Home » » UKWELI UTAKUWEKA HURU: Kweli Kinana shujaa, jasiri anayetoboa siri ya CCM

UKWELI UTAKUWEKA HURU: Kweli Kinana shujaa, jasiri anayetoboa siri ya CCM

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Ifikapo mwaka 2015 hamasa za kisiasa kwa upande wa Zanzibar zitakuwa katika kiwango cha juu huku ikitegemewa kutokea kwa mabadiliko ya uamuzi miongoni mwa wapigakura, hususan vijana ambao wengi wao wamezaliwa baada ya Mapinduzi ya mwaka 1964.
 Mabadiliko yatajitokeza kuanzia wakati wa kutafuta wagombea kupitia vyama vya siasa na katika hatua hii, makundi ya vijana yatajiunga pamoja kuona wanafanikiwa kupenyeza watu wao, lakini pia yale mambo ambayo wanadhani yatawafikisha katika maisha bora zaidi watayapa nguvu huku wakiwapuuza wanasiasa ucharwana wababaishaji wengine.
 Vijana wengi wanaonekana kuanza kuzitupia kisogo siasa zisizowahakikishia maisha bora, Si vyama vya upinzani au vyama tawala; vyote vitakuwa katika wakati mgumu kipindi hicho.
Lakini ugumu zaidi utajitokeza ikiwa atajitokeza mwanasiasa mwenye kubeba matumaini ya vijana baada ya uchaguzi.
 Zile porojo za mifereji kutoa maziwa na asali naona hazitasikilizwa tena na kundi la vijana ambao wengi wao wamekata tamaa, hasa wakitazama siku zinakwenda huku ahadi za wanasiasa ni zile zile hakuna jipya, hazibadiliki wakati mambo yamebadilika.
 Jambo moja ambalo kwa upande wa Zanzibar vyama vya siasa vinapaswa kushukuru Mungu ni kitendo cha Katiba kukubali kuwepo kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) ambayo inavihakikishia vyama vyote vitakavyoungwa mkono na wapigakura kwa asilimia kubwa kuwemo ndani ya serikali.
 Kwa hali ya mambo inavyokwenda, mabadiliko ya wapigakura, mabadiliko ya kiuchumi duniani, ukosefu wa ajira na kuongezeka kwa tofauti kubwa kati ya walionacho na wasionacho, hakuna chama cha siasa kitakachoweza kutamba kuwa kina uhakika na ushindi.
 Wale wanaomkejeli rais wa awamu ya sita, Zanzibar, Amani Abeid Karume kwa kitendo chake cha kukubali mabadiliko katika mfumo wa siasa wakati wa uongozi wake, wataweza kujutia vitendo vyao pale matokeo ya uchaguzi yatakapotangazwa huku vyama karibu vyote vilivyoshiriki uchaguzi vikikaribiana sana.
 Ingawa hilo siyo jambo geni katika historia ya siasa za Zanzibar, lakini katika hali ambayo haitotarajiwa, karata ya mwisho ya kuamua mshindi katika uchaguzi mkuu ujao, itachezwa na wapigakura vijana ambao watatazama zaidi namna wanavyoweza kuvuka katika dimbwi la umaskini.
  Wakati wa viongozi wenye sifa za shaka shaka umeshapita, wenye visasi na kukurupuka katika utendaji kwa maslahi binafsi umeshapita ni zama za siasa za maridhiano huku siasa ikitumikia uchumi na kuonekana kwa vitendo kubadilika kwa maisha ya watu na sio ukuaji wa uchumi kwa takwimu za vitabuni.
 Jambo hili siyo la kufikirika, ni suala lililo wazi kabisa kwamba vijana watatumika kama nguvu kubwa ya mageuzi ya kisiasa, kijamii na kiuchumi na hali hii sio kwa Zanzibar tu, bali litazikumba nchi karibu zote Afrika.
 Wazanzibari walio chini ya miaka 30 wanawakilisha zaidi ya asilimia 78 ya idadi ya watu, hivyo vijana wengi  wanaonekana kama vile kukatishwa tamaa na vikwazo vya kielimu, ajira na masuala mengine katika jamii ndani ya ulingo wa kisiasa na nje pia.
Taarifa ya Sensa ya Watu na  Makazi ya mwaka 2012 inaonyesha kwamba asilimia 78 ya Watanzania wapo chini ya umri wa miaka 35 na nusu yao  wapo chini ya umri wa miaka 17.
Hawa ni vijana ambao wanataka kuona matumaini yao yakitimia katika maisha.
 Lazima tukubali kwamba matumaini ya vijana yanajengwa kwa uhalisia wa mambo na kwamba masuala ya kuboresha  huduma za kijamii za elimu, makazi bora, afya, maji safi na salama, demokrasia na utawala bora ni mambo ambayo vijana wanayatizama kwa jicho pana.
Katika kufikia kutimiza  haja za vijana tunahitaji kufikiria zaidi mfumo bora na imara wa mundo Muungano wetu ambao utawahakikishia fursa za ajira na kupunguza umaskini kwa kiwango kikubwa.
 Jamii ya vijana  katika nchi inatazamwa kwa umakini zaidi hasa  kwa sababu ya nguvu za ushawishi kisiasa, kiuchumi na hata kijamii.
Katika uchaguzi mkuu hapo mwakani, vijana wa Zanzibar wanasema watakachohitaji ni hatma yao watawezaje kumudu hali za maisha katika changamoto ya ukosefu wa ajira na udhaifu wa maamuzi ya watekelezaji sera?
 Wakati hayo yakiendelea kwa wapigakura vijana, kwa wanasiasa nako hali itakuwa ngumu zaidi kwao maana kwa kipindi kirefu sasa wametoa msukumo kidogo kwa kipaumbele cha kuondoa umaskini, maisha bora,lakini pia hakuonekani kama kuna dhamira ya dhati ya kukwamuka, hivyo wapigakura vijana wasiokuwa na ajira, makazi bora wanaweza kuvutiwa na mwanasiasa atakayewapa matumaini yanayoingia akilini mwao.
 Uchaguzi wa mwakani utakuwa ni wa tano tangu kurejeshwa tena kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.
Bila shaka kutakuwa na mabadiliko ya kila aina, kuanzia wagombea, kampeni na hata aina ya hotuba za mikutano ya kampeni inategemewa kuywa tofauti sana na chaguzi zilizopita.
 Wapigakura waliozaliwa mwaka 1992 ambao mwakani watakuwa ni sehemu ya wapigakura katika uchaguzi mkuu, watakuwa wameshapata picha ya wanasiasa tulionao.
 Siyo wadogo tena wa kuweza kuwabaini wanasiasa wababaishaji, wazugaji na wasaka tonge kwani vijana wamejifunza mengi, wameyaona mengi, wamewajuwa wanafiki na watu wakweli, wamewaona wababaishaji na watu makini.
Hawatafanya uzembe tena, watakuwa makini kupembuwa mchele upi na pumba zipi, nani msakatonge na nani anawafaa kwa kubadilisha maisha yao, nani atawapa shibe ya siku moja katika maisha ya miaka mitano ijayo na nani atawapa neema ya maisha yaliotononeka angalau kuvuka mstari mwekundu wa umaskini.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa