WAZANZIBARI
wametakiwa kuuenzi Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kutumia
vizuri fursa za kiuchumi ambazo ni kubwa, zitakazowakomboa vijana
kuachana na ajira za serikali. Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa na Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud wakati
akifungua Kongamano la Vijana wa Vyuo Vikuu vya Zanzibar kuhusu faida za
Muungano na hasara zake kama ukivunjika.
Alisema
Wazanzibari wanayo kila aina ya fursa katika Muungano uliopo sasa kwa
ajili ya kujiimarisha kiuchumi, kama wanavyotumia baadhi ya wananchi wa
Zanzibar waliopo Tanzania Bara, ambao wamewekeza katika miradi
mbalimbali, ikiwemo biashara.
“Faida
za Muungano uliopo sasa ni kubwa sana kuliko hasara za kuvunjika kwa
Muungano huo....Wazanzibari wanatakiwa kuzitumia fursa za kiuchumi
zilizopo sasa kwa ajili ya kujiendeleza,” alisema.
Akifafanua,
Aboud alisema Muungano uliopo sasa, una changamoto nyingi ikiwemo kero,
ambazo zimekuwa zikiyumbisha Muungano huo, lakini hata hivyo alisema
faida za Muungano ni kubwa.
Mwanafunzi
wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Ali Salim alikiri kuwepo
kwa fursa nyingi za Muungano ambapo Zanzibar inaweza kufaidika nazo,
lakini akasema Serikali zote mbili zinatakiwa kuziainisha kwa wananchi.
Kwa
mfano, alisema Wazanzibari wanao uwezo mkubwa wa kuwekeza sehemu yoyote
ya Jamhuri ya Muungano pamoja na kufanya biashara bila ya vikwazo kama
ilivyo sasa.
“Muungano
wa Tanganyika na Zanzibar faida zake ni kubwa zaidi kwa Zanzibar yenye
idadi ndogo ya watu wa wastani milioni moja na laki tatu kulitumia soko
kubwa la Tanzania Bara lenye zaidi ya watu milioni 43,” alisema.
Fatma
Mohamed mwanafunzi wa mwaka wa tatu Chuo Kikuu cha Tunguu, anayesomea
Sheria, alisema ukosefu wa elimu kuhusu faida za Muungano zinazopatikana
kwa pande mbili, zimewafanya baadhi ya watu kuona Muungano huo hauna
faida.
Kwa
mfano, alisema Wazanzibari wanafaidika na mikopo ya elimu ya juu
inayotolewa na Serikali mbili, ambapo mwanafunzi kutoka Zanzibar anaweza
kuomba mkopo wa elimu ya juu katika Bodi ya Mikopo ya Muungano.
“Hizi
fursa zilizopo kama Wazanzibari watazichangamkia vizuri, basi wanayo
nafasi kubwa ya kupiga hatua ya kiuchumi na maendeleo ikiwemo Sekta ya
Uwekezaji,” alisema.
Kongamano
hilo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu ni sehemu ya makongamano mbalimbali
yatakayoendeshwa na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, ambayo lengo lake
ni kutoa elimu zaidi kuhusu faida za Muungano. Muungano wa Tanganyika
na Zanzibar utafikisha miaka 50 mwakani. Uliasisiwa Aprili 26, mwaka
1964.
Chanzo;Habari Leo
0 comments:
Post a Comment