Home » » Mitego yawekwa kuwanasa wafanyabiashara wanaoingiza bidhaa feki Zanzibar

Mitego yawekwa kuwanasa wafanyabiashara wanaoingiza bidhaa feki Zanzibar



Zanzibar
SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imesema haitamvumilia mfanyabiashara yeyote atakayebainika kuingiza bidhaa zilizopita muda wa matumizi au zilizo chini ya viwango zinazoweza kuathiri afya za wananchi au kuharibu mazingira.
Onyo hilo limetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Fatma Abdulhabib Ferej, huko ofisini kwake Migombani, alipokuwa akitoa taarifa rasmi kwa vyombo vya habari juu ya hatua ya serikali kuuharibu unga wa ngano tani 780 ambao uliingizwa Zanzibar ukiwa haufai kwa matumizi.
Waziri Ferej alisema serikali itaendelea kuchukua hatua za kuhakikisha bidhaa zote zinazoingizwa nchini zinakuwa na ubora na zinazingatia viwango vinavyostahiki ambazo hazitaweza kuleta madhara kiafya kwa watumiaji na kimazingira.
Akizungumzia unga wa ngano ulioharibiwa, Ferej alisema unga huo uliingizwa Zanzibar April mwaka jana na kampuni ya Bopar Enterprises ukitokea nchini Uturuki ukiwa kwenye makontena 30 ambapo baada ya kufanyiwa uchunguzi wa kawaida ulibainika haufai kutumiwa na binaadamu.
Alisema baadaye Bodi ya Chakula na Dawa ilipiga marufuku uingizaji na usambazaji wa unga huo na kuwaagiza wamiliki na wasafirishaji wa unga huo kuurejesha unakotoka haraka kwa mujibu wa sheria.
Hata hivyo, waziri alisema kulitokea mabishano baina ya wamiliki wa unga huo na kampuni iliyousafirisha iitwayo Mediterranean Shipping Company; mabishano ambayo yalipelekea unga huo kukaa kwa muda mrefu katika bandari ya Malindi.
Alieleza kuwa unga huo mbali na uchunguzi hata kwa macho ulikuwa na fangasi na funza ambapo pia ulianza kuhatarisha afya za wafanyakazi wa eneo la bandari ya Malindi na watumiaji wa eneo hilo.
Alisema baada ya serikali kuona mvutano huo unaendelea huku afya za wananchi zikiwa hatarini, iliingilia kati na ilishirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, ambapo iliamuliwa unga huo ukaharibiwe Tanzania Bara, kwa vile Zanzibar hakuna eneo la kutosha kwa kazi hiyo.
Waziri Ferej alisema mwezi Juni mwaka huu makontena 30 ya unga huo wa ngano yalipelekwa Dar es Salaam katika tanuri la kiwanda cha saruji cha TPCC kilichoko Tegeta, ambako unga huo ulichanganywa na mchanga na kuharibiwa.
“Kwa furaha naomba nichukue fursa hii kutoa taarifa kuwa unga mbovu tani 789 uliokuwa umeingizwa Zanzibar umeshaharibiwa,” alisema Waziri Ferej.
Alisema gharama zote za uteketezaji wa unga huo jumla ya sh 64,153,500 ambazo zimelipwa na kampuni iliyoleta unga huo Bopar Enterprises na Miditerranean Shipping Company Limited.
Chanzo: Tanzania Daima


0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa