Home » » Wazanzibari wataka uwiano Bunge la Katiba

Wazanzibari wataka uwiano Bunge la Katiba

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 Suala la uwiano wa wajumbe katika Bunge Maalumu la Katiba, kati ya Tanzania Bara na Zanzibar, juzi jioni lilizua malumbano yaliyotokana na mjumbe, Said Ally Mborouk, kueleza kuwa Zanzibar kwa muda mrefu imekuwa ikionewa na kudhulumiwa.
Hali hiyo ilijitokeza wakati wajumbe hao walipokuwa wakichangia michango yao katika Rasimu ya Kanuni ya Uendeshaji wa Bunge hilo mjini Dodoma.
Mbarouk alisema Zanzibar ni moja ya nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwamba kuna haja ya kuitendea haki kwa kuhakikisha kuwa inakuwa na idadi sawa ya wajumbe wakati Bunge litakapoanza vikao.
“Sisi Wazanzibari kwa muda mrefu tumekuwa tukilalamika kuwa Watanganyika wamekuwa wanatuonea, wanatudhulumu katika Muungano huu. Mara nyingine mjadala wa malalamiko haya hufanyika katika Baraza la Wawakilishi ambalo wewe mheshimiwa Mwenyekiti (Pandu Ameir Kificho) ni Spika,” alisema na kuongeza;
“Sasa wenzangu wa Zanzibar tumepata nafasi kwa kushirikiana na wenzetu wa Tanganyika ama kuimarisha au kuusambaratisha Muungano wetu.”
Alisema utungaji wa kanuni hizo unaweza kuzaa katiba itakayosaidia kuondoa uonevu, dhuluma na kero za Muungano zilizodumu kwa miaka 50 iliyopita.
Pia alisema kanuni hizo zinaweza kuzaa Katiba itakayoendeleza kero ama kusambaratisha kabisa Muungano kama ambavyo imetokea kwenye nchi nyingine duniani zilizokuwa zimeungana.
Alisema Bunge hilo lina nafasi kubwa ya kuondoa kero za Muungano na kwamba ni lazima suala hilo lianzie katika utungaji wa kanuni.
Kauli hiyo ilimfanya Job Ndugai ambaye pia ni Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kusimama na kujibu.
Katika majibu yake, Ndugai alisema kuna muhimu wa wajumbe kuwa na umakini katika lugha wanazozitumia katika vikao vikubwa kama hicho.
“Lugha ni muhimu sana. Utu wa mtu uko katika lugha... kitu muhimu ni kujenga hoja ili wenzako wakuunge mkono,” alisema na kuongeza: “Lakini anaposimama mtu akasema kwa miaka 50 ya Muungano huu kumekuwa na dhuluma na uonevu na mambo kama hayo ehh, haya bwana.”
Alisema Bunge hilo ndio mahali ambapo watu wanaweza kutoa madukuduku yao lakini kwa kutumia lugha za kistaarabu.
Chanzo;Mwananchi 

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa