Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge.
Bunge la 11 limeweka historia ya aina yake baada ya
zaidi ya askari 50 kuingia ndani ya ukumbi na kuwatoa kwa kuwabeba
wabunge wa upinzani kutokana na kukataa amri ya Mwenyekiti wa Bunge,
Andrew Chenge, ya kuwataka watoke kwa hiari.
Chanzo cha tukio hilo ni kutokana na kauli ya serikali kwamba
Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), halitarusha moja kwa moja vikao
vya Bunge, jambo lililopigwa tangu kwenye kikao cha asubuhi na
kusababisha kiahirishwe.
Baadaye, baada bunge kurejea jioni na mwenyekiti kusoma uamuzi wa
kamati ya uongozi, wabunge wa upinzani walianza kuomba mwongozo.
Baada ya wabunge kadhaa kuomba mwongozo na wengi zaidi kuendelea
kujitokeza, Chenge aliwataja baadhi ya wabunge wa upinzani na kuwataka
waende nje kwa madai kuwa walikuwa wanafanya fujo, jambo lililosababisha
wenzao wote kusimama na kupinga amri hiyo.
Baada ya bunge kuahirishwa kwa dakika 10, zaidi ya polisi 50 na
wengine wa usalama wa taifa pamoja na askari kanzu, waliingia ndani ya
ukumbi wa bunge na kuwataka wabunge wote wa upinzani watoke ndani ya
ukumbi wa Bunge.
Hatua hiyo ilipingwa na wabunge hao, na kuanza kubishana kwa
takribani dakika 30 na hata askari walipoingia baadhi yao walianza
kuzozana nao. Hali ilipozidi kuwa mbaya, wabunge wanaume walivua tai
zao na kuendelea kubishana na wenzao.
Mbunge wa kwanza kuanza kukunjwa na askari hao ni wa Kilombero,
Peter Lijualikali, ambaye alishikwa na askari wa kikosi cha kutuliza
ghasia (FFU) na kutolewa kwenye kiti chake mpaka eneo inapowekwa siwa.
Wabunge wengine walivyoona hivyo, waliingilia kati na kumtoa huku
mbunge huyo akivua koti lake na kutunishiana misuli na askari hao.
Wabunge wengine waliorushiana ngumi na askari ni Halima Mdee (Kawe), Mwita Waitara (Ukonga) na John Heche (Tarime Vijijini).
Heche kwa upande wake alidai kuwa, askari hao walimpiga mkononi na
kitu kizito na alipokwenda hospitalini aliambiwa arudi kesho kwa ajili
ya uchunguzi zaidi.
Baada ya kutoka katika ukumbi wa Bunge, Mbunge wa Viti Maalumu,
Sabrina Sungura, alianza kuangua kilio akisema amedhalilishwa kwa
kuvuliwa nguo na askari hao. Alisema alivuliwa hijabu yake na kuibiwa
cheni na hereni zake.
Mbunge wa Liwale, Zuberi Kuchauka, alidaiwa kupigwa na kuumizwa
vibaya hali iliyosababisha apumzishwe kwenye zahanati ya Bunge wakati
Mbunge wa Micheweni, Juma Kombo, akidai kupigwa na kuvuliwa nguo.
Katika tukio hilo lililodumu kwa takriban dakika 40, wakiwa katika
ukumbi wa Bunge, askari mmoja alionekana kuwarushia wabunge maneno
makali.
“Nakwambia uheshimiwa wako huko huko, mimi hapa nitakuchapa sasa hivi,” alisikika askari huyo akisema maneno hayo.
Mdee alisema licha ya kichapo walichopata wabunge wengi wakiwa ndani ya ukumbi wa Bunge, pia walipigwa walipotolewa nje.
“Ukishatoka pale ukumbini kabla hujafika nje, kuna eneo ambalo watu
hawaoni ndipo kulikuwa na askari wengi wanapiga watu,” alisema.
Mbwa watumika
Katika mlango wa kutoka nje ya ukumbi huo, kulikuwa idadi kubwa kubwa ya askari wengine wakiwa na mbwa.
Askari hao walifunga mageti ya kwenda kwenye ukumbi huo pamoja na
ule wa Pius Msekwa, hali iliyofanya waandishi wa habari kushindwa kwenda
eneo walilokuwa wakitokea askari hao.
Waandishi watimuliwa
Baada ya hali kuwa mbaya zaidi kwenye ukumbi wa Bunge, maofisa wa
usalama wa taifa na watumishi wa Bunge nje ya ukumbi waliwakataza
waandishi kupiga picha.
Hata wale walioonekana kujaribu kupiga picha kwa kutumia simu, walinyang'anywa na maofisa wa usalama wa taifa na kuzifuta.
Kauli ya Bunge
Baada ya Bunge la jioni kurejea, Chenge alilieleza Bunge kuwa
Kamati ya Uongozi imekaa na kukubaliana kuwa Mwenyekiti wa Bunge alikuwa
sahihi alipokataa kuahirisha mkutano wa Bunge ili kauli ya Nape
ijadiliwe.
Alisema kamati hiyo pia imeona hakuna haki ya bunge iliyovunjwa kwa
mujibu wa haki, kinga na madaraka ya bunge, hivyo hoja ya kujadili
hotuba ya Rais iendelee kama ilivyokuwa imepangwa.
“Endapo kuna mbunge ambaye hataridhika na uamuzi huu, ni haki yake
kutumia kanuni kuwasilisha malalamiko yake kwa Katibu wa Bunge,” alisema
Chenge.
Baada ya kauli hiyo, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu
Lissu, aliomba mwongozo kwa kuhoji kwa nini suala hilo limejadiliwa na
Kamati ya Uongozi badala ya ile ya kanuni au kiti cha Spika. Chenge
alimjibu kuwa hakuna kanuni iliyovunjwa kwa hatua iliyochukuliwa.
Baada ya jibu hilo, Mbunge wa Babati Mjini pia wa Chadema, Paulina
Gekul, aliomba mwongozi kwa kutumia kanuni ya 49 (2), ambayo inakataza
kauli za mawaziri zinazotolewa bungeni zisizue mjadala.
Akijibu hoja hiyo, Chenge alisema: “Wakati namjibu Zitto nilisema
kama yeye anaona kauli yake imeibua mjadala ambao kanuni haziruhusu,
ndiyo msingi huo ambao nimesema alete huku.
Kanuni ya 52 (2) ambayo hoja hii ilitolewa na waziri mkuu jana,
huwezi tu ukaisitisha kwa namna hiyo, ndiyo maana nasema tuheshimu
kanuni hizi, nawasihi sana tuendelee na mjadala.”
Heche naye aliomba mwongozo na kusema kutorusha matangazo hayo moja
kwa moja ni kuvunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano, ibara ya 18,
inayozungumzia uhuru wa kupata habari na kutoa, na Chenge kusema kwa
jinsi ambavyo kanuni zinamruhusu atatoa mwongozo huo baadaye.
Baada ya jibu hilo, wabunge wengi zaidi wa upinzani walisimama
kutaka kupewa mwongozo na kiti, hali ambayo ilisababisha wenzao wa CCM
kuwaambia watoke nje.
Baada ya kelele kuzidi, Chenge aliyekuwa amepokea kikaratasi kutoka
kwa mmoja wa wasaidiza wake, alisoma majina ya Lissu, Ester Bulaya
(Bunda Mjini), Godbless Lema (Arusha Mjini) na Gekul na kuwataka watoke
nje ya ukumbi wa Bunge.
Hali hiyo ilifanya wenzao waanze kuzomea zaidi, hatua iliyomfanya Chenge ahairishe Bunge na kuamuru askari waingine kuwatoa.
KIKAO CHA ASUBUHI
Zilikuwa dakika 25 kwa Chenge, kukalia kiti cha Spika kwa mara ya
kwanza akiwa mwenyekiti wa Bunge, zilizowasha moto ndani chombo hicho
cha kutunga sheria pale hoja ya serikali ya kuachana na matangazo ya
moja kwa moja yanayorushwa na TBC, ilipowachefua wapinzani na
kusababisha kikao cha asubuhi kuvunjika.
Hali ya hewa bungeni ilichafuka baada ya Waziri wa Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, kutoa kauli ya serikali juu ya
TCB kutorusha matangazo ya moja kwa moja ya majadiliano ndani ya Bunge
kwa kile alichosema ni gharama kubwa kwa shirika hilo.
Alisema TBC ilianza kurusha matangazo hayo mwaka 2005 na kwamba
kabla ya hapo ilikuwa ikiyarekodi na kisha kuyarusha usiku kwenye
kipindi kilichoitwa ‘leo katika bunge’ kipindi alichosema kilikuwa
kikionyesha mambo muhimu yaliyotokea bungeni.
Alisema kwa sasa gharama za kurusha matangazo hayo zimepanda na
kufikia Sh. bilioni 4.2 kwa mwaka kwa mikutano minne ya Bunge, hivyo TBC
itakuwa hairushi tena matangazo na badala yake itakuwa inarekodi na
usiku kurusha vitu muhimu vilivyotokea kwa muda wa saa moja.
Baada ya kauli hiyo, hali ya hewa ilibadilika baada ya wabunge wa upinzani kusimama kutaka mwongozo wa spika.
Mbunge aliyeanza kusimama ni Zitto Kabwe wa Kigoma Mjini (ACT-
Wazalendo), ambaye alisimama kwa kutumia Kanuni ya 69 inayohusu
kuahirishwa kwa Bunge.
Chenge alimtaka Zitto aketi kwa maelezo kwamba kwa utamaduni wa Bunge, kauli za mawaziri zikishatolewa huwa hazijadiliwi.
Hali hiyo ilifanya kuwapo kwa kurushiana maneno kati ya wabunge wa
upinzani na kiti cha spika kwa upande mmoja na wabunge wa CCM wakirusha
maneno kwa wabunge wa upinzani.
Baada ya Chenge kushikilia kauli yake hiyo, Halima Mdee alisimama na kumwambia: “mbona una papara, si usikilize?”
Malumbano hayo yaliendelea mpaka pale Zitto alipokubali kusoma
kanuni hiyo na vifungu vyake viwili kama alivyoelekezwa na kiti kisha
kutoa hoja yake na kusema TBC si shirika la kibiashara na kutorusha
matangazo hayo ni kuwanyima wananchi fursa.
“Hotuba ya Rais tunayoijadili ilionyeshwa moja kwa moja, iweje
muhimili wa Bunge unapoijadili isionyeshwe moja kwa moja ili wabunge
wajadili na watoe maazimio,” alisema Zitto.
Ndipo Chenge aliposimama na kusema: “Nimemsikiliza kwa makini Zitto
kwa hoja yake ambayo msingi wake unaanzia Kanuni ya 49 inayohusu kauli
za mawaziri.
“Kwa mujibu wa mazoea yetu kauli za mawaziri hazijadiliwi bungeni
lakini hilo halizuii mbunge kuleta hoja binafsi kupitia katibu kwa
taratibu ambazo zimewekwa.
“Uamuzi wangu kwamba kama Zitto unaona kuna umuhimu wa hoja hizo
kuletwa, naomba ulete taarifa hiyo kwa taratibu hizo. Uamuzi wangu ni
kwamba kuahirisha mjada wa Rais haitakuwa uendeshaji bora wa shughuli za
Bunge. Naagiza meza tuendelee.”
Kauli hiyo ilionekana kuwakera zaidi wabunge wa upinzani ambao
walisimama kwa wingi na kuanza kusema lazima hoja ya Zitto isikilizwe
huku wakirushiana maneno.
Kutokana na hali hiyo, Chenge alisimama tena na kuwaambia wabunge
hao kuwa kwa mujibu wa Kanuni za Bunge, kiti cha spika hakiwezi kupewa
taarifa kama ambavyo baadhi ya wabunge walikuwa wakiomba.
Baada ya kauli hiyo, majibizano yalihama na kuwa kati ya Chenge na Halima Mdee.
Halima: Mwenyekiti hoja kuhusu haki za Bunge.
Change: Halima nakusihi uketi.
Halima: Hoja kuhusu haki za Bunge
Chenge: Nakusihi uketi
Halima : Naomba unisikileze basi.
Chenge: Halima nakusihi uketi.
Halima: Hoja kuhusu haki za Bunge Kanuni ya 55 kifungu cha pili.
Baada ya kauli hiyo, wabunge wa upinzani walitulizana na baadhi yao
kuwataka wenzao waketi hali iliyompa nafasi Chenge kuendelea na kikao.
“Samahani sana wabunge, tukienda hivi kwa kulazimishana yale
tunayotaka hatutaenda. Nimemwomba Zitto anayetaka kutoa taarifa kufuata
utaratibu.
"Halima unataka kuleta hoja ya haki za Bunge, unataka Bunge
tukusikilize, alichosema zitto nimesema mkalete hoja binafsi,
zitazungumzwa na Bunge hili. Mimi nataka tujielekeze kwenye shughuli
muhimu zilizo mbele yetu,” alisema Chenge.
Baada ya kauli hiyo, Halima alisikika akisema:“Hakuna shughuli
muhimu zaidi ya wananchi kutusikiliza tunazungumza nini.” Wabunge
wengine wa kambi ya upinzani walisikika wakipaza sauti kwa kusema
‘usituburuze’
Baada ya kauli hizo kuzidi, Chenge alisema: “Sitaki kufika kutumia mamlaka ya kiti”.
Kauli hiyo ilionekana kuwakera zaidi wabunge wa upinzani ambao
wengi waliwasha vipaza sauti na kuanza kusema: “Tumia mamlaka ya kiti”,
usituburuze, usitutishe, tumechoka kuburuzwa, huwezi kuzuia TBC kienyeji
hivyo.”
Naye Mbunge wa Konde, Khatib Said Haji, alisikika akisema: “Sisi
hatutongozani humu, lazima wananchi wasikie tunachozungumza ni nini.”
Baada ya kauli hiyo, Chenge alimsihi tena Halima kuketi kwa maelezo kwamba yeye ndiye aliyeanzisha hoja hiyo na watu kusimama.
Kutokana na wabunge hao kukubali kuketi, Chenge alisema hoja
iliyowasilishwa na wabunge hao ni nzuri na nyeti hivyo anasitisha vikao
vya Bunge ili Kamati ya Uongozi ikae na kulipitia kisha Bunge lingerejea
baada ya saa sita na nusu mchana.
Kauli hiyo iliwafurahisha wabunge wa upinzani ambao walianza
kuimba, Chenge, Chenge, Mtemi, Mtemi, huku wenzao wa CCM wakiwa
wamenyamaza kimya.
Saa 6:30 ilipofika, Chenge alirudi tena na kuahirisha Bunge mpaka saa 10 jioni kwa maelezo kuwa Kikao cha Uongozi kinaendelea.
Maoni ya Wabunge
Waitara alisema serikali kuchukua uamuzi huo ni kukiuka demokrasia
na kwamba juzi walipomuuliza Nape sababu za TBC kutokurusha matangazo
hayo alisema ni kwa sababu ya kuharibika kwa mitambo.
Alisema kwa namna moja CCM wanatumia njia hiyo ili kama njia ya
kuibia wapinzani majimboni kwao, na kwamba hawana mchango wowote na kazi
yao bungeni ni kulala.
Naye Devotha Minja, alisema serikali haina sababu ya msingi ya
kuizuia vyombo vya habari kwa kuwa ni haki ya wananchi kusikiliza
wawakilishi wao.
Pia, baadhi ya wabunge wa CCM, walipinga hatua hiyo ya serikali wakisema lazima kuna jambo inataka kulificha.
CCM waweka msimamo
Baada ya kuahirishwa kwa Kikao cha Bunge, wabunge wa CCM walikutana
kwenye kikao cha ndani na mmoja wa wabunge walioudhuria alisema
walimbana Nape kwa taarifa yake hiyo kwa kumweleza kuwa alikosea namna
alivyoiwasilisha.
“Tumemwambia angetakiwa aje na hoja nzito zaidi ya kwamba kama
Bunge linadaiwa na TBC tuone namna ya kulipa. Lakini tumesema matangazo
ya moja kwa moja yaendelee ingawa kwa sasa ni vigumu kwa sababu
tunadaiwa.
Kama ni kubana matumizi, wabunge wabanwe kwenye mambo ya magari na
posho zingine ili matangazo ya moja kwa moja yaendelee. Tumekubaliana
kila mtu achangie kutokana na hoja itakavyoletwa hiyo jioni,” alisema
mmoja wa wabunge wa CCM.
WADAU WA HABARI WAPINGA
Wadau mbalimbali wa habari nchini wamepinga vikali hatua ya
serikali kutangaza uamuzi wa TBC kutorusha tena vipindi vya Bunge,
katika jitihada zake za kupunguza gharama, huku wakieleza iko ajenda ya
siri nyuma ya jambo hilo linalolenga kuwanyima wananchi haki yao
kikatiba.
Wadau hao walisema hatua hiyo haina afya kwa demokrasia ya nchi na
ni kurudisha utawala wa kiimla na kijima katika nchi ambayo ilishatoka
kwenye mfumo huo.
Wakizungumza na Nipashe kwa nyakati tofauti, wameitaka serikali
kufikiria upya juu ya uamuzi huo kwa kuwa kodi za Watanzania ndizo
zinatumika na wana haki ya kujua kile wanachokizungumza wawakilishi wao
katika mhimili huo muhimu.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi
Mukajanga, alisema nchi yoyote inapimwa kwa masuala ya uwazi na
ushirikishwaji kama mambo yake yanatangazwa au ni siri, kigezo cha
uongozi, jamii na kwa kiasi gani Bunge lake linatangazwa.
Alisema kama kigezo ni kupunguza gharama hakina mashiko kwa kuwa
TBC ni mali ya umma inayolipiwa kodi na wananchi ili kuwafikishia
taarifa na vipindi mbalimbali ambavyo vyombo binafsi haviwezi kurusha.
Naye Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC),
Onesmo Olengurumwa, alisema uamuzi huo ni wa kushtusha kwa kuwa nchi
ilishafikia jitihada za kuweka uwazi ili wananchi wapate taarifa kwa
mujibu wa Katiba.
Alisema vipindi vya moja kwa moja viliwezesha wananchi kuwaona
wawakilishi wao na kwamba si vizuri kuchuja wanayoyazungumza kwa niaba
yao. Aliwaomba wabunge bila kujali itikadi zao kupinga jambo hilo kwa
kuwa linaathari kwao na wasipofanya hivyo wananchi wana haki ya kuwaona
ni wasaliti.
Mwanazuoni wa Sayansi ya Siasa na Utawala, Prof. Mwesiga Baregu,
kwa upande wake alisema uamuzi huo wa serikali ni ishara ya kurudisha
nchi katika utawala wa kiimla, kubana demokrasia iliyojengwa kwa muda
mrefu.
Alisema Watanzania wanatakiwa kuanza kudai haki, kupinga hatua hiyo
kwa kuwa ni kuminya utoaji, utafutaji na uhuru wa habari hasa kwa
kupitia sheria zilizoanza hivi karibuni kama Sheria ya Makosa ya
Mtandao.
Alisema iwapo inafikiriwa kuwa demokrasia ni ghali, Watanzania wasubiri kushuhudia ubabe katika demokrasia.
Naye Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), Deus
Kibamba, alisema hatua hiyo ni mwendelezo wa kuwanyima Watanzania
taarifa ambayo ni kinyume cha ibara ya 18 ya Katiba.
Alisema ibara hiyo inasema, kila mtu ana haki ya kupata taarifa, kuzipokea na kuzisambaza bila kujali mipaka wakati wowote.
MBOWE, MBATIA WAZUNGUMZA
Baada ya kutolewa bungeni, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni,
Freeman Mbowe, alikutana na waandishi wa habari na kusema sababu ya
gharama iliyotolewa na serikali bungeni ilibadilika wakiwa kwenye kikao
cha kamati ya uongozi na badala yake ikasema uamuzi wa kuzuia matangazo
ya vikao vya Bunge moja kwa moja umechukuliwa ili watu wafanye kazi
badala ya kuangalia Bunge.
Mkutano huo na waandishi wa habari pia uliudhuriwa na Kiongozi Mkuu
wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe na Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, James
Mbatia.
“Kwenye kamati ya uongozi nyie hamkuwapo mimi nilikuwapo na Zitto
pamoja na Mdee. Baada ya Zitto na Mdee kutoa hoja zao, mjadala ukahama
kutoka kwenye fedha na kusema uamuzi huo umechukuliwa ili Watanzania
wafanye kazi kwa sababu kwa kuangalia televisheni watu hawafanyi kazi na
kwamba watu wengi hawaangalii televisheni mchana ila wanaangalia usiku.
Tulipinga hoja hiyo kwa kusisitiza huu ni mpango wa serikali ambao
ulianza kabla ya uchaguzi, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.
Leo ni miezi mitatu tangu tumalize uchaguzi lakini hata sisi
haturuhusiwi kufanya mikutano, kitendo cha kusema TBC wao ndiyo tu
warekodi na baadaye waamue nani arushwe na nani asirushwe hewani siyo
haki,” alisema Mbowe.
Alisema wamekataa hoja hiyo, lakini cha kushangaza Mwenyekiti wa
Bunge na makatibu wao wakakimbia kiti na kuacha askari waliendeshe.
Alisema wamepata taarifa kuwa, lengo la serikali ni kuzuia mjadala
wa Zanzibar, hoja za uchaguzi mkuu na maamuzi mabovu yaliyofanywa na
serikali ya awamu ya tano yasiwafikie wananchi.
“Tulikuwa tumejiandaa kutumia hii ‘forum’ (jukwaa) kuonyesha
wananchi upande wa pili kwa kile kilichofanyiwa na serikali hii ya
Magufuli”.
Mbowe pia alisema baadhi ya wabunge wameibiwa simu zao, saa, pochi na vitu vingine vya thamani.
Kwa upande wake, Mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi), James Mbatia,
alisema anachokifanya Rais John Magufuli ni kutaka kuibana demokrasia
ili aonekane anafanya kazi, lakini hawatakubaliana na hali hiyo na
kwamba watapigania demokrasia hadi tone la mwisho ili kuona haki
inatendeka.
Imeandikwa na Fredy Azzah, Beatrice Shayo, Dodoma, Salome Kitomari na Chrstina Mwakangale, Dar
SOURCE:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment