Home » » SERIKALI ITATUE MATATIZO YA WAALIMU

SERIKALI ITATUE MATATIZO YA WAALIMU

Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa. 

Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa ametoa kauli ambayo bila shaka imewagusa wengi katika jamii.
Akinukuliwa na gazeti hili juzi alipokuwa akifungua Chuo cha Ualimu cha Benjamin Mkapa kilichopo Wilaya ya Wete kisiwani Pemba, Mzee Mkapa alitoa rai kwa Serikali iliyopo madarakani kuboresha masilahi ya walimu, jambo alilosema alishindwa kulitekeleza wakati wa utawala wake.
Japo amekiri kuwa masilahi ya walimu bado yapo chini na kwamba alifanya makosa kutowasaidia, huku akishauri utawala wa sasa kutoiga makosa yaliyofanywa na uongozi wake, sisi tunasema kauli hiyo ni ya mtu anayejikosha.
Katika nchi hii, walimu kama kada muhimu na nyeti kwa Taifa, wamekuwa wakiilalamikia Serikali kutowapa haki na stahili zao mbalimbali kwa miaka nenda rudi.
Kinachosikitisha ni kuwa badala ya kuzivalia njuga kero za walimu, Serikali karibu zote zimekuwa zikitumia nguvu za dola kufifisha harakati na juhudi za walimu kudai haki zao. Serikali zetu zimekuwa zikifanya mazungumzo ya mara kwa mara na baadhi ya kada za utumishi na hata kutekeleza ahadi inazotoa ili kupoza watumishi wake, lakini zimeshindwa kufanya hivyo kwa walimu.
Matokeo yake, walimu wanaendelea kuumia. Ukitoa udogo wa mishahara yao na kutolipwa hata zile stahili zao halali, mazingira ya kazi vituoni nayo yanazidi kuongeza ukubwa wa tatizo.
Tunaamini baadhi ya kero sugu za walimu kama vile malimbikizo ya mishahara kwa wanaopanda madaraja, malipo ya fedha za likizo na uhamisho zimo ndani ya uwezo wa Serikali ya sasa na hata iliyopita chini ya Mkapa.
Kama rasilimali za nchi zitagawanywa kwa haki na kufuata vipaumbele muhimu vya taifa, huku mianya ikizibwa ili watu wachache wasitapanye rasilimali hizo au kujinufaisha wao binafsi, Serikali zetu zina uwezo mkubwa wa kumaliza kero hizi.
Kinachoonekana ni kuwa Serikali hazijawa na azma madhubuti ya kumaliza kero hizi na nyinginezo zinazowakabili walimu wa Tanzania.
Kukiri makosa yanayoweza kuepukwa hakusaidii kumaliza vilio vya walimu au hata kukuza hadhi ya ualimu ambayo sasa imeshapotea.
Uzoefu unaonyesha viongozi wastaafu nchini wameanza kujenga tabia ya kukemea, kuelekeza na hata kuwakosoa wenzao pale wanapotoka madarakani. Mathalani wapo wanaokemea vitendo vya rushwa na ubadhirifu serikalini ilhali walishindwa kufanya hivyo walipokuwa madarakani tena katika nyadhifa kubwa.
Kama awamu ya tatu licha ya kutambua haja ya kuboresha masilahi ya walimu, ilishindwa kuwatimizia haja zao, hii inabaki kuwa changamoto kwa utawala wa sasa ili viongozi wake wasije kuendeleza ada iliyoanza kujengeka ya viongozi wastaafu kutoa udhuru wa kushindwa kutekeleza majukumu wakiwa nje ya ulingo wa uongozi.

Awamu ya nne chini ya Rais Jakaya Kikwete imebakiwa na miaka miwili kumaliza muhula wake. Vilio vya walimu vinaendelea, hadhi na heshima ya walimu na ualimu vimeshaporomoka siku nyingi. Rais na timu yake bado wana nafasi ya kurekebisha hali ya mambo.
Serikali yetu isijitue mzigo wa kero za kimasilahi na mazingira ya ufanyaji kazi zinazowakabili walimu nchini. Serikali ndio mwajiri wa walimu na mtatuzi wa mambo yanayowasibu.
Walimu ni nguzo na chachu ya maendeleo ya Taifa hili. Wataalamu na watendaji wanaotarajiwa kuiletea maendeleo nchi lazima wapitie mikononi mwa walimu. Kwa kuzingatia umuhimu wao, Serikali haina budi kuwajali walimu hasa kwa kuwatimizia masilahi yao.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa