Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mwenyekiti ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec), Jecha Salim Jecha.
Tangazo la Mwenyekiti ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar
(Zec), Jecha Salim Jecha, la tarehe ya marudio ya uchaguzi, limeliweka
Jeshi la Polisi na Vikosi vya Serikali ya Mapinduzi (SMZ) `mguu sawa'
kwa kuimarisha ulinzi mkali visiwani humu.
Chanzo cha kuimarishwa kwa ulinzi huo kumetokana na watu
wasiofahamika kusambaza vipeperushi vyenye ujumbe wa uvunjifu wa amani
katika maeneo tofauti ya Manispaa ya Mji wa Zanzibar.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Mkadam Khamis
Mkadam, alithibitisha kusambazwa kwa vipeperushi na polisi imeanza
kuwasaka watu hao.
Alisema vipeperushi vya uchochezi vilianza kuonekana mitaani muda
mfupi baada ya Zec kutangaza tarehe ya kurudiwa Uchaguzi Mkuu Machi 20,
mwaka huu.
Hata hivyo, Kamanda Mkadam alisema kuwa uchunguzi wa awali
umeonyesha moja kwa moja vipeperushi hivyo kuwa vina malengo ya kisiasa
kutokana na ujumbe wake na kuwataka wananchi kutoa taarifa za kuwafichua
watu hao.
“Tutahakikisha Zanzibar inakuwa shwari katika kipindi chote hasa
wakati huu wananchi wanasubiri uchaguzi wa marudio kufanyika Machi 20,
mwaka huu,” alisema Kamanda Mkadam.
Aidha, alisema kuwa kumekuwapo na viashiria vya uvunjifu wa amani
Zanzibar na kuwataka wananchi na wafuasi wa vyama vya siasa na viongozi
wao, kuhubiri amani na kuimarisha misingi ya umoja wa kitaifa.
“Jeshi la polisi halitamvumilia wala kumuonea huruma mtu yeyote
atakayebainika kuvuruga amani ya nchi,” alisisitiza Kamanda Mkadam.
Aidha, alisema ni kweli polisi walitumia mabomu ya vishindo juzi
kuwatawanya wananchi waliokuwa wamekusanyika katika mtaa wa Kundemba
kinyume cha sheria.
Alisema kuwa katika mkusanyiko huo, mtu mmoja alikamatwa na baada ya kumpekua alikutwa akiwa na dawa za kulevya.
“Jeshi lililazimika kufyatua bomu ili kuwatawanya vijana waliokuwa
katika eneo hilo na kurahisisha kumkamata kijana aliyekuwa na dawa za
kulevya,” alisema.
Askari wa doria wakiwa katika magari ya Jeshi la Polisi
waliochanganyikana na wa Vikosi vya SMZ, wamekuwa wakifanya doria katika
mitaa mbalimbali ya kuingia na kutoka Manispaa ya Mji wa Zanzibar kabla
ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa marudio.
CHANZO:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment