Home » » Serikali tatu homa yapanda Z’anzibar

Serikali tatu homa yapanda Z’anzibar

WAKATI viongozi wakuu wa serikali wakiwa katika mchakato wa kuteua wabunge 201 wa Bunge la Katiba, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Magharibi, Yussuf Mohamed Yussuf, amesema mfumo wa serikali tatu kama utapitishwa uhai wa muungano utabaki shakani.
Mwenyekiti huyo wa CCM mkoa, alibainisha hayo jana kwenye mkutano wa hadhara wa kampeni za Jimbo la Kiembesamaki uliofanyika uwanja wa Garden mjini Unguja wakati akimdadi mgombea wa chama hicho, Mahmoud Thabit Kombo.
Alisema maisha ya Watanganyika na Wazanzibari yanategemeana kulingana na miingiliano ya kihistoria na mlingano wa maisha ukifanana na mabadiliko ya mfumo na ujio wa serikali tatu huenda ukawa hatari na balaa jipya nchini.
Alisema watu waliotoa maoni ya kutaka muungano wa mkataba hawakufikia malengo yao na kwamba pendekezo la Tume ya Mabadiliko ya Katiba, linalotaka  mfumo wa serikali tatu  lisishangiliwe kama ushabiki wa Simba na Yanga.
“Wananchi msikubali kupelekwa puta, CCM haitapepesa macho wala masikio yake kuafiki mfumo  mpya, tunajua una hatari na majanga, watakaopata shida ni wananchi wanyonge, zitazameni  adha zilizopo hivi sasa  Libya, Syria, Sudan Kusini, ” alisema.
Alieleza kutokana na vyanzo haba vya kiuchumi vilivyopo Zanzibar, serikali ya tatu itakuwa ni vigumu kuigharamia na kwamba ukitaka kujua Zanzibar inaitegemea Tanzania Bara kiuchumi aliwataka wakaangalie wasafiri katika bandari  ya Malindi kutoka Bara wakibeba vikapu vya mchele, mbatata na nyanya kutoka Tanganyika.
Aidha, mwenykiti huyo wa CCM aliwataka wananchi kutowasikiliza viongozi wa CUF akiwemo Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba na Katibu Mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad, wanaoshabikia mabadiliko ya mfumo huo kwa kufikiria  kushika madaraka na masilahi binafsi.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa