Home » » MTANDAO UNAOHUSISHA WATOTO NA MAPENZI JINSIA MOJA WAFUATILIWA

MTANDAO UNAOHUSISHA WATOTO NA MAPENZI JINSIA MOJA WAFUATILIWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WIZARA ya Uwezeshaji Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto ya Zanzibar, imesema imeanza kuufuatilia mtandao uliokuwa ukiwahusisha vijana wenye umri wa miaka 16 na kuendelea, kufanya mapenzi ya jinsi moja Unguja na Pemba.
Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Msham Abdalla Khamis alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari, akieleza hali ya matukio ya vitendo vya udhalilishaji wa jinsi. Pia, alikuwa akieleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali kupambana na matukio ya aina hiyo ambayo yamekuwa tishio kwa maendeleo ya jamii visiwani humu.
Alisema kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na taasisi mbalimbali, ikiwemo za dini ya Kiislamu imebaini kuwepo kwa kundi la vijana wanaofanya mapenzi ya jinsi moja na kwamba hali ni mbaya zaidi katika kisiwa cha Pemba.
Khamis alisema, kitendo cha vijana kuanzia umri wa miaka 16 kujishughulisha na vitendo vya ngono ya jinsi moja ni kinyume na maadili ya taifa la Tanzania na hatari kwa vijana ambao ni tegemeo na nguvu kazi ya taifa kukosa nguvu za kazi, kwani watakuwa wameathirika na hali hiyo.
“Zipo taarifa tunazifanyia kazi kwa sasa ambazo ni kuongezeka kwa vitendo vya mapenzi ya jinsi moja kwa wanaume kwa wanaume kuanzia umri wa miaka 16 Unguja na Pemba. Madhara yake makubwa ni kuwa na vijana wasio na tija kwa taifa hapo baadaye,” alisema.
Alisema, matukio hayo yanachangiwa na kuporomoka kwa maadili ikiwemo vijana wengi hivi sasa kuiga utamaduni wa kigeni, kudanganywa kwa tamaa zilizopindukia ya anasa. Ofisa katika Wizara ya Uwezeshaji Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto, Halima Masheko alithibitisha kuwepo kwa taarifa hizo ambazo wizara imeanza kuchukuwa juhudi za kuutafuta mtandao unaojishughulisha na kuwaingiza vijana katika mapenzi ya jinsi moja.
Naye ofisa katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali huko Pemba, aliyekataa kutaja jina gazetini, alikiri kuwepo kwa wimbi la vijana wa kiume kujiingiza katika vitendo hivyo. Alisema, katika shule moja visiwani Pemba (hakuitaja), wanafunzi walidiriki kutaka wapenzi hao wa jinsi moja kutengewa darasa lao maalumu kutokana na kuonesha hadharani mahusiano yao na kuwakera wenzao.
Utafiti wa Tume ya Ukimwi ya Zanzibar (ZAC) umebaini kwamba kundi linalofanya mapenzi ya jinsi moja la wanaume kwa wanaume linaongoza kwa maambukizi ya ugonjwa huo Zanzibar kwa asilimia 12.
CHANZO; HABARI LEO.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa