Home » » MOSOTI, BUTOYI WAMTESA PHIRI

MOSOTI, BUTOYI WAMTESA PHIRI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Kocha wa Simba, Patrick Phiri amepatwa na kigugumizi cha uamuzi wa nani abaki kati ya Mkenya Donald Mosoti na Mrundi Butoyi Hussein kujaza nafasi ya beki wa kati.
Hadi jana, Phiri alikuwa akikuna kichwa kuhusu nani asajiliwe msimu ujao baina ya wachezaji hao.
Akizungumza na gazeti hili jana,  Phiri alisema wachezaji wote ni wazuri, lakini anahitaji muda zaidi wa kufanya uamuzi wa busara.
“Natakiwa kuwa makini katika uamuzi wangu kuhusu nani nimchukue kati ya Mosoti na Butoyi.
“Nimewaona katika mazoezi, Mosoti ni beki mzuri hata huyu mpya (Butoyi), pia ni mzuri, ila nitaendelea kumwangalia zaidi,” alisema.
Wiki hii, uongozi wa klabu ya Simba ulimleta nchini kwa majaribio beki huyo mpya kutoka Telecom ya Djibouti ambaye kwa Kirundi jina lake lina maana ya Dotto. Butoyi alianza mazoezi na Simba juzi  huku Zacharia Hanspoppe akiwa na matumaini kuwa ndiye atakayechukua nafasi ya Mosoti.
Mosoti alisema hata ikitokea akaondoka Simba kabla ya Desemba kama walivyokubaliana haitakuwa tatizo kwani ni mpango ambao upo, ingawa alipendelea kuachana na timu hiyo wakati wa dirisha dogo la usajili.
Awali, Mosoti aliomba kuvunja mkataba na Simba ili ajiunge na klabu moja ya nchini Qatar ambayo alikwenda kufanya majaribio na kufuzu. Hata hivyo ilishindikana kutokana na kuwa na mkataba mrefu.
“Nilizungumza na  waajiri wangu  (Simba) kuhusu hilo, walinikubalia kuwa nikitaka kuondoka nitaruhusiwa.
Baada ya mazungumzo niliona ni vyema niondoke Desemba, ila kulikuwepo na makubaliano kwamba ikitokea hata kabla ya wakati huo niruhusiwe, hivyo hakuna tatizo kwa hilo,” alisema.
Katika hatua nyingine, Phiri amesema anaanza kukipima kikosi chake kwa kucheza mechi na timu ndogo kabla ya kuangalia michezo ya kimataifa.
Simba ipo visiwani hapa inafanya mazoezi yake kwenye uwanja wa Chuoni na  keshokutwa usiku itacheza mechi yake ya  kwanza ya kirafiki na timu ya daraja la pili ya Kilimani City. Mechi hiyo itafanyika  kwenye Uwanja wa Amaan
Mbali na mchezo huo wa kwanza kwa kocha huyo Mzambia, Simba pia itacheza na Miembeni inayoshiriki Ligi Kuu ya hapa wiki ijayo, Tanzania  Prisons na Mtibwa Sugar ambazo zinashiriki Ligi Kuu Bara.
Phiri alisema kuwa wachezaji wake wanatia moyo kwani wameonyesha mabadiliko makubwa na hakusita kumsifu beki wa kulia wa timu hiyo, Nassoro Masoud ‘Chollo’ akisema kuwa kiwango chake kimepanda.
Msimu uliopita Chollo alitumia muda mwingi nje ya uwanja kutokana na kuwa majeruhi na hivyo kutoa nafasi kwa beki chipukizi, William Lucian ‘Gallas’ kucheza nafasi yake.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa