Home » » CHADEMA Z'BAR YAKOSOA UWANJA WA KITAIFA

CHADEMA Z'BAR YAKOSOA UWANJA WA KITAIFA

Zanzibar. Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar umedumaza dhana ya demokrasia ya vyama vingi na kuficha misingi ya utawala bora kutokana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kushindwa kuwachukulia hatua za kisheria viongozi waliohusika na ufisadi visiwani hapa.
Tamko hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Hamad Mussa Yussuf wakati akimnadi mgombea wa chama hicho Jimbo la Kiembesamaki, Hasimu Juma Issa katika mkutano wa hadhara wa kampeni uliofanyika katika Viwanja vya Kiembesamami kisiwani Unguja.
Hamad alisema, kuundwa kwa Serikali hiyo mwaka 2010 taswira ya upinzani wa kweli imepotea na kutoweka na sasa viongozi waliounda umoja huo wakionekana kutetea masilahi binafsi na kuwasahau wananchi wanaoishi kwa dhiki, shida na njaa.
Alisema hata Kamati za Baraza la Wawakilishi zinapofanya uchunguzi na kugundua vitendo vya ufisadi uliofanywa na baadhi ya watendaji na viongozi wa Serikali, hakuna hatua za kisheria zinazochukuliwa.
“Baraza la Wawakilishi Zanzibar limeshindwa kufuata nyayo za Bunge la Muungano ili kuchunguza mambo yanayolirudisha nyuma Taifa na kuyasimamia. Ni Baraza la Washirika wa vyama vya CCM na CUF, kuna ufisadi unaofumbiwa macho na vigogo hawajali maisha ya wanyonge,” alisema Hamad.
Miongoni mwa ripoti za ubadhirifu wa fedha za umma alizozitaja ni pamoja na Shirika la Umeme Zanzibar (Zeco), Baraza la Manispaa ya Mji wa Zanzibar (ZMC) mbali na ripoti za uchunguzi wa uuzaji wa majengo ya Serikali yaliouzwa kwa bei ya kutupwa kinyume na sheria.
Naibu Katibu Mkuu huyo wa Chadema Zanzibar alisema, vyama vya CCM na Cuf vimepoteza mwelekeo na wakati mwafaka umefika kwa wananchi wa Zanzibar kuamua kupatikana chama mbadala kitakachopigania masilahi ya wananchi na kuibana Serikali ndani ya nje ya vikao vya baraza.
Kwa upande wa mgombea uwakilishi, Hasim Juma Issa alisema iwapo wananchi watampa ridhaa ya kuwa mwakilishi atajenga hospitali itakayotoa huduma zote ikiwamo uzazi na upasuaji na kuwataka wananchi kumuunga mkono ili kuyafikia malengo yake.
Alisema hataogopa kuibana SMZ na kuongeza kasi ya uwekezaji katika sekta ya viwanda vidogovidogo na kuishangaa Serikali ya Mapinduzi ikikosa viwanda na kuongeza kasi ya uvuvi huku ikizungukwa na rasilimali ya bahari.
Zanzibar,hapa upinzania umekufa,wakubwa wanaitafuna nchi na umaskini unazidi kukithiri,vikataeni vyama vya CCM na Cuf,vimepoteza imani yake kwa jamii,”alisema Hasim.
Alisema pamoja na wawakilishi wa Cuf na CCM kuendelea kupokea ruzuku toka SMZ wameshindwa hata kujenga ofisi za majimbo pia fedha wanazopewa na Serikali wameshindwa kuzifanyia marejesho ya matumizi yake na kuahidi akishinda ataanzisha ofisi itakayofanya kazi hadi siku za mapumziko.
Pia alisema wananchi wengi wa Kiembesamaki hutumia maji ya visima na kuahidi ikiwa atashinda atahakikisha kunachimbwa visima vyenye maji matamu na kuweka mtandao wa usambazaji maji katika kila nyumba kwenye jimbo hilo.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa