Home » » Serikali kuleta meli ya kisasa Zanzibar

Serikali kuleta meli ya kisasa Zanzibar

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar ipo mbioni kuleta meli kubwa na ya kisasa itakayokuwa ikisafirisha abiria kutoka Unguja  kwenda Pemba ambayo itakuwa na garantii ya usalama.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Vuai Ali Vuai,  alitoa kauli hiyo mjini Unguja juzi alipohutubia mkutano wa tano wa hadhara wa kampeni za uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kiembesamaki uliofanyika viwanja vya Kisima mbaazi, Kiembesamaki.
Akimnadi mgombea nafasi ya uwakilishi wa jimbo hilo kupitia CCM, Mahmoud Thabit Kombo, aliwataka wananchi kukiunga mkono chama hicho ili kuendelea kuwaletea maendeleo na kuimarisha Muungano ambao sasa unadumu kwa miaka zaidi ya 50.
Alisema katika kuzingatia sera, ilani na kanuni za chama, tayari serikali imeshaagiza meli kubwa na ya kisasa ambayo itakuwa ikichukua abiria wengi na kwa wakati katika kufanya safari zake Unguja na Pemba.
“Meli ipo njiani, na itawasili muda wowote kuanzia sasa. Itakuwa mkombozi kwa wananchi wa visiwa hivi ambapo watapata chombo chenye garantii katika usafiri wa majini,” alisema Vuai.
Mgombea wa uwakilishi wa jimbo hilo, Mahmoud Thabit Kombo, alipongeza wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kwenye mkutano huo na kuwaomba kumpa kura za ndiyo kwenye uchaguzi utakaofanyika Februari 2.
Mahmoud alisema atahakikisha anasimamia sera na Ilani ya CCM katika kufikia malengo yaliyokusudiwa ikiwemo kuwatetea wananchi kwenye Baraza la Wawakilishi.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa