Home » » MWAKILISHI AMMWAGIA SIFA RAIS DK. SHEIN.

MWAKILISHI AMMWAGIA SIFA RAIS DK. SHEIN.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein.
Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi, Hamza Hassan Juma, amempongeza Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein (pichani), kwa kuongoza nchi katika misingi ya demokrasia na kudumisha hali ya mani na usalama.
 
 Mjumbe huyo ambaye pia ni mwakilishi wa Jimbo la Kwamtipura (CCM), alitoa pongezi hizo wakati akichangia bajeti ya makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Rais Ikulu na Utawala Bora kwa mwaka 2015/2016.
 
 Alisema historia inaonyesha kwamba katika miaka ya nyuma iliyopita kipindi kama hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, nchi huwa ipo kwenye mtafaruku na vitendo vya uvunjifu wa amani.
 
Alisema katika uongozi wa awamu ya saba ya Dk. Shein amedhibiti hali hiyo na wananchi wanaishi kwa amani na usalama hasa katika kipindi hiki cha kukaribia uchaguzi mkuu. 
 
“Kwa kweli Dk. Shein anahitaji pongezi kwa kudumisha amani na anastahiki kuendelea tena kipindi chake cha pili cha kuongoza nchi hii,” alisema.
 
 Aidha, alisema licha ya Rais wa Zanzibar kufanikiwa katika kudumisha amani na usalama, lakini pia amedhibiti magendo ya karafuu na kupandisha bei ya zao hilo.
 
 Alieleza kuwa wananchi wa Pemba wamenufaika mno na kilimo cha zao la karafuu kutokana na zao hilo kuwa na tija likilinganishwa na miaka iliyopita. 
 
“Baadhi ya wananchi kisiwani Pemba wanaojishughulisha na kilimo cha karafuu wamenufaika lakini cha kushangaza hadi leo baadhi ya wananchi hao hawaweki fedha zao benki jambo ambalo ni hatari,” alisema.
 
 Aliwashauri wakulima hao wa karafuu kuweka fedha zao benki ili kutowapa mwanya wahalifu ambao hawana nia njema.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa