya kuwavutia Vijana kujiunga kwa wingi la Chama cha Mapinduzi itasimamiwa na kufanywa na Vijana hao wa CCM wa Vyuo Vikuu ambao changamoto inayowakabili kwa sasa ni kutoa mbinu za kutumia ili malengo yaliyokusudiwa yafikiwe mapema iwezekanavyo. 
Aliwashauri Vijana hao wa CCM wa Vyuo Vikuu kujizatiti zaidi katika ujenzi wa Chama chao kama walivyofanya Vijana Wasomi wa Chama cha zmani cha ASP wa Young African Social Union (YASU) ambao kazi yao kubwa ilikuwa kuwakusanya vijana kwa kuwapatia elimu nyakati za jioni. 
Balozi Seif alisema kundi la Vijana wa Afro Shirazy Party { Yasu } lilikuwa na mipango mizuri ya kujenga Chama chao na kupelekea kuanzisha Magazeti ya Kipanga na Tai pamoja na kujenga Jumba la ghorofa maarufu Yasu liliopo Mtaa wa Miembeni Mjini Zanzibar. 
Akizungumzia uimara wa Chama cha Mapinduzi katika kipindi cha miaka 39 iliyopita tokea kilipoasisiwa mwaka 1977 Balozi Seif alisema zipo faida nyingi zilizoimarika kupitia CCM akizitaja kuwa ni pamoja na uimarishaji wa Muungano, Uongozi wa pamoja kati ya pande mbili za Muungano huo , Uchumi pamoja na Demokrasia. 
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM alifahamisha kwamba historia ya Demokrasia Nchini Tanzania ikiandikwa haitokamilika bila ya kutoa nafasi ya pekee kwa CCM kutokana na juhudi zake za kufungua milango ya Demokrasia Nchini. 
Balozi Seif alisema Demokrasia madhubuti ndani ya CCM ndio iliyoanzisha Mjadala wa haja ya kuwa na mfumo wa vyama vingi vya Kisiasa na kupelekea kufunguliwa milango ya Demokrasia mwaka 1992. 
Alieleza kwamba ufunguzi huo wa milango ya Demokrasia Nchini chini ya Chama cha Mapinduzi umewezesha kuibuka kwa zaidi ya vyama 18 vya siasa Nchini Tanzania na hatimae kupata usajili wa kudumu kutoka msajili wa vyama vya Siasa Tanzania. 
“ Tofauti ya CCM na vyama vyengine nchini ni uimara wa demokrasia ndani ya chama chenyewe wakati vile vyengine vinazungumzia demokrasia kwenye majukwaa tuu ndani ya vyama vyenyewe hakuna kitu kama hicho ”. Alisema Balozi Seif. 
Kuhusu hali ya amani inayoendelea kuwepo Nchini Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya CCM Taifa alisema kwa vile Amani ni itikadi iliyoota mizizi ndani ya Chama cha Mapinduzi kila mfuasi wa chama hicho anatakiwa kuikumbatia kwa mahaba yake yote itikadi hiyo muhimu. 
Alisema Chama cha Mapinduzi katika uhai wake wote kimekuwa mstari wa mbele katika kuhubiri Amani na utulivu na kujiwekea sifa Kimataifa kikiendelea kuamini kwamba bila ya kuwepo amani Taifa kamwe halitaweza kuleta Maendeleo. 
Kwa vile Amani, Utulivu na Maendeleo ni kama watoto pacha Balozi Seif alitoa wito kwa Vijana hao wa Chama cha Mapinduzi kutoka Vyuo vikuu kujaribu wawezavyo kuitumia Taaluma yao katika kuhubiri amani. 
Alieleza kwamba Vijana hao wanapaswa kueneza itikadi hiyo katika maeneo mbali mbali nchini kwa kutumia nguvu zao zote wakibeba ujumbe wa Taasisi hiyo ya Kisiasa wa CCM ni Amani na Amani ni CCM. 
Alisisitiza na kutahadharisha kwamba Jamii imekuwa ikishuhudia kupitia vyombo mbali mbali vya Habari na Mitandao ya Kijamii jinsi machafuko ya Kisiasa yanavyozidi kusambaa katika sehemu mbali mbali Ulimwenguni. 
Alisema machafuko hayo yanayoleta majanga, maafa pamoja na fadhaa huacha mayatima na vizuka kadhaa . Hivyo ni vyema yakatumika kama mafunzo kwa upande wa Wananchi na wafuasi wa vyama vyote Nchini na kuwa tayari kuepukana nayo kwa gharama zozote zile. 
Akitoa Taarifa Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyuo Vikuu Nchini Tanzania Nd. Hamid Saleh Muhina alisema lengo la kuundwa kwa shirikisho hilo ni kuwaandaa Vijana katika mazingira ya kisasa ya sayansi na Teknoloji ili wajekuwa viongozi bora wa hapo baadaye. 
Nd. Hamid alisema mpango huo ndio njia pekee itakayoliwezesha Taifa kuwa na hazina kubwa ya vijana wasomi watakaokuwa na uwezo kamili wa kutekeleza majukumu yao katika mfumo wa mtandao wa mawasiliano ya kisasa. 
Akielezea suala la kufutwa kwa uchaguzi Mkuu Mwenyekiti huyo wa Shirikisho la Vyuo Vikuu Nchini Tanzania alisema Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar { ZEC } ilikuwa sahihi kufanya hivyo baada ya kubaini kasoro kadhaa zilizofanywa na baadhi ya watu waliosimamia Uchaguzi huo. 
Nd. Hamid alivitaka vyama vya siasa ambavyo bado havijaamua kushiriki uchaguzi wa marejeo kutafakari kwa makini maamuzi yao ili isije fikia wakati Wananchama wa wakawapotezea haki yao ya Kidemokrasia ya kuchagua Viongozi wanaowataka. 
Mapema Mwenyekiti wa Vijana wa CCM wa Vyuo Vikuu Zanzibar Nd. Khamis Kheir Ali alisema kwa niaba ya Umoja huo ameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kutekeleza vyema sera zake kiasi kwamba Jamii ya Watanzania wanaendelea kufaidika na Maendeleo yanayotandikwa. 
Nd. Kheir alitolea mfano Sekta ya Elimu ambayo kwa sasa imetoa afueni kwa Wananchi walio wengi hasa Vijijini kutokana na uamuzi wa makusudi wa Serikali kufuta ada anazowajibika Mzazi kuchangia sekta hiyo. 
Alisema wananchi wameshuhudia uimarishwaji wa miundo mbinu ya sekta ya elimu unaotoa fursa kwa wananfunzi wa sekondari kupata nafasi za kuendelea na taaluma zao katika vyuo vya elimu ya juu hapa hapa nchini. 
Washiriki hao wa Kongamano la maadhimisho ya kutimia miaka 39 ya Chama cha Mapinduzi wameuhakikishia Uongozi wa Juu wa Chama hicho kwamba mbali ya kusimamia uchaguzi wa marejeo ifikapo Tarehe 20 Mwezi wa Machi lakini pia watashiriki vyema kupiga kura kwenye uchaguzi huo ili kukamilisha haki yao ya Kidemokrasi.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa