Home » » SMZ yavionya vyombo vya habari

SMZ yavionya vyombo vya habari

 
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), imeonya vyombo vya habari kwamba haitosita kuvichukulia hatua za kisheria ikiwemo kuvifungia vyombo vitakavyotumia vibaya uhuru wa vyombo vya habari kwa kuchapisha na kutoa habari zenye lengo la kuvuruga amani.
Kauli hiyo imetolewa jana na Waziri wa Habari Utangazaji Utalii na Michezo, Said Ali Mbarouk, wakati alipokutana na viongozi na wahariri wa redio binafsi ya Zenj FM pamoja na Coconut.
Redio hizo hivi karibuni zilirusha moja kwa moja kongamano la wastaafu wa vikosi vya ulinzi na usalama, ambapo azimio lao kuu lilikuwa utengano kwa watu wa Pemba na Unguja. Akifafanua zaidi, Mbarouk alisema SMZ yenye sura ya Umoja wa Kitaifa kwa sasa imetulia na malumbano ya kisiasa yaliyokuwepo zamani yamemalizika na wananchi wanaishi vizuri kwa pamoja.
Alisema chokochoko za aina hiyo pamoja na kauli hizo, kamwe hazitaachiwa zichukuwe nafasi tena ya kuleta mgawanyiko wa wananchi ambao kwa sasa wamemaliza tofauti zao tangu kuwepo kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
'Sisi tukiwa wasimamizi wa sera za Serikali hatutasita kuvichukuliya hatua kali za kisheria vyombo vya habari vyenye lengo la kuwagawa wananchi kwa kutumia kisingizio cha uhuru wa vyombo vya habari......uhuru wa vyombo vya habari upo lakini una mipaka yake'alisema.
Aliwataka viongozi na wahariri kuwa makini sana kuhakikisha waandishi waliopo chini ya dhamana zao wanafuata maadili ya fani na taaluma ya uandishi wa habari na kamwe kutoruhusu vyombo hivyo kutumika kinyume na maadili kwa maslahi ya watu wachache.
Karipio la Waziri Mbarouk limekuja ambapo hivi karibuni redio hizo zilirusha moja kwa moja hewani makongamano yaliyotayarishwa na umoja wa askari wastaafu yakiwa na matamshi mazito ya kuwataka wananchi wa visiwa viwili hivi kutengana.
Katika mikutano miwili iliyofanyika katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi hapo Kikwajuni na huko Makunduchi, wastaafu hao walionesha kutofurahishwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliopo sasa inavyoendeshwa chini ya Rais Dk Ali Mohamed Shein kusema imeshindwa kuimarisha amani na utulivu kufuatia kujitokeza kwa matukio mbali mbali ya watu kumwagiwa tindikali.
Aidha Mbarouk ameitaka Tume ya Utangazaji kufuatilia vyombo vya habari na kuona kwamba wanatekeleza na kufuata masharti waliyopewa ya leseni za kurusha matangazo kwa wananchi.
Ofisa Mwandamizi wa Redio ya Zenj FM Suleiman Juma Kimea alikiri kutokea kwa kasoro mbalimbali katika baadhi ya vipindi vilivyorushwa hewani moja kwa moja katika makongamano hayo na kusema kwamba hayatorudiwa tena.
“Tunakiri kujitokeza kwa kasoro mbali mbali katika matangazo yaliyorushwa hewani moja kwa moja na kituo chetu na tunaahidi kwamba hayatojitokeza tena,' alisema.
Chanzo:Habari Leo

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa