Home » » CCM Z'bar: kauli ya CUF inasikitisha

CCM Z'bar: kauli ya CUF inasikitisha

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, kimedai kimesikitishwa na kauli za uchochezi zilizotolewa na Chama cha Wananchi (CUF), kuhusu uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kiembesamaki, uliofanyika Februari 2 mwaka huu, visiwani humo.
Katibu wa Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya Taifa Zanzibar kutoka Idara ya Oganaizesheni, Bw. Haji Mkema Haji, aliyasema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari.
Alisema kitendo cha CUF kudai uchaguzi huo haukuwa huru na haki, kinaonesha chama hicho hakijakomaa kisiasa ambapo kauli hiyo, haileti taswira nzuri kwa Zanzibar.
"CCM imesikitishwa na taarifa hii ya uchochezi, upotoshaji mkubwa kwa jamii iliyotolewa na viongozi wa CUF kwa waandishi wa habari," alisema Bw. Haji.
Aliongeza kuwa, jimbo hilo ni ngome ya CCM na si mara ya kwanza kwa CUF kulalamika na kutoa madai kama hayo jambo ambalo linaonesha hawajakomaa kisiasa.
Bw. Haji alisema chama chao kimeridhishwa na uchaguzi huo pamoja na kuwapongeza wakazi wa jimbo hilo kwa kumchagua Bw. Mahmoud Thabit Kombo kushinda kuwa mwakilishi wao.
Alisema hawakutarajia kusikia kauli kama hizo hasa wakati huu ambao Zanzibar ipo katika muundo wa Serikali ya Umoja wa kitaifa ili kumaliza siasa za chuki, uhasama na uzushi.
Aliwataka viongozi wa CUF kuacha kutoa malalamiko yasiyo na maana kwani kufanya hivyo ni kurudisha siasa za chuki ambazo hivi sasa hazina nafasi tena.
Wiki iliyopita, CUF ilimuomba Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein kuifuta Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), na kudai imeshindwa kusimamia vyema chaguzi mbalimbali visiwani humo.
Mkurugenzi wa Habari, Uenezi, Haki za Binadamu na Mawasiliano ya Umma wa CUF Zanzibar, Bw. Salim Bimani alisema chama hicho hakijaridhishwa na mwenendo wa ZEC ambayo imekuwa ikishindwa kuendesha chaguzi kwa misingi ya haki na uhuru.

Chanzo;Majira

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa