ZANZIBAR.
MAKAMU
wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Mhe. Othman Massoud Othman amevitaka
vikundi vya mazoezi nchini kuweka kanuni na miongozo ya maadili ambayo
itasaidia kuondoa mitizamo hasi kwa jamii juu ya ushiriki wa makundi
yote katika vikundi vya mazoezi na michezo.
Ametoa
wito huo wakati akizungumza na vikundi vya mazoezi katika halfa ya
kuhamasisha ushiriki wa jinsia zote kwenye mazoezi na michezo ikiwa ni
maadhimisho ya kutimia miaka kumi ya klabu ya mazoezi Gombani kisiwani
Pemba.
Alisema,
kuwepo kwa kanuni zinazosimamia maadili katika mazoezi na michezo
kutasaidia watu wengi hasa wanawake kuona eneo hilo ni salama kwao na
kuondoa dhana potofu iliyojengeka katika jamii.
Alieleza,
"niwaombe tuweke kanuni za kusiamamia maadili zitakazo ondoa dhana
potofu kwa jamii ili tuweze kuwavutia watu wengi kushiriki mazoezi
kwasababu hili jambo ni jema zaidi."
Aidha,
makamu huyo wa kwanza wa Rais ambaye aliongoza matembezi na mazoezi ya
wanamichezo hao alifahamisha kuwa taifa linapata hasara kubwa kugharamia
matibabu ya maradhi yasiyoambukiza yanayosababishwa na mfumo wa maisha
ambapo iwapo jamii itakuwa na mwamko wa kushiriki katika mazoezi na
michezo itasaidia kupunguza gharama hizo.
"Jambo
hili ambalo mnaliendeleza kwetu sisi wengine linatupa faraja sana
kwasababu tunajua mnafanya jambo kubwa kwa jamii na nchi yetu kwani kama
kuna jambo ambalo nchi inapata hasara ni kwenye matibabu. Na matibabu
ya maradhi yasiyoambukiza kwahakika ni ya ghali sana na nyinyi nyote ni
mashahidi," alieleza, Mhe. Othman Masoud.
Katika hatua nyingine alihimiza jamii kupewa elimu ya matumizi lishe ili kujiepusha na ulaji holela unaopelekea athari kiafya.
Mhe.
Othman Masoud alisema, “twende mbali zaidi kutoa ya elimu ya lishe kwa
jamii. Kwasababu hili wengi bado huko tuna tatizo. Tumeacha sasahivi
vyakula asilia. Mwingine anaona pengine vyakula asilia sio usasa. Lazima
twende katika hatua ya kujitunza na kujipenda kwa kutambua kipi kibaya
na kipi kizuri cha kula.”
Naye
Mkuu wa wilaya ya Chake chake, Abdalla Rashid amemshukuru Mhe. Othman
kwa kuwa miongoni mwa washiriki katika bonanza hilo na kuwahimiza
wananchi kuhakikisha kwamba wanahamasishana ili wajenge utamaduni wa
kufanya mazoezi katika kujiepusha na maradhi mbalimbali yasiyoambukiza.
Akitoa
salamu za wadau, afisa programu ya michezo kwa maendeleo kutoka Chama
Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ), Khairat
Haji alieleza bado kuna changamoto kwenye jamii ya uelewa kuhusu
umuhimu wa mazoezi na kupelekea vikwazo kwa makundi yote hasa wanawake
kushiriki kikamilifu katika mazoezi na michezo.
Aidha
aliongeza, ukosefu wa miundombinu na vifaa wezeshi vya mazoezi ni
kikwazo katika ufikiaji wa usawa wa kijinsia kkwenye michezo na kuomba
serikali na wadau kusaidia kuboresha miundombinu hiyo ili kuwezesha kila
mmoja kushiriki bila kikwazo.
"Kuna
changamoto kadhaa ambazo tumeziona ikiwemo ukosefu wa vifaa na
miundombinu wezeshi kwaajili ya makundi yote kushiriki katika michezo
mbalimbali," alifahamisha afisa huyo.
Kwa
upande wake mwenyekiti wa klabu ya mazoezi Gombani, Hamad Malengo
aliomba wadau kuungana pamoja kushiriki katika michezo na mazoezi ili
kuondoa dhana hiyo potofu iliyojengeka katika jamii kuwa kushiriki
michezo ni kujifunza uhuni.
Alisema,
"elimu kwa jamii inahitajika zaidi ili kutoa mwamko wa watu kushiriki
kwenye mazoezi na kuachana na dhana kwamba michezo ni uhuni. Ni lazima
tusimame pamoja ili kila mmoja wetu aweze kushiriki mazoezi kwaajili ya
afya yake.”
Hafla
hiyo ya kuhamasisha ushiriki wa jinsia zote kwenye mazoezi na michezo
ikiwa ni maadhimisho ya kutimia miaka kumi ya klabu ya mazoezi Gombani
kisiwani Pemba iliyoandaliwa kwa kushirikiana na TAMWA-ZNZ na Shirika ka
Bima la Zanzibar imevishirikisha vilabu zaidi ya vitano vya mazoezi
kutoka Unguja, Tanga na wenyeji Pemba.