Home » » CCM yaibuka kidedea Kiembesamaki

CCM yaibuka kidedea Kiembesamaki

Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), imemtangaza Mahmoud Thabit Kombo (CCM), kuwa mshindi wa uwakilishi katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kiembesamaki uliofanyika jana mjini Zanzibar.

Katika uchaguzi huo, wapiga kura 2,458 ndiyo waliojitokeza kati ya wapigakura 5,122 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga kura katika jimbo hilo.
Akitangaza matokeo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Kiembesamaki, Suluhu Ali Rashid alisema mgombea wa CCM amepata kura 1,856 sawa na asilimia 76.5 wakati mgombea wa CUF, Abdulmalik Haji Jecha alipata kura 445 sawa na asilimia 18.3. Mgombea wa ADC Amani Ismali Rashid alipata kura 84 sawa na asilimia 3.5.
Wagombea wengine na kura zao katika mabano ni Hashim Juma Issa Chadema (34 sawa na asilimia 1.4), Ali Mohamed Ali wa Tadea (kura 6  sawa na asilimia 0.2) Ramadhan Simai Mwita akiambulia kura 1 sawa naasilimia 0.0 kutoka Chama cha Sau.
Suluhu alisema wagombea wa vyama vitano wamesaini kuyakubali matokeo hayo isipokuwa mgombea wa CUF, Abdulmalik ambaye aliondoka mapema baada ya matokeo hayo kutangazwa.
“Uchaguzi haukuwa huru na wa  haki, kulikuwa na wizi wa kura, wapo watu walikuwa wakipakiwa kwenye magari na kuletwa vituoni,” alisema Abdulmalik.
Hata hivyo, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Hamad Mussa Yussuf alisema uchaguzi ulikuwa huru na wa haki na hakuna ukiukwaji wowote wa sheria uliofanyika na kusema ulikuwa ni uchaguzi mdogo wa mfano kuwahi kufanyika visiwani humu.
Hamad alisema taratibu za uchaguzi ziliheshimiwa na kufuatwa ikiwa ni pamoja na vifaa kuletwa mapema vituoni huku Daftari la Wapiga kura likiwa na picha za rangi.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Tadea, Ali Juma Khatib alisema uchaguzi huo ni wa mfano huku akiipongeza ZEC kwa kazi nzuri ya katika hatua za upigaji wa kura, kuhesabu na majumuisho.
Khatib alisema kimsingi taratibu zote zilifuatwa katika vituo ikiwa ni pamoja na uchaguzi huo kuwa na uwazi wa kutosha na  matokeo kutangazwa kwa muda mwafaka kwa kutumia teknolojia ya kisasa.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Zanzibar, Walide Bakari Jabu alisema matokeo hayo ni fundisho kwa wapinzani na kusema hizo ni salamu maalumu katika kuelekea mwaka 2015.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya matokeo kutangazwa mshindi mteule wa CCM, Mahmoud Thabit Kombo alisema atafanya kazi kwa kushirikiana na makundi yote bila ya kujali itikadi za kisiasa.
“Wakati wa kampeni umemalizika, sasa ni jukumu letu sote kutekeleza ilani ya uchaguzi ya CCM na kutimiza ahadi nilizozitoa kwani haziwezi kufikiwa bila ya ushirikiano na kufanya kazi pamoja,” alisema Mahmoud.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa