Home » » PONDA AIBUKIA UCHAGUZI WA ZANZIBAR

PONDA AIBUKIA UCHAGUZI WA ZANZIBAR

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
AKIZUNGUMZA kwa mara ya kwanza tangu atoke mahabusu, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Shehe Ponda Issa Ponda amemuomba Rais John Magufuli kutimiza ahadi yake ya kushughulikia hali ya kisiasa visiwani Zanzibar.
Ponda amemtaka Rais Magufuli kutekeleza ahadi yake aliyoitoa bungeni juu ya kufuatilia hatma ya hali ya kisiasa visiwani Zanzibar na kutoa tamko la yale yaliyofikiwa katika mazungumzo ya kutafuta suluhu yaliyokuwa yakihusisha pande mbili zinazovutana za Chama cha Wananchi (CUF) na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Rais achukue ahadi yake aliyoitoa bungeni, ana wajibu wa kuitekeleza kwa vitendo na ahakikishe mzozo huu anaupatia ufunbuzi bila ya kuitumbukiza Zanzibar kwenye dhiki na uhasama,” alisema Ponda.
Pia alisema vyombo vya usalama vilivyopo Zanzibar vipo kwa amri yake hivyo endapo patatokea jambo lolote kabla ya kumaliza mzozo wa kisiasa uliopo visiwani humo ni yeye atakayelaumiwa.
Ponda alisema wao kama Jumuiya na Taasisi za Kiislamu wanaunga mkono hatua za mwanzo zilizochukuliwa kunusuru hali ya kisiasa Zanzibar kwa kufanya mazungumzo baina ya vyama hasimu vya CUF na CCM pamoja na kuunga mkono ahadi ya Rais Magufuli ya kushughulikia mzozo huo aliyoitoa wakati akizindua Bunge.
Aidha, amehoji ukimya uliopo hadi sasa kwani Watanzania hawajapewa taarifa ya pamoja kutoka CCM na CUF kuhusu mazungumzo waliyofanya yameishia wapi na yapi wamekubaliana na yapi hawajakubaliana na nini hatima ya mazungumzo yao.
Shehe Ponda aliyekuwa pamoja na msemaji wa Shura ya Maimamu Tanzania, Shehe Rajabu Katimba, alikanusha taarifa iliyotolewa jana kuwa Kiongozi wa Uamsho, Shehe Farid Ahmad ameunga mkono uchaguzi huo wa marudio.
“Tumemtembelea Shehe Farid gerezani, lakini pia tulikutana na wanasheria wake pamoja na viongozi wa gereza kutaka kujua kama aliandika barua yoyote na si yeye wala mwanasheria au magereza waliothibitisha kufanya hivyo naye kutuomba kukanusha taarifa hizo na kusema hazina ukweli wowote,” alisema Shehe Ponda.
CHANZO : HABARI LEO.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa