BAADHI ya viongozi wa CCM wa Zanzibar, vijana na wazee,
wananichekesha sana kiasi kwamba nawaona kama watu waliochanganyikiwa
ama kutojua hali ilivyo katika dunia ya leo ya utawala wa kidemokrasia.
Kila nikijaribu kutafakari wanayonena, wanayotenda, kauli na vitendo
vyao havina lengo jingine lolote lile isipokuwa kutaka wazushe vurugu
Visiwani na watu wasielewane.
Wanachokitaka ni kile kinachoitwa patashika nguo chanika, yaani kila
penye kheri pawepo shari na kila penye amani pawe na mtihani.
Kwa viongozi wengi wa CCM, hasa wale waliochupia siasa hivi karibui,
kaulimbiu ya “Mapinduzi Daima” haimaanishi kutafuta maendeleo, bali ni
kuwepo vurugu.
Watu hawa wanafanya kila juhudi za siri na za dhahiri za kuzusha
mambo ambayo kama hapatumiki hekima na busara, yanaweza kuzusha tena
siasa za chuki na uhasama.
Baada ya kuwasikia baadhi ya hao wanaojiita wastaafu katika Serikali
ya Zanzibar na vikosi vya usalama kutaka Unguja na Pemba zitengane na
wasiwajibishwe kwa uchochezi wao, sasa tunasikia mengine yasiyokuwa na
lengo jingine isipokuwa kupalilia siasa za chuki na uhasama.
Miongoni mwa vichekesho vya vongozi hawa vya hivi karibuni ni kile
alichokitoa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Unguja, Haji Ameir Haji.
Kiongozi huyu, bila ya kutafuna maneno wala kuzungumza kwa mafumbo,
amewataka wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kupitia tiketi ya CCM waache
mara moja kuikosoa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika vikao vya
Baraza.
Kwake yeye kufanya hivyo ni dhambi kubwa na haisameheki ndani ya CCM.
Badala yake anawataka wawakilishi hao siku zote wafanye kila juhudi za
kuisifu serikali kwa kutekeleza sera za CCM na ilani ya uchaguzi ya
chama hicho.
Hata pakitokea ufisadi, rushwa na ubadhirifu wa mali za serikali,
basi wawakilishi wa CCM waisifu serikali, kama matendo hayo ya kihalifu
ndiyo sera ya chama hicho.
Kiongozi huyu, bila ya kuona vibaya wala haya, amewataka wawakilishi
hao kutofanya urafiki na wala wasishirikiane na wawakilishi wa vyama
vingine.
Hapa tujiulize nini lengo la kiongozi huyu katika wakati huu ambao
Zanzibar ambayo ilitikisika vibaya kisiasa na watu kutoelewana na hata
kuuana ikiwa shuwari na kuanza kujipatia maendeleo.
Kwa kutolewa kauli kama hii, ungelitarajia viongozi wa CCM kumkosoa na hata kumuonya asirudie matamshi kama hayo.
Lakini viongozi wa chama hiki wamekaa kimya, na kitendo hiki ni
kielelezo cha utamaduni uliopo ndani ya CCM cha kulindana hata kwa
maovu. Hii ni hatari kwa CCM na Zanzibar.
Kukaa kwao kimya kumenipa tafsiri nyingi; mojawapo ni kwamba CCM
inazungumzia tu amani na utulivu, lakini vitendo vyake havielekei huko.
Hapa tunapaswa kujiuliza hawa wahafidhina wa CCM wanataka kuipeleka wapi Zanzibar?
Wapo waliotaka Unguja na Pemba zitengane na wakubwa wao kuwavumilia
na sasa tunaambiwa wawakilishi wa CCM wasishirikiane kwa njia moja au
nyingine na wenzao wa chama cha CUF.
Watu hawa bila ya kuona vibaya wala haya ati wanasema tokea enzi za
kale watu wa visiwa hivi sio wamoja. Huu ni unafiki mkubwa.
Wanachojali wao na kuthamini ni karafuu za Wapemba na sio watu wa
kisiwa hicho wanaozilima na kuzichuma. Huu ni ubaguzi wa hali ya juu na
uchochezi mkubwa wa kisiasa, ambao haufai hata kidogo kulelewa wala
kuvumiliwa.
Si ajabu kesho akatokea mtu mwingine katika kundi la wahafidhina
akitaka Baraza la Mawaziri la Zanzibar ligawike sehemu mbili, moja ya
CCM na nyingine ya CUF.
Baada ya hapo tena akaambiwa Rais Ali Mohamed Shein asishirikiane na
wala asishauriane na Makamu wa Pili wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad
katika kuiongoza Zanzibar.
Ninaamini kwa dhati kama kauli mbaya kama hii ingelitoka kwa kiongozi
wa chama cha upinzani na hasa CUF, basi Zanzibar igekuwa haikaliki.
Tungelisikia watu wengi wanafunguliwa mashitaka ya uchochezi na
kuhatarisha amani na utulivu. Lakini kwa vile aliyetoa kauli mbaya kama
hii ni kiongozi wa CCM, basi hulindwa kwa nguvu zote kwa vile ni
“mwenzetu” na “tumetoka naye mbali”.
Lakini sishangazwi hata kidogo kusikia kauli za hatari kama hizi
kutoka kwa baadhi ya viongozi wa CCM kwa sababu bado wahafidhina
wanaumia ndani kwa ndani kuona Zanzibar imetulia kisiasa na hawafurahii
kuwepo Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Watu hawa, kwa mujibu wa hali ilivyo, wapo huru kutukana watu matusi
ya nguoni hadharani na kuandika matangazo machafu kwenye mbao za
maskani zao.
Yote haya yanaonekana hayavunji sheria za nchi kwa vile wanaofanya ni
viongozi wa CCM. Kwa maana nyingine ni kusema viongozi wa CCM Zanzibar
wapo huru kuvunja sheria na kutoa kauli za matusi na uchochezi.
Sio siri kuwa wengi wa hawa wahafidhina wanadaiwa kuwa ni watu
waliozoea kutuma vijana kupiga watu ovyo mitaani na majumbani na
kusababisha yatima, vizuka na vilema kwa sababu ya siasa.
Kwa kweli kuwavumilia watu wenye kauli za aina hii, zinazochochea
uhasama ni hatari na wanaweza kuwa ndio chanzo cha kuzusha wimbi
jingine la vurugu za kisiasa Zanzibar.
Wakati umefika kwa viongozi wa juu wa CCM kutafakari kauli na vitendo
vya hawa wahafidhina ambao ninaweza kusema kwa kinywa kipana kuwa
hawaitakii mema Zanzibar. Kazi yao kubwa ni fitna tu.
Kuwanyamazia na kutowawajibisha kisheria wale wote wanaotoa kauli za
uchochezi au kuhatarisha amani ni jambo la hatari sana. Lazima
wawajibishwe kisheria.
Hawa watu hawaitakii mema Zanzibar na watu wake, na kwamba kila mtu
muovu ni hatari. Tukumbuke wahenga walivyotuasa kwa kutuambia “majuto
mjukuu.”
Jamani wahafidhina ni watu hatari, lakini wahafidhina pia wajue
kwamba Wazanzibari wapo macho na hawapo tayari kurejea kwenye siasa za
kutukanana, kupigana na kuuana.
Historia katika nchi mbalimbali imeonyesha watu wa aina hii huweza
kudanganya watu kwa muda tu na sio siku zote. Mwizi siku zake ni 40,
lakini za wachochezi huzidi kidogo tu na haziwi maisha.
Kwa maovu wanayoyatenda na ndoto zao mbaya wanazoitakia Zanzibar,
waelewe kuwa wahenga hao hao walitahadharisha watu wabaya kwa
kuwaambia; “kila mchimba kisima huingia mwenyewe.”
chanzo;tanzania daima
0 comments:
Post a Comment