Home » » Chonde chonde wanasiasa, mti na macho!

Chonde chonde wanasiasa, mti na macho!

Zanzibar. Mojawapo kati ya sababu za kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) Zanzibar ni kumaliza siasa za uhasama, chuki na kukaribisha siasa za maridhiano, ushindani wa sera na zenye kutoa majibu ya matatizo ya wananchi.
Kutokana na hali hiyo, vyama vilitarajiwa vishindane kwenye ulingo sawa wa kisiasa kwa sera nzuri ambazo watu wataziamini na kuziunga mkono.
Hata hivyo, Zanzibar inakwenda hatua kumi mbele, inarudi hatua tisa nyuma. hali ya kisiasa hivi sasa inasikitisha na kukatisha tamaa na iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa, inaweza kuturejesha tena kwenye siasa za chuki na uhasama.
Wanasiasa wanafanya mikutano, wanahuburi chuki, uhasama, kashfa na ubaguzi, jambo ambalo halioneshi kama kweli kuna nia safi baada ya maridhiano.
Ninachokiona ni kwamba vyama vya siasa na wanasiasa kwa ujumla wao, hawana jipya la kuwaambia wananchi wa Zanzibar.
Malumbano yanayoendelea ya vyama vikuu kwenye SUK yanatia kichefuchefu. Zanzibar ina matatizo ya kiuchumi, hali za maisha ni ngumu, lakini hakuna anayezungumzia masuala hayo zaidi ya matusi na kashfa.
Wananchi hawana shida ya matusi wala kashfa maana kama kutukana, kukashfu watu kila mmoja ni mjuzi wa hilo. Watu wanalotaka ni kuona hali zao za maisha zinakuwa bora zaidi. Wanahitaji siasa safi na uongozi bora.
Mwishoni mwa Oktoba kuliandaliwa mikutano kadhaa ya CCM na CUF katika maeneo tofauti ya Unguja na Pemba. Kwenye mikutano hiyo walihutubia viongozi wenye dhamana kwenye vyama vyao na katika Serikali.
Ingawa kauli za viongozi hao zinaonekana kuwa zimejikita kwenye vijembe na vitisho kwa watu wanaotoa maoni yanayowachukiza wao; wale waliozitamka si watu wapuuzi wala wajinga wasioelewa uzito na umuhimu wa kuyaenzi maridhiano ya SUK.
Vita hii ya maneno ni uthibitisho wa baadhi ya viongozi kukosa uvumilivu. Ni dhambi kuruhusu hali hii itawale fikra zetu. Tutambue kuwa Zanzibar ina matatizo ya kijamii ambayo hayawezi kutatuliwa kwa ubabe, vitisho wala kuwakashfu watu, bali kwa kuyaenzi na kuyalinda maridhiano ya kisiasa kwa nia njema.
Ni wajibu wa viongozi kukubali dhamana zao na wajibu wao mbele ya jamii, pia ni muhimu kwa wanasiasa ndani ya SUK kuaminiana tofauti na hali ilivyo sasa.
Viongozi katika SUK walio kwenye vyama vya siasa ni muhimu kutanguliza busara na hekima kuliko jazba na nongwa. Hivyo basi, CCM na CUF, kama kweli wana dhamira ya dhati kuiepusha nchi yetu na balaa la kurejea kwenye vurugu na siasa za chuki, hawana budi wakubaliane kiungwana kuheshimu na kutekeleza maridhiano ya kisiasa.

chanzo;mwananchi.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa