Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Sakata la Mwenyekiti wa Chama cha National League for Democracy
(NLD), Dk Emmanuel Makaidi kudaiwa kufanya njama zilizofanikisha yeye
na mkewe kuteuliwa wajumbe wa Bunge la Katiba, limechukuwa sura mpya
baada ya kiongozi wa chama hicho Zanzibar kujiuzulu na kujivua
uanachama.
Akitangaza uamuzi wa kuachana na chama hicho juzi,
Naibu Katibu Mkuu NLD Zanzibar, Khamis Haji Mussa alisema ameshindwa
kuvumilia kitendo hicho alichodai kinadhalilisha chama.
“Kwa hiari yangu nimeamua kujiuzulu uanachama na
kuacha wadhifa niliokuwa nao ndani ya NLD, jina zuri la tawi la Ustawi
wa Kitaifa wa Demokrasia ni nadharia tu, vitendo vyake ni udikteta na
ubabe... nashauriana na wanasheria kuona kama kuna kesi ya kufunguliwa,”
alisema Mussa.
Hatua hiyo imekuja siku chache baada ya NLD
Zanzibar pia kutoa tamko la kumtaka Rais Jakaya Kikwete kufuta uteuzi
huo, kwa madai walioteuliwa kutoka chama hicho ni mtu na mkewe hivyo
kukosa sura ya Muungano.
Mussa alisema ameshindwa kuvumilia kwa sababu
kitendo hicho kinadhalilisha chama na kinaashiria ukosefu wa misingi ya
uwazi na uadilifu.
Alisema amefikia uamuzi huo kutokana na madai
kwamba Dk Makaidi ameonyesha waziwazi anaiongoza NLD kwa ubinafsi,
ubaguzi na kuitenga Zanzibar katika uwakilishi wa Bunge la Katiba. Mussa
alisema Dk Makaidi amejidhihirisha ni mbaguzi na anaweza kuligawa taifa
kwa misingi ya Uzanzibari na Utanganyika, ikiwa siku moja atabahatika
kupewa dhamana.
Alisema utetezi uliotolewa na Dk Makaidi umekosa
nguvu ya hoja, zaidi ametumia umwamba unaoweza kuvipaka matope vyama
vingine vya siasa.
Katika utetezi wake, Dk Makaidi alisema NLD
Zanzibar walichelewa kupeleka majina kwa Rais wa Zanziba na kwamba,
kuteuliwa kwa mkewe hakuna matatizo kwa sababu ana sifa zinazotakiwa.
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment