Home » » JAJI MKUU:MGOGORO Z'BAR UNGEAMULIWA KIMAHAKAMA.

JAJI MKUU:MGOGORO Z'BAR UNGEAMULIWA KIMAHAKAMA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.  
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu.
Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, amevunja ukimya kwa kusema kuwa alitegemea sana kuwa mgogoro wa kisiasa ulioibuka Zanzibar, baada ya kufutwa kwa uchaguzi mkuu wa mwaka jana ungepelekwa mahakamani.
 
Mbali na mgogoro huo uliotokana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salum Jecha, kufuta uchaguzi huo wa Oktoba 25 kwa madai ya kuwapo na kasoro nyingi, Jaji Makungu amesema suala hilo pamoja na mengine ya sheria na katiba yangewasilishwa mahakamani ili kupatiwa tafsiri sahihi ya vifungu vinavyobishaniwa.
 
Jaji Makungu alitoa kauli hiyo katika hafla ya kuwakabidhi vyeti mawakili wapya 47 na hakimu mmoja iliyofanyika katika Mahakama ya Zanzibar mjini hapa jana.
 
Alisema cha ajabu ni kuwa masualaa hayo yaliachiwa kujadiliwa mitaani na katika vyombo vya habari na kuviacha vyombo vya sheria hususan Mahakama.
 
“Ningelitoa wito kwenu pale ambapo masuala ya kikatiba na kisheria yanapojitokeza basi tuyawasilishe mahakamani kwa mujibu wa katiba ya nchi yetu. Mahakama ndicho chombo pekee kilichopewa mamlaka ya kisheria ya kutoa tafsiri ya kisheria,” alisema Jaji Makungu.
 
MGOGORO WA KISIASA ZANZIBAR
Mgogoro wa kisiasa uliibuka Oktoba 28, mwaka jana, baada ya Jecha kutangaza kufuta matokeo ya urais, uwakilishi na udiwani, akidai kuwa kulikuwapo na ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi katika maeneo kadhaa hususan ya Pemba.
 
Awali Oktoba 26, mgombea urais kupitia Chama cha wananchi (CUF) Malim Seif Sharif Hamad alitangaza kuwa alikuwa ameshinda katika uchaguzi huo kisha kuwasilisha fomu za matokeo Zec.
 
Tangazo la Jecha licha ya kupingwa na CUF ambayo ilitaka Maalim Seif atangazwe mshindi na kuapishwa, pia lilikosolewa na waangalizi wa kimataifa na wa ndani ambao ripoti zao za awali zilieleza kuwa uchaguzi huo ulikuwa mzuri kuliko wa mwaka 2010.
 
Vile vile, nchi kadhaa zikiwamo Marekani, Uingereza na Ireland ziliitaka Zec kuendelea kutangaza matokeo kwa kuwa ripoti za waangalizi zilionyesha kuwa ulikuwa uchaguzi huru na haki.
 
Hali hiyo ilisababisha kufanyika kwa mazungumzo ya kusaka suluhu yaliyowashirikisha Maalim Seif, mgombea wa CCM, Dk. Ali Mohamed Shein; Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi na marais wastaafu wa Zanzibar, Aman Abeid Karume, Ali Hassan mwinyi na Dk. Salmin Amour.
 
Mazungumzo hayo hata hivyo hayakupata suluhu na Zec kutangaza kuwa uchaguzi wa marudio utafanyika Machi 20, kwaka huu, ingawa CUF imetangaza kutoshiriki kwa maelezo kuwa sio uchaguzi halali kwani ulishafanyika.
 
Suala lingine ambalo limezua mgogoro ni ukomo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK). CUF na makundi mkadhaa wanasema uhaio wa serikali hiyo ulishamalizika wakati CCM wanasema kuwa Rais na viongozi wengine wa serikali hiyo bado wako madarakani hadi rais mpya atakapoapishwa.
 
WITO KWA MAWAKILI
 
Aliwataka mawakili kutokubali kuburuzwa na wanasiasa kwa kutekeleza malengo yao kwani mawakili ni watu muhimu sana mahakamani na katika jamii.
 
Alisema moja ya misingi ya demokrasia katika nchi ni kuwa na vyama vingi vya siasa na demokrasia ya mahakama ni kuwa na mawakili.
 
“Kesi kuwa mawakili kwa pande zote mbili na mawakili hao wakatoa hoja za kisheria kwa uweledi kunasaidia kufikia uamuzi sahihi, lakini kesi yenye wakili upande mmoja mara nyingi huonekana kama kesi ya upande mmoja,”  alisema.
 
Aidha, alisema kesi ambayo haina mawakili inakuwa nyepesi kwa hakimu au jaji kwa vile wahusika mara nyingi wanashindwa kuibua hoja za kisheria na wakati mwingine mahakama hulazimika kuibua hoja za kisheria.
 
“Hivi sasa tuna mawakili wengi, hivyo tujitokeze kuchukua kesi hizi na tuwasaidie wananchi ambao hawana uwezo mkubwa wa kifedha,” alisema.
 
Aliwataka mawakili hao kuienzi taaluma ya sheria na kutokubali  ichafuliwe na wanasiasa kwa maslahi yao kwani siasa na uchu wa fedha ndio maadui wawili wakubwa wanaoiandama taaluma hiyo.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar, Ibrahim Mzee Ibrahim, alisema kuongezeka kwa mawakili ni imani yake kwamba wananchi wanaohitaji wasaidizi wa sheria watapata fursa zaidi kuwakilishwa.
 
Naye Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Said Hassan, ambae aliwakilishwa na Wakili wa Serikali, Mtumwa Said Sandal, alisema kuwa sekta ya sheria inaendelea kukua siku hadi siku kutokana na kuongezeka wataalamu wa sheria.
 
Aliongeza kuwa mawakili wazingatie kuwa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kwa kuwa ndiyo iliyotoa mamlaka kwa Mahakama kuwa chombo pekee cha kikatiba chenye mamlaka ya kutekeleza utoaji wa haki.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa