Home » » BALOZI SEIF IDD ATAKA IKULU YA KIBWENI IKARABATIWE

BALOZI SEIF IDD ATAKA IKULU YA KIBWENI IKARABATIWE

Taasisi inayosimima uhifadhi na matengenezo ya nyumba za Serikali imeshauriwa  kuifanyia marekebisho yaliyosalia Ikulu ndogo ya Kibweni ili itumike vyema katika maadhimisho ya Sherehe za kutimia miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar  ya mwaka 1964.

Ushauri huo umetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif  Ali Iddi alipofanya ziara fupi ya kuikagua nyumba hiyo  iliyopo pembezoni mwa Makao Makuu ya Kikosi cha kuzuia Magendo Zanzibar { KMKM } Kibweni Wilaya ya Magharibi Mkoa wa Mjini Magharibi.

Balozi Seif ambaye ameridhika kiasi na hali halisi ya mazingira ya Ikulu hiyo alisema ni vyema   nyumba hiyo ya Serikali  ikapangiwa taratibu za kutumika badala ya kuachwa ikikaa bure .

Amesema Serikali katika kipindi kirefu imekuwa ikipokea wageni wa Kitaifa na Kimataifa wenye hadhi ya kuishi kwenye nyumba hiyo lakini wengi kati yao wanaishia kuwekwa  katika Hoteli  za Kitalii jambo ambalo linaweza kuepukwa.

Amewataka wahusika wa matengenezo ya nyumba za Serikali  kuhakikisha kwamba nyumba  hiyo { Ikulu } inakamilishwa hitilafu  ndogo ndogo zilizobakia ili iweze kuhudumia wageni watakaoalikwa kuhudhuria maadhimisho ya  sherehe za Mapinduzi kutimia Nusu Karne.

Hata hivyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  aliwapongeza wasimamizi wa Ikulu hiyo ya Kibweni kwa hatua  wanazozichukuwa katika kuihudumia nyumba hiyo kongwe.

Alisema mazingira bora yaliyopo hivi sasa kwenye nyumba hiyo  yanaruhusu kwa baadhi ya Mikutano na Kazi za  Viongozi Wakuu wa Serikali  kuzifanyiwa katika eneo hilo.

Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Ikulu Nd. Salum Maulid alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba tatizo liliopo hivi sasa katika nyumba hiyo ni  marekebisho ya jiko la kupikia pamoja na huduma ya maji ambayo haipatikani kikawaida.

Nd. Salum alisema huduma hiyo ya maji safi   hupatikana kwa nadra katika kipindi kirefu tatizo ambalo linahitaji kufanyiwa utafiti wa kina na kulitafutia ufumbuzi wa kudumu.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa