Home » » WANAOKWAMISHA MIRADI ZANZIBAR KUKIONA

WANAOKWAMISHA MIRADI ZANZIBAR KUKIONA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imetakiwa kutowafumbia macho watendaji wa taasisi wanaokwamisha au kuchelewesha miradi ya wawekezaji kiasi ya kuwavunja moyo.
Hayo yalisemwa na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wakati wakitoa maoni kuhusu mradi mkubwa wa uwekezaji katika sekta ya utalii huko Matemwe unaotekelezwa na Kampuni ya Penny Royal.
Mwakilishi wa Jimbo la Welezo, Hassan Khamis Hafidh alisema ni aibu kuona serikali imefungua milango kwa wawekezaji kuwekeza, lakini bado vipo vikwazo mbalimbali ambavyo ni chanzo cha kuwavunja moyo wawekezaji sawa na kuwepo dalili za rushwa.
Mratibu wa mradi huo, Saleh Mohammed Said alisema wanapambana na vikwazo mbalimbali katika utekelezaji wa mradi huo, ikiwemo mlolongo wa kodi na madai mbalimbali kutoka kwa wananchi ambayo hayana msingi na uhalali.
Alisema wameshindwa kupata vibali vya kazi kwa wafanyakazi wa kigeni, kitendo ambacho kimerudisha nyuma maendeleo ya ujenzi wa mradi huo kuanza kikamilifu.
“Hatujaridhishwa na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa kijiji cha utalii cha Matemwe kwa sababu ya urasimu mkubwa, ikiwamo milolongo ya kodi.....hadi sasa hatujapata kibali cha wafanyakazi wetu wa kigeni kufanya kazi Zanzibar,” alisema.
Aidha, alisema wamekuwa wakidai fidia mbali mbali kutoka kwa wanakijiji wa eneo hilo ambapo inaonesha wazi wazi kwamba wananchi hawajafahamu umuhimu wa mradi huo kwa maisha na maslahi ya wakazi wa kijiji hicho ikiwemo kuzalisha ajira.
Mkurugenzi Mkuu wa Mradi huo, Brian Thompson alisema, wanakusudia kujenga kijiji cha utalii cha mfano ambacho kitakuwa na huduma zote ikiwamo ya uwanja wa ndege utakaorahisisha watalii kufika hapo moja kwa moja. Aidha, alisema mradi huo unakusudia kutoa ajira kwa wananchi wa Zanzibar huku ukilenga wanakijiji cha Matemwe wapatao 1,500.
“Mradi huu umelenga kuongeza pato kwa Serikali katika Sekta ya utalii pamoja na kutoa ajira kwa wananchi wa Zanzibar,” alisema.
Spika wa Baraza la Wawakilishi, Zubeir Ali Maulid alisema, sekta ya utalii ndiyo tegemeo la taifa katika kuingiza fedha za kigeni na kuzalisha ajira kwa vijana kwa hivyo serikali na taasisi zake zinatakiwa kujenga mazingira mazuri yatakayowavutia wawekezaji kuwekeza.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa