Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein
Mwanasheria Mkuu (AG) wa zamani Zanzibar, Othman
Masoud Othman, amesema Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein,
anapaswa kujiuzulu kwa sasa na Jaji Mkuu kuiongoza visiwa hivyo kwa
kuunda kamati maalum itakayochunguza uhalali wa kufutwa kwa matokeo ya
uchaguzi mkuu visiwani humo.
Aidha, amesema Rais Dk. John Magufuli anapaswa kuingilia kati
mgogoro uliopo visiwani humo, ili kuinusuru nchi kuingia katika mgongano
wa kisiasa.
Aliyasema hayo jana wakati wa kongamano la wazi juu ya changamoto
za kisheria zilizojitokeza baada ya kufutwa kwa uchaguzi mkuu wa
Zanzibar uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana, lililoandaliwa na Chama Cha
Wanasheria Tanganyika (TLS), jijini Dar es Salaam jana.
Alisema Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, anapaswa
kuingoza Zanzibar kwa sasa na kuunda tume huru itakayochunguza uhalali
wa kisheria uliosababisha kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi huo na
kusababisha mvutano wa kisiasa visiwani humo.
Alisema endapo kamati hiyo itabaini kuwa hakukuwa na uhalali wa
kufutwa kwa uchaguzi huo, waliohusika kufutwa watatakiwa kufikishwa
katika mikono ya sheria.
Naye mwanasheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu
(LHRC), Harold Sungusia, alisema changamoto zilizojitokeza wakati wa
uchaguzi mkuu bara ni nyingi mojawapo ni kutokuwa na maandalizi ya
kutosha kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
“Zaidi ya mikutano 172 ilifanyika nje ya muda uliopangwa, kwa
mujibu wa utafiti tuliofanya katika mikoa mitano ya Dar es Salaam,
Tabora, Arusha, Mbeya na Tanga, wanasisasa wengi hawakufuata sheria ya
muda,” alisema Sungusia.
Sababu nyingine ni lugha zilizotumika katika baadhi ya mikutano ya
kampeni haikuwa nzuri na kwamba wagombea wengi walitumia lugha za matusi
huku zaidi ya mikutano 188 iliyofanywa na wagombea ilikuwa na lugha za
matusi.
Alisema viashiria vya rushwa pia vilitawala katika uchaguzi huo,
ambapo zaidi ya mikutano 139 kulikuwa na viashiria vya rushwa na
changamoto nyingine waliyobaini ni ucheleweshwaji wa kutangaza matokeo
katika baadhi ya vituo vya kupigia kura.
Naye Wakili wa Kujitegemea, Fatma Karume, alisema ili kutojirudia
kwa kile kilichotokea Zanzibar, inapaswa kuwapo kwa mahakam huru na tume
ya uchaguzi huru.
Alisema bila ya kuwapo kwa vitu hivyo hali mbaya ya kisiasa visiwani humo inaweza kujirudia kila uchaguzi utakapofanyika.
Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Chama Cha Wananchi
CUF, Ismail Jussa, alisema hicho kinashikilia msimamo wake wa kutotaka
kurudia uchaguzi visiwani humo.
Alisema viongozi wa bara kujiweka pembeni katika mgogoro huo unaendelea visiwani humo kunaweza kuudhofisha muungano.
CHANZO:
NIPASHE.
0 comments:
Post a Comment