Home » » SABABU ZA CUF KUJITOA ZANZIBAR ZAANIKWA.

SABABU ZA CUF KUJITOA ZANZIBAR ZAANIKWA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad.
Chama cha Wananchi (CUF), kimetangaza uamuzi wake wa kutoshiriki uchaguzi wa marudio Zanzibar, uliopangwa kufanyika Machi 20, mwaka huu, na kutoa sababu zilizokifanya kufikia uamuzi huo.
 
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Jecha Salum Jecha, alitangaza msimamo wa tume hiyo kuwa ni kurudia uchaguzi huo baada ya kubaini kuwapo kwa dosari katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana. 
 
Tamko hilo, lilitolewa jana na Mwenyekiti wa CUF, Dk. Twaha Tasilima, huku akisema sababu zilizowafanya kutoshiriki ni kwamba uchaguzi huo si halali kwa kuwa uchaguzi halali ulishafanyika Oktoba, 25, mwaka jana.
 
Alisema sababu nyingine kubwa  ni kutokana na matamko yote mawili ya Mwenyekiti wa ZEC, kutokuwa halali na kwenda kinyume cha Katiba ya Zanzibar na Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar Na. 11 ya 1984.
 
“Hakuna kifungu chochote cha Katiba ya Zanzibar au Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar, kinachotoa uwezo kwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar na hata kwa tume yenyewe kufuta uchaguzi au kuitisha uchaguzi wa marudio,” alisema Tasilima.
 
Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo, sababu nyingine ni kwamba  upande wa uchaguzi wa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani ulikamilika na washindi wote kupewa shahada za kuwathibitisha na kuwatambua kuwa washindi halali.
 
“Kwa upande wa uchaguzi wa Rais wa Zanzibar, alisema matokeo yalishabandikwa nje ya vituo vya majumuisho vya majimbo yote 54 na kwamba kilichokuwa kinaendelea baada ya hapo ni kuhakiki matokeo kutoka majimboni na kazi hiyo ilishakamilika kwa majimbo 40 na majimbo 31 yalishatangazwa kabla ya Jecha kutangaza kufuta uchaguzi huo,” alisema.
 
Alisema pia Baraza Kuu la Uongozi la CUF lilifikia uamuzi wa kususia uchaguzi huo kutokana na kutiwa moyo na taasisi na jumuiya zote za kimataifa na kikanda zikiwamo Jumuiya ya Madola, Umoja wa Ulaya (EU), Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
 
Pia alisema Marekani na Uingereza zimeonyesha msimamo wao wa kuungana na Wazanzibari na kutetea haki yao ya kidemokrasia na uamuzi halali uliofanya katika uchaguzi mkuu, uliomalizika mwaka jana.
 
WITO KWA WAZANZIBAR
Kikao hicho cha baraza kilichofanyika jana katika ofisi za Makao Makuu ya CUF, Buguruni jijini Dar es Salaam kwa saa nne, kiliazimia kuwa Wazanzibari wote wanaoipenda nchi yao na ambao wanaamini katika utawala wa sheria, demokrasia na kuheshimu Katiba na sheria za nchi kutoshiriki uchaguzi huo wa marudio.
 
Dk. Taslima alisema Wazanzibari wanapaswa kudai haki yao ya msingi ya uamuzi wa kupiga kura Oktoba 25, mwaka jana kwa amani.
 
Baraza hilo lililokuwa na ajenda moja pia lilijadili na kutolea uamuzi kauli ya  Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, kuandika barua ya kutaka vyama vya siasa kushiriki uchaguzi wa marudio.
 
“Baraza Kuu halikutarajia kama Jaji Mutungi angefanya kazi ya kutumikia maslahi ya watawala na kushindwa kukemea uovu wa kubaka demokrasia na haki za watu,” alisema.
 
Alisema pia wamesikitishwa na kitendo cha Rais Dk. John Magufuli, kukwepa dhamana na wajibu wake kama Mkuu wa Nchi, kuiacha njiani kazi aliyoianza ya kutafuta ufumbuzi wa uchaguzi huo.
 
“Baraza linamtaka Rais Magufuli kujitathmini na kujiuliza anajiweka vipi na kutoa taswira gani mbele ya macho ya Watanzania na jumuiya ya kimataifa kutokana na kutosimamia ahadi yake aliyoitoa mbele ya Watanzania wakati akilizindua Bunge jipya kwamba atafanya kazi na vyama vya CUF na CCM ili kutafuta ufumbuzi wa jambo hili,” alisema.
 
Pia alisema CUF inalaani matumizi ya nguvu kubwa ya vyombo vya ulinzi na usalama dhidi ya wananchi wasio na hatia na ambao wamekuwa watulivu, licha ya vitendo vingi vya uchokozi wa makusudi na hata mashambulizi ya hujuma dhidi yao yanayofanywa na makundi ya vijana wa CCM waliowekwa katika kambi kadhaa kisiwani Unguja.
 
Sambamba na hilo, waliiomba jumuiya ya kimataifa hasa taasisi zinazosimamia haki za binadamu na zinazopambana na makosa ya jinai kimataifa, ikiwamo Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC) kufanya uchunguzi wa kauli na matendo ya uhalifu, uvunjwaji mkubwa wa haki za binadamu na ubaguzi.
 
KAULI YA MAALIM SEIF
Akijibu maswali mbalimbali kutoka kwa waandishi wa habari jana, Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad,  alisema kususia uchaguzi huo kuna heri kuliko kufanya uchaguzi ambao wana uhakika CCM imejipanga kushinda.
 
Alisema CCM imejipanga kutumia vyombo vya dola kuhakikisha inapata ushindi, hivyo CUF kushiriki uchaguzi huo ni sawa na kujitia kitanzi na kuchinjwa shingo.
 
“Hatuwezi kurudia uchaguzi usiyo halali na kama kususia uchaguzi ni kuwapa uhalali wa kutawala hata tusiposhiriki ni lazima CCM kitashinda kwani tayari kiongozi mmoja alishatangaza kuwa baada ya upigaji kura kumalizika saa 10:00 jioni watatangaza matokeo yao saa 2:00, hii ina maana kuwa tayari wana mshindi na sisi tunaenda kushiriki haramu,” alisema.
 
Alisema pia kwa vyama vingine kushiriki uchaguzi huo, hakuwezi kuzuia azma ya serikali kumtangaza Dk. Ali Mohammed Shein wa CCM kuwa mshindi kwa kuwa vyama hivyo havina nguvu na kwamba hakuna chama kinaweza kupata zaidi ya kura 400.
 
SMZ YAWEKA MSIMAMO 
Wakati CUF ikitangaza uamuzi huo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inasema uchaguzi wa marudio uko pale pale kama ulivyopangwa.
 
Kadhalika, uamuzi wa Chama cha CUF kususia uchaguzi wa marudio umewagawa wanasiasa na wanaharakati visiwani Zanzibar.
Mgawanyiko huo umetokana na kuwepo wanaounga mkono msimamo wa CUF wa kususia uchaguzi wa marudio na wanaopiga azimio la Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kugomea uchaguzi uliyopagwa kufanyika Machi 20, mwaka huu.
 
Akizungumza na Nipashe mjini Zanzibar jana, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, alisema uchaguzi wa marudio utafanyika kama ulivyopangwa na Tume ya Uchaguzi  Zanzibar na kwamba  serikali inaendelea kukamilisha gharama za kufanikisha uchaguzi huo.
 
“Kama wao wamejitoa sawa lakini uchaguzi utafanyika kama ulivyopangwa kwa sababu suala la kushiriki uchaguzi au kutoshiriki ni la hiari kwa chama,” alisema.
 
Balozi Seif alisema ZEC ilifuta matokeo ya uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana,  baada ya kujiridhisha kuwa ulipoteza sifa na viwango vya kuwa uchaguzi huru na wa haki.
 
 Kwa upande wake, mwanasheria mkongwe wa Zanzibar, Awadhi Ali Said, alisema uamuzi wa CUF ni sahihi katika kulinda Katiba na misingi ya utawala bora.
 
Alisema kuwa uamuzi wa kufuta matokeo ya uchaguzi mkuu yalikuwa batili na kitendo cha kuingia katika uchaguzi sawa na kuhalalisha ubatili wake.
 
Awadhi alisema Jecha alifuta matokeo ya uchaguzi kibabe bila  kuzingatia matakwa ya Katibva na sheria ya uchaguzi ya Zanzibar na kwamba kitendo hicho kimeiingiza nchi katika sokomoko la kisiasa na mgogoro wa kikatiba. Alishauri hekima na busara kutumika badala ya kulazimisha kufanyika kwa uchaguzi huo.
 
Pia alisema kukosekana mpatanishi baada ya kufanyika kwa mazungumzo ya kutafuta muafaka wa mgogoro wa uchaguzi, ndilo chimbuko la  kukwama mazungumzo hayo.
 
Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Tadea, Juma Ali Katibu, ambaye alikuwa mgombea urais wa Zanzibar, alisema kama juhudi za kutafuta muafaka zimekwama, CCM na CUF wakaribishe wapatanishi kutoka nje.
 
Alisema Zanzibar inapita katika mazingira magumu ya kisiasa kwa kufanyika uchaguzi wa marudio kabla ya kupatikana kwa maridhiano baina ya pande mbili zinazovutana.
 
MSIMAMO WA CCM 
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai, alisema chama chake kimefunga mjadala wa malumbano ya uchaguzi na badala yake kinajitayarisha na uchaguzi wa marudio.
 
Alisema kuwa hatima ya Serikali ya Umoja wa kitaifa Zanzibar (SUK) itajulikana baada ya kukamilika kwa uchaguzi mkuu wa marudio na kuwataka watu kuacha kutabiri kifo cha serikali hiyo baada ya washirika pamoja kugoma kushiriki.
 
“Serikali ya Umoja wa Kitaifa si ya CCM na CUF. Chama  chochote kinaweza kuingia na kuunda serikali ya pamoja kama kitakidhi mashariti ya Katiba ya Zanzibar,” alisema Vuai.
 
Kuhusu CUF kususia uchaguzi huo, alisema hakuna madhara yoyote kutokana na vyama 14 ambavyo vilijitokeza katika uchaguzi wa awali  kukubali kushiriki.
 
Kuhusu kushiriki uchaguzi huo, Vuai alisema CCM imeamua kuingia katika uchaguzi wa marudio baada ya kujiridhisha kuwa uchaguzi wa Oktoba 25, mwaka jana, ulivurugwa na wasimamizi wa uchaguzi na si viongozi wa tume hiyo.
 
Alisema wasimamizi wa uchaguzi wa vituo, majimbo na wilaya ndiyo walivuruga uchaguzi mkuu na serikali inapaswa kuchukua hatua za kisheria.
 
Msimamo huo wa CCM unashabihiana na wa serikali uliotolewa jana Bungeni kwamba suala hilo limemalizika kwa kuwa tume imeshatangaza kuwa utarudiwa na tarehe ya kufanya hivyo imeshapangwa.
 
Katika msimamo wake huo, serikali ilitangaza kuwa mjadala huo umeshafungwa na kwamba hauwezi kujadiliwa tena ndani ya Bunge, hasa katika kipindi hiki ambacho wabunge wanajadili hotuba ya Rais Dk. John Magufuli.     
 
Huku CCM na serikali zikitoa msimamo huo, mwanasiasa mkongwe Hassan Nassor Moyo, alisema uamuzi uliofanywa na CUF ni mzito,  hivyo anahitaji muda kuangalia mwelekeo wa upepo wa kisiasa wa Zanzibar.
 
“Suala hili gumu kidogo. Niache  niangalie upepo wa siasa unavyokwenda kabla kulitolea maoni yake,” alisema Moyo ambaye ni Waziri wa kwanza Katiba ya Sheria baada ya kuasisiwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.
 
Mkurugenzi wa ZEC, Salum Kassim Ali, alipoulizwa, alisema yeye si msemaji wa Tume na kutaka atafutwe Jecha ambaye hakupatikana baada ya simu yake kuita mara kadhaa bila kupokewa au kujibu maswali kupitia ujumbe mfupi wa simu (sms).
 
Uamuzi wa CUF kujitoa katika uchaguzi umeibua mjadala mkali katika Manispaa ya Mji wa Zanzibar huku wafuasi wa CCM wakionekana katika mazingira ya furaha na wafuasi wa CUF wakijadili kwa umakini uamuzi wa Baraza kuu la Uongozi.
Imeandaliwa na Mary Geofrey, Dar  na Mwinyi sadallah, Zanzibar
  
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa