TATIZO la uhaba wa vyombo vya usafiri kati ya Zanzibar na Tanzania
Bara ikiwemo boti zinazokwenda kwa kasi, kwa kiasi kikubwa kumechangia
kuwepo kwa tatizo la ulanguzi wa tiketi kwa abiria na kusababisha
usumbufu mkubwa.
Ulanguzi wa tiketi hizo umeshuhudiwa na Naibu Waziri wa Mawasiliano,
Ujenzi na Uchukuzi, Mohammed Ahmada wakati alipofanya ziara katika eneo
la bandari ya Malindi.
Tiketi moja ya boti zinazokwenda kwa kasi zinazomilikiwa na Kampuni
ya Azam Marine inayouzwa Sh 20,000 hupanda bei na kufikia Sh 30,000 hadi
40,000.
Ahmada, akizungumza jana alionesha kukerwa na tatizo hilo na kuahidi
kulifanyia kazi kwa sababu linaleta usumbufu mkubwa kwa wananchi,
wakiwemo kinamama na wazee.
Alisema ingawa tatizo hilo limechangiwa kwa kiasi kikubwa na ukosefu
wa vyombo vingi vinavyofanya safari kati ya Zanzibar na Tanzania Bara,
lakini isiwe sababu ya kupandisha bei kwa kiwango hicho na kusababisha
usumbufu mkubwa kwa wananchi wenye kipato cha chini.
Meneja wa Usafiri wa Kampuni ya Azam Marine, Ali Mohamed Abeid
alikiri kuwepo kwa tatizo la tiketi za magendo ambalo wamekuwa
wakipambana nalo kwa kiwango kikubwa.
0 comments:
Post a Comment