WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,
George Simbachawene amevunja mkataba baina ya mwekezaji wa kigeni na
kijiji cha Chole wilayani Mafia.
Amechukua uamuzi huo kutokana na kijiji kutokuwa na haki ya kumiliki Mali Kale, ambazo kisheria zote humilikiwa na Serikali Kuu.
Mkataba uliovunjwa na Simbachawene ulikuwa ukihusu Kampuni ya Chole
Mjini Conservation and Development Company Ltd, inayomilikiwa na Jean
Devillies na mkewe, Ann Devillies na kijiji cha Chole.
Akizungumza na wakazi wa kijiji cha Chole kilichopo katika kata ya
Jibondo wilayani Mafia, Simbachawene alisema eneo la Mali Kale ambalo
zamani lilikaliwa na Waarabu na baadaye Wajerumani ni mali ya Serikali
Kuu na kwamba kijiji hakikuwa na nguvu ya kisheria ya kumiliki eneo
hilo.
Simbachawene aliongeza kuwa mara baada ya nchi kupata Uhuru, mali
kale zote zilichukuliwa na Serikali Kuu na kwamba kijiji bila
kushirikisha serikali kilikosa nguvu ya kisheria kumiliki eneo hilo.
“Mkataba huu ambao mwekezaji anaona ni mkataba sahihi kwake na
unamfanya kuhisi kuwa ana haki zote, unaonekana una tatizo kwa sababu
umeingiwa mwaka 2007 lakini kabla ya mwaka 2007 mwekezaji huyu alikuwa
na hati,” alisema.
Waziri huyo alisema kipengele cha 227 kinaeleza kuiwezesha kampuni
kupata hati miliki ya eneo kutoka kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili ya
eneo lote, ambalo kwa wakati huo lilikuwa tayari linamilikiwa na kampuni
hiyo.
Simbachawene alifafanua kuwa kipengele hicho, kina matatizo kwani
maana yake ni kuwa kijiji kinatakiwa kiiwezeshe kampuni kupata hati
wakati Mkataba huo unaandaliwa tayari kampuni hiyo ilikuwa na hati.
Kipengele kingine kilichokuwa na utata, kwa mujibu wa mkataba huo ni
kile cha 228 ambacho kinasema kutoruhusu mtu yeyote au kampuni au
taasisi yoyote bila makubaliano na kampuni isipokuwa kwa mkazi wa Chole.
Waziri Simbachawene alisema kuwa kipengele hicho, kinakiuka sheria za
nchi kwa kuzuia wawekezaji wengine kufanya biashara ya utalii katika
kijiji hicho. Hivyo, Waziri alisema kuwa kijiji hakikuwa na mamlaka ya
kuingia Mkataba na mwekezaji kwa ajili ya eneo la Mali Kale na hivyo
Mkataba huo ni batili na hauwezi kutambulika kisheria kama mwekezaji
huyo anavyoamini.
Waziri Simbachawene alisema kuwa Mkataba huo hauna nguvu ya kisheria
na hivyo haupo, na kwamba mwekezaji huyo kwa sasa hana mamlaka ya
kumiliki eneo hilo ambalo ni mali ya Serikali Kuu.
HABARI LEO
0 comments:
Post a Comment