MKE wa Rais wa Zanzibar
Mama Mwanamwema Shein amesema kuwa suala la udhalilishaji wa kijinsia, hasa kwa
wanawake na watoto limekuwa sugu katika jamii hivi sasa kutokana na kusikika
kila kukicha, hali ambayo haitoi picha
nzuri katika jamii.
Mama Shein aliyasema
hayo leo huko katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani wakati akifungua
Kongamano la siku moja lililozungumzia Unyanyasaji wa Wanawake na Watoto,
Kongamano ambalo limetayarishwa na Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Bint Saad.
Katika hotuba yake
alisema kuwa licha ya kuwepo kwa Kampeni
dhidi ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia iliyoanzishwa mwaka
2014, bado jamii ina wajibu wa kutafuta mbinu na mikakati zaidi hasa ya
kuelimisha ubaya wa vitendo vya udhalilishai wa kijinsia hasa kwa wanawake na
watoto.
Kutokana na hayo, Mama
Shein alitumia fursa hiyo kuipongeza Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti Bint
Saad kwa kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu wa
Saba pamoja na jitihada za taasisi nyengine katika kukabiliana na vitendo hivyo
vibaya.
“Tuna wajibu wa
kuchukua hatua za haraka kwani wagenga walisema ‘usipoziba ufa, utajenga
ukuta’, sote tuache muhali, tuchukue hatua ili tuepuke kujenga ukuta kwani ni
dhahiri kuwa vitendo vya udhalilishaji haviwezi kutupelekea kuwa na jamii bora
ya waungwana na wastaarabu wenye maadili mema’,alisema Mama Shein.
Aidha, Mama Shein
aliitaka jamii kuzilinda haki za watoto na kuwakinga na vitendo vya
udhalilishaji kwa kuziimarisha familia kwani familia zisizokuwa imara huvunjika
na kusababisha matatizo kwa watoto, hasa kwa kukosa malezi bora na haki zao
nyengine.
Alieleza kuwa baadhi
ya tafiti zilizofanywa hivi karibuni zinaonesha kuongezeka kwa idadi ya talaka
katika jamii sababu ambayo inatajwa kuwa husababisha watoto kukosa ulinzi wa watu
wabaya kupata fursa kuwadhalilisha.
Hivyo, Mama Shein
aliwataka wanandoa kuendelea kustahamiliana na kuwataka wazee wazidi kuzilinda
ndoa za vijana wao na kuwasisitiza umuhimu wa kuvumiliana na kusameheana ili
wajukuu wapate malezi bora huku akiwanasihi viongozi wa dini kuelimisha ubaya
na atahri za talaka.
Katika kukabiliana na
vitendo vya udhalilishaji hasa kwa watoto, Mama Shein alisema kuwa ni lazima
wazazi wawe mbele katika kuhakikisha watoto wanapata haki zao ikiwemo elimu na
kueleza kusikitishwa kwake kusikia kuwa katika jamii bado kuna wazazi
wanaowakatisha masomo watoto wao kwa ajili ya kuolewa.
Pamoja na hayo, Mama
Shein aliunga mkono kauli mbiu ya Kongamano hilo inayosema kwamba “Kina mama
tumesema unyanyasaji wa kijinsia sasa basi” na kusisitiza mashirikiano ya
pamoja katika kuhakikisha malengo ya kongamano hilo yanafikiwa.
Nae Waziri wa Kazi,
Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto Maudline Cyrus Castico alisema
kuwa Wizara yake kwa kushirikiana na taasisi zinazoshughulikia masuala ya
udhalilishaji wa wanawake na watoto inatekeleza wajibu wake kwa mashirikiano
makubwa na taasisi hizo zikiwemo za Serikali, zisizo za Kiserikali pamoja na
Mashirika ya Maendeleo.
Waziri Castico alisema
kuwa mikakati mbali mbali imekuwa ikitumiwa na taasisi za Serikali na zisizo za
Serikali katika kupambana na tatizo hilo ambapo Wizara yake kwa kushirikiana na
Wadau mbali mbali imetunga Sera, Sheria na Miongozo mbali mbali inayosimamia
utekelezaji wa mapambano hayo.
Alisema kuwa Serikali
katika uongozi wa Rais Dk. Shein haikukaa kimya katika kuhakikisha inatokomeza
vitendo hivyo na kwamba hatua na mikakati mbali mbali imewekwa katika kufikia
azma ya malengo yaliyowekwa na kueleza kuwa vitendo hivyo vilikuwepo tokea
zamani lakini vilikuwa havitolewi taarifa.
Nae Mwenyekiti wa
Taasisi ya Mwanaharakati Siti Bint Saad, Nasra Mohammed Hilal alieleza umuhimu
wa kushirikiana katika kupiga vita suala hilo na kusisitiza kuwa kongamano hilo
ni moja kati ya maagizo na maazimio ya Taasisi yake.
Mapema Mratibu wa Taasisi hiyo Aziza Saleh alisema kuwa Taasisi hiyo inaelewa fika ugumu
wa vita hivyo na iko tayari kushirikiana na taasisi zote zenye nia na lengo la
kupiga vita suala hilo la udhalilishaji wa kijinsia kwa kupitia kongamano hilo
litakalosaidia kujua ukubwa wa suala hilo na pia, litajadili katika kupata njia
muwafaka na hatua za kulitokomeza
kabisa.
Katika kongamano hilo
mada mbali mbali zimetolewa zinazohusiana na suala zima la udhalilishaji wa
wanawake na watoto.
Viongozi mbali mbali
walihudhuria katika Kongamano hilo wakiwemo Mawaziri, Manaibu Waziri, Naibu
Spika wa Baraza la Wawakilishi Mgeni Hassan Juma, Mkuu wa Mkoa wa Mjini
Magharibi Ayoub Mohamed, Mshauri wa Rais anayeshughulikia masuala ya Maendeleo
ya Wazee, Wanawake na Watoto Bi Zainab Omar pamoja na viongozi wengine wa
Serikali na vyama vya siasa na washiriki wengineo.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
0 comments:
Post a Comment