Home » » Ahimiza wananchi kujiunga na Saccos

Ahimiza wananchi kujiunga na Saccos

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi, Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd amewasihi maofisa maendeleo ya jamii kuhamasisha wananchi kujiunga kwenye Vyama vya Kuweka na Kukopa (Saccos) wajipatie kipato.
Alisema hayo juzi jijini hapa wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 50 tangu kilipoanzishwa Chuo cha Maendeleo ya Jamii (CDTI) Tengeru, sanjari na mahafali ya tatu ya chuo hicho yaliyotoa wahitimu zaidi ya 109 ambao walitunukiwa shahada zao na makamu huyo.
Alisema endapo wananchi hawatapewa elimu ya kujiunga na vyama vya kuweka na kukopa, maendeleo hayataweza kupatikana.
Alisema utoaji wa mbinu za kujikwamua maisha ni muhimu ukatolewa na maofisa hao ili wananchi waweze kunufaika na mikopo ya chini na ya kati, inayotolewa katika halmashauri mbalimbali kwa ajili ya kuinua kipato vyao ndani ya familia.
Alisema ni fedheha kwa baadhi ya maofisa maendeleo ya jamii kuacha wananchi wakitaabika wakati wao wanao ujuzi wa kuwezesha kupata mafanikio.
“Naomba sana maisha ya wananchi yaboreshwe badala ya kuachwa kama hawana watu wa kuwaongoza, hamasisheni wananchi wajiunge na vicoba kwa maendeleo yao kwani maofisa maendeleo ya jamii wanapaswa kuwa mfano katika kutetea na kuleta maendeleo,” alisema.
Wahitimu 109 walitunukiwa shahada ya kwanza ya Maendeleo ya Jamii, Usimamizi wa Programu za Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Maendeleo pamoja na Stashahada ya Uzamili ya Maendeleo ya Jamii.
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba aliwasihi maofisa maendeleo ya jamii nchini kuhakikisha wanaandaa programu zenye kuwaletea maendeleo jamii ikiwemo kuwainua zaidi vijana na wanawake katika kukuza uchumi.
Chanzo;Habari Leo

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa