Home » » ELIMU ITOLEWE KWA WANANCHI ILI KUZUIA KASI YA MAAMBUKIZI MAPYA YA VVU WILAYANI MAFIA - MAMA SALMA KIKWETE‏

ELIMU ITOLEWE KWA WANANCHI ILI KUZUIA KASI YA MAAMBUKIZI MAPYA YA VVU WILAYANI MAFIA - MAMA SALMA KIKWETE‏


Na Anna Nkinda – Maelezo, Mafia
 Viongozi wa wilaya ya Mafia na wafanyakazi wa Idara ya afya wametakiwa kuhakikisha elimu ya maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) inatolewa kwa wananchi hii itawasaidia  kubadili tabia na kuepukana na ugonjwa huo ambao maambukizi yake yanazidi kuongezeka.

Mwito huo umetolewa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati alipotembelea Hospitali ya wilaya hiyo na kuongea  na viongozi wa Serikali pamoja na na watumishi wa sekta ya Afya.

Mama Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema takwimu zinaonyesha maambukizi mapya ya VVU katika wilaya hiyo  yanaongezeka  kila mwaka kutoka asilimia 2.2 kwa mwaka 2012 na kufikia asilimia 2.9 kwa mwaka 2014.

“Ni jukumu letu sote kuhakikisha  elimu inatolewa kwa wenyeji wa wilaya hii kuhusu maambukizi ya VVU, wananchi wajitokeze kwa wingi kupima kwa sababu huduma hii inapatikana bure katika zahanati 16 na dawa za kupunguza makali zinatolewa katika  zahanati 4”.

Binadamu ni kiumbe wa kipekee sana kwani Mwenyezi Mungu amempa akili ya kujua mema na mabaya, leo hii anakuja mgeni hujui mahali alikotoka unakubali kufanya naye mapenzi matokeo yake unapata ugonjwa wa Ukimwi usio na kinga wala tiba hapo ni kujitakia lazima hatua za makusudi ziweze kuchukuliwa ili kukabiliana na tatizo hili”, alisema Mama Kikwete.

Kuhusu changamoto ya  watumishi haswa wauguzi, wakunga na waganga katika wilaya hiyo aliwashauri viongozi hao kutafuta  njia za  kuwavutia wauguzi na waganga, ili wakifika wasiwe na tamaa ya kukimbilia katika wilaya au mikoa mengine.

Mwenyekiti huyo wa WAMA alisema, “Njia hizi siyo lazima ziwe za kuwapa fedha nyingi, bali kuwatafutia sehemu nzuri ya kukaa, na kuwapatia mazingira bora ya kazi ikiwemo, kuwepo kwa vifaa tiba na dawa. Mganga akimtibu mgonjwa kisha akapata nafuu  inamtosha  kuridhika na kusikia furaha moyoni. Hii peke yake ni motisha ya hali ya juu”.

Mama Kikwete pia aliwahimiza viongozi hao pamoja na watumishi wa sekta ya afya kuwahamasisha wananchi  ili wajiunge na  Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) kwani katika wilaya hiyo ni asilimia 27 tu ya wananchi ndiyo wamejiunga na huduma hiyo.

“Mfuko huu pamoja na mfuko wa Taifa wa bima ya Afya (NHIF) ni muhimu sana. Hakuna nchi duniani inayoendeshwa bila kuwa na bima ya Afya. Bima hizi hamtaziona umuhimu wake mpaka pale utakapopata dharura ya kuugua au kuuguliwa”, alisisitiza.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndekilo aliwataka wahudumu hao wa afya kuwanyenyekea na kuwatumikia wananchi kwa moyo wa uaminifu jambo ambalo litapunguza malalamiko kwani hakuna mjadala katika afya ya mtu.
Mhandisi  Ndekilo alisema kijiografia kisiwa cha Mafia kinatakiwa kujitegemea kwa mambo mengi na siyo kutegemea nje kama wananchi watapata huduma nzuri ya afya watatibiwa kisiwani humo na hivyo wagonjwa wa rufaa wa kwenda Hospitali ya Taifa ya Muhimbili watapungua.
 “Wadau wa Maendeleo  wanawapenda wanamafia na wako tayari kuwasaidia tutashirikiana kwa pamoja ili tuweze kuzitatua changamoto zinazowakabili kwani afya bora inaleta maendeleo”, alisema.

Kuhusu Katiba inayopendekezwa alisema Serikali imepeleka nakala za kutosha wilayani humo hivyo basi watenge muda wa kuisoma na kuielewa ili wakati ukifika wakaipigie kura.

Akisoma taarifa ya afya Mganga Mkuu wa wilaya Dkt. Credianus Mgimba alisema kuna zahanati 16 zinazotoa huduma za  uzazi na mtoto kati ya zahanati 18 zilizopo ambapo mbili ni za watu binafsi na hazitoi huduma ya afya ya uzazi na mtoto. Hakuna  kituo cha Afya ila Serikali imetenga eneo la ujenzi katika kijiji cha  Kironge.

Hospitali iko moja ambayo ni ya wilaya inavitanda 65 na wastani wa wagonjwa wa kulazwa kwa siku ni 55 katika wodi nne  na wagonjwa wa n je (OPD) 250.

Dkt. Mgimba alisema licha ya Hospitali ya wilaya kuwahudumia wananchi wapatao 50963  kati ya hao wanaume 26126  na wanawake 24837 kutoka visiwa nane vya Mafia pia inawahudumia  baadhi ya wananchi kutoka wilaya za Rufiji, Mkuranga na Kilwa.

Hii ni kutokana na jiografia ya bahari  na mito kwao ni salama na rahisi zaidi kusafiri haraka kwenda  Mafia kuliko kwenda kutibiwa  Hospitali zao za wilaya na hii huongeza gharama ya kuwahudumia kwani bajeti tutengwa kutokana na idadi ya wakazi.

“Hali ya maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi siyo ya kuridhisha kwani idadi ya wanaoishi na VVU inaongezeka. Kwa mujibu wa takwimu katika vituo vya kutolea huduma  kwa mwaka 2012 walikuwa wagonjwa 1072 sawa na asilimia 2.2, mwaka 2013 , wagonjwa 1378 sawa na silimia 2.7 na mwaka 2014 , wagonjwa 1498 sawa na asilimia 2.9”.

“Ongezeko hili linachangiwa na mwingiliano wa wageni toka toka nje ya wilaya na ongezeko la tabia hatarishi kwa maambukizi mapya ya VVU. Changamoto ni watu wengi kutojitokeza kupima kwa hiari  na unyanyapaa licha ya elimu hiyo kutolewa mara kwa mara  na huduma za upimaji kupatikana”, alisema Dkt. Mgimba.

Alizitaja changamoto zinazowakabili kuwa ni upungufu wa watumishi, upungufu wa dawa na vifaa tiba na mashine za kutolea huduma , kutokuwa na chanzo cha uhakika cha maji, uchakavu wa chumba cha kuhifadhia maiti na ukosefu wa jokofu, upungufu wa nyumba za watumishi na kutokuwa na usafiri wa dharula wenye uhakika wa kuwasafirisha wagonjwa nje ya kisiwa.

Dkt. Mgimba alisema , “Ili kukabiliana na changamoto hizo tumeweza kuwashawishi wazawa wenye sifa kwenda kusomea kada ya afya ili wakimaliza warudi na kufanya kazi katika mazingira waliyoyazoea, kuimarisha ukusanyaji wa fedha za uchangiaji wa huduma zinazotolewa Hospitalini na zahanati za Serikali, kufanya matengenezo ya mashine na ukarabati wa majengo kwa awamu kadri fedha zitakapopatikana.

Naye Mkuu wa wilaya hiyo Dkt. Nassor Himid ambaye ni daktari wa magonjwa ya wanawake alisema ili kukabiliana na upungufu wa madaktari atakuwa anafanya  kazi katika Hospitali hiyo kwa masaa mawili kuanzia saa mbili hadi saa nne asubuhi kila siku pale ambapo hatakuwa na  kazi nyingi ofisini.

Dkt. Himid alisema “Nimeongea na  wataalam kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili watakuja kutoa huduma kwa kipindi  fulani na kuondoka pia kukiwa na kazi ya upasuaji kwa magonjwa ya wanawake nitakuja kufanya kazi hiyo pamoja na kuwa mimi ni mkuu wa wilaya  bado taaluma yangu ya udaktari ipo palepale”,. 

Aidha Mbunge wa jimbo la Mafia Abdulkarim Hassan Shah alisema kuharibika kwa mashine za mionzi na Ultrasound katika Hospitali ya wilaya ni tatizo kubwa kwani ikitokea ajali hakuna vifaa wanalazimika kukodi ndege na kuwakimbiza wagonjwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa ajili ya matibabu na vipimo.

“Ajali nyingi zinazotokea huku ni za pikipiki na watu kudondoka kwenye minazi kwa kuwa mashine zimeharibika wafanyakazi wa Hospitali hii wanapata lawama nyingi na kwakuwa wako wachache ukilinganisha na idadi ya wagonjwa hata huduma zinachelewa. Kupatikana kwa vifaa kutasaidia kuachwa kulaumiwa na wagonjwa watapata huduma”, Mbunge Shah alisema.

Kutokana na tatizo la kuharibika kwa mashine za mionzi (X-Ray), Ultrasound na kutokuwa na genereta la dharula Hospitalini hapo Mjumbe wa Taasisi ya Maendeleo ya Kisiwa cha Mafia (MIDEF) Dkt. Ramadhan Dau ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) alisema MIDEF watawasiliana na wafadhili wao ili vifaa hivyo viweze kupatikana.

Dkt. Dau alisema, “Ninaamini ifikapo mwezi wa tano mwaka huu vifaa hivi vitakuwa vimepatikana kwani kukosekana kwa mashine za mionzi na ultrasound  kunawafanya wananchi kupata  tabu ya matibabu na kulazimika kuingia gharama ya  kusafiri kwenda nje ya kisiwa kupata  huduma hii”,.

Wakati huo huo Mama Kikwete alitembelea shule ya Sekondari ya Micheni nakuongea na wazazi, walimu na wanafunzi wa shule hiyo.Akiwataka wanafunzi kusoma kwa bidii na kujiepusha na vitendo vikatavyowapelekea kukatisha masomo yao ikiwemo kupata mimba katika umri mdogo na ugonjwa wa Ukimwi na kutotimiza ndoto za maisha yao.
Aliwahimiza wazazi na walimu kusimamia elimu ya watoto wao hii ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanakwenda shule na kuhudhuria masomo yao. Pia wasikubali kuwaacha wakakosa elimu kwa ajili ya ujauzito, wakapata magonjwa ya ngono, wakapoteza maisha na kuzaa katika umri mdogo.

Mama Kikwete alisisitiza, “Mnatakiwa   kuwa mfano wa  kuigwa, kutoa malezi na huduma rafiki na bora, kuepuka mila na desturi zinazochangia tabia hatarishi, kujenga na  kusimamia nidhamu na kuzungumza na watoto na kuwapa elimu ya afya na uzazi na stadi za maisha”.

Msisahau kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura ili muweze kuichagua katiba inayopendekezwa na kuwachagua viongozi wakati wa uchaguzi mkuu utakapofanyika mwishoni mwa mwaka huu pia wanawake jitokezeni kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi”.

Akiongea kwa niaba ya wanafunzi wenzake dada mkuu wa shule hiyo Nasara Khalifani ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha nne   alimkaribisha Mama Kikwete shuleni hapo na kuzitaja changamoto zinazowakabili kuwa ni  upungufu wa vifaa vya maabara, kutokuwa na umeme na kutokuwa na maktaba, upungufu wa vitabu vya masomo ya sanaa na upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi.

Mama Kikwete alikuwa  wilayani humo kwa ziara ya kikazi ya siku mbili na katika Hospitali ya wilaya aliwaahidi kuwapatia vitanda viwili vya kujifungulia, viatu vya kuvaa chumba cha upasuaji, kitanda cha kubebea wagonjwa wanaoingizwa chumba chumba cha upasuaji, kitanda cha upasuaji, mashine ya kutolea dawa za usingizi na katika shule ya Sekondari Micheni  aliwapatia wanafunzi zawadi ya shilingi laki tano.
Mwisho


        
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa