Home » » AG MASTAAFU: SHEIN ACHIA NGAZI.

AG MASTAAFU: SHEIN ACHIA NGAZI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein
Mwanasheria Mkuu (AG) wa zamani Zanzibar, Othman Masoud Othman, amesema Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, anapaswa kujiuzulu kwa sasa na Jaji Mkuu kuiongoza visiwa hivyo kwa kuunda kamati maalum itakayochunguza uhalali wa kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi mkuu visiwani humo.
 
Aidha, amesema Rais Dk. John Magufuli anapaswa kuingilia kati mgogoro uliopo visiwani humo, ili kuinusuru nchi kuingia katika mgongano wa kisiasa.
 
Aliyasema hayo jana wakati wa kongamano la wazi juu ya changamoto za kisheria zilizojitokeza baada ya kufutwa kwa uchaguzi mkuu wa Zanzibar uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana, lililoandaliwa na Chama Cha Wanasheria Tanganyika (TLS), jijini Dar es Salaam jana.
 
Alisema Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, anapaswa kuingoza Zanzibar kwa sasa na kuunda tume huru itakayochunguza uhalali wa kisheria uliosababisha kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi huo na kusababisha mvutano wa kisiasa visiwani humo.
 
Alisema endapo kamati hiyo itabaini kuwa hakukuwa na uhalali wa kufutwa kwa uchaguzi huo, waliohusika kufutwa watatakiwa kufikishwa katika mikono ya sheria.
 
Naye mwanasheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia, alisema changamoto zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mkuu bara ni nyingi mojawapo ni kutokuwa na maandalizi ya kutosha kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
“Zaidi ya mikutano 172 ilifanyika nje ya muda uliopangwa, kwa mujibu wa utafiti tuliofanya katika mikoa mitano ya Dar es Salaam, Tabora, Arusha, Mbeya na Tanga, wanasisasa wengi hawakufuata sheria ya muda,” alisema Sungusia.
 
Sababu nyingine ni lugha zilizotumika katika baadhi ya mikutano ya kampeni haikuwa nzuri na kwamba wagombea wengi walitumia lugha za matusi huku zaidi ya mikutano 188 iliyofanywa na wagombea ilikuwa na lugha za matusi.
 
Alisema viashiria vya rushwa pia vilitawala katika uchaguzi huo, ambapo zaidi ya mikutano 139 kulikuwa na viashiria vya rushwa na changamoto nyingine waliyobaini ni ucheleweshwaji wa kutangaza matokeo katika baadhi ya vituo vya kupigia kura.
 
Naye Wakili wa Kujitegemea, Fatma Karume, alisema ili kutojirudia kwa kile kilichotokea Zanzibar, inapaswa kuwapo kwa mahakam huru na tume ya uchaguzi huru.
 
Alisema bila ya kuwapo kwa vitu hivyo hali mbaya ya kisiasa visiwani humo inaweza kujirudia kila uchaguzi utakapofanyika.
Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Chama Cha Wananchi CUF, Ismail Jussa, alisema hicho kinashikilia msimamo wake wa kutotaka kurudia uchaguzi visiwani humo.
 
 Alisema viongozi wa bara kujiweka pembeni katika mgogoro huo unaendelea visiwani humo kunaweza kuudhofisha muungano.
CHANZO: NIPASHE.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa