Home » » ZANZIBAR YAANZA KUTAFUTA MAFUTA

ZANZIBAR YAANZA KUTAFUTA MAFUTA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd akikata utepe kuashiria kuzindua kazi ya utafiti wa utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia Zanzibar kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume mjini Unguja jana. (Picha na Maelezo, Zanzibar).

KAZI ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia Zanzibar, imeanza rasmi jana kwa Kampuni ya Bell Geospace Enterprises Limited ya Uingereza, kufanya utafiti huo kwa niaba ya Kampuni ya Rak Gas ya Ras Khaimah.
Akizindua utafiti huo uliofanyika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume mjini Unguja jana, Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd alisema kwamba utafiti huo, unafungua milango katika rasilimali ya mafuta na gesi asilia.
“Kuna watu walikuwa wakisema kwamba Zanzibar hatutachimba mafuta, leo wananchi wenyewe mnashuhudia kazi inaanza…Zanzibar inaendesha utafiti wa kwanza kabisa kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta,” alisema Balozi Idd.
Alisema serikali haifanyi mambo kwa kubahatisha na kuwaasa wanasiasa kuacha kuwapotosha wananchi juu ya suala zima la utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia kwani suala hilo halihitaji ushabiki wa kisiasa.
Makamu wa Pili wa Rais alisema kwamba suala la mafuta na gesi asilia, sasa linasimamiwa Zanzibar moja kwa moja baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kufanya marekebisho ya Katiba na kuliondoa suala hilo katika orodha ya mambo ya Muungano.
Alieleza kuwa kazi hiyo ya utafiti wa mafuta na gesi asilia ni hatua muhimu katika uchimbaji wa mafuta ambapo inaweza kuchukua miaka mitano kukamilika kwake kwani ni jambo lenye kuhitaji muda, lakini yapo matumaini makubwa ya kufanikiwa kwa suala hilo.
“Tunawaomba wananchi wawe na utulivu, wasiwe na hofu yoyote wakati watakapoiona ndege hii maana itakuwa ikipitapita katika sehemu za bahari na nchi kavu… itapita chini sana, lakini utafiti unaofanywa hauna athari yoyote kwa binadamu na hata kwa wanyama na mimea,” alisema Balozi Idd.
Makamu huyo wa Pili wa Rais alisema kwa muda mrefu, serikali imekuwa na mazungumzo na Kampuni ya Rak Gas ya Ras Khaimah, ambayo mazungumzo hayo yamezaa matunda ya kuanza kwa kazi ya utafiti, ambapo pia kampuni hiyo imekuwa mshirika wa maendeleo wa Zanzibar.
Mtaalamu wa uchimbaji mafuta kutoka Kampuni ya RAK Gas ya Ras Khaimah, Dk Osama Abdelaal alisema kampuni wanatumaini makubwa ya kufanikiwa katika utafiti huo.
Kiongozi wa timu ya watafiti kutoka Kampuni ya Bell Geospace Enterprises Limited ya Uingereza, Stefan Kuna akitoa maelezo mafupi kuhusu kazi ya utafiti huo, alisema kwamba watatumia muda wa miezi mitatu kufanya utafiti huo Unguja na Pemba.
Mtaalamu huyo alisema ndege yao ya utafiti, itakuwa ikiruka kila siku mapema asubuhi na itakuwa angani kwa muda wa saa sita, wakitafiti maeneo yote ya nchi kavu ya visiwa Zanzibar vikubwa na vidogo pamoja na maeneo ya bahari iliyozunguka visiwa hivyo.
Kampuni hiyo ya kigeni inasaidiwa kazi na kampuni ya kizalendo ya Brunswick Zanzibar Limited, ambayo inahusika na shughuli za uombaji wa vibali kutoka serikalini kwa ajili ya ufanikishaji wa kazi ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia Zanzibar.
Kuanza kwa kazi ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia, kunaanza baada ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohammed Shein kutia saini Sheria ya Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia, Novemba mwaka jana.
Kutungwa kwa sheria hiyo kunatokana na masharti ya Kifungu cha Nne Sheria ya Mafuta na Gesi Asilia 2015 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inataja kwamba shughuli za uendeshaji wa mafuta na gesi asilia, utafanywa Zanzibar kwa kusimamia na kuendeshwa na taasisi kwa mujibu wa Sheria za Zanzibar.
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa