Home » » ˜TOENI USHAHIDI WA WABAKAJI MAHAKAMANI

˜TOENI USHAHIDI WA WABAKAJI MAHAKAMANI

MRATIBU wa mtandao wa kupambana na vitendo vya udhalilishaji kijinsia Jeshi la Polisi Makao Makuu, Hasina Ramadhan Toufik ameitaka jamii kutoa ushahidi mahakamani kwa watu wanaotuhumiwa kubaka ili kukomesha matukio hayo.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia katika Hospitali ya Wagonjwa wa Akili Kidongo Chekundu mjini hapa, Toufiki alisema wagonjwa wa akili wamekuwa walengwa wa matukio ya ubakaji.
Alisema ubakaji kwa watu wenye matatizo ya akili, haukubaliki na kuitaka jamii kuwa tayari kuwafichua watu wa aina hiyo kwa kutoa ushahidi mahakamani.
“Walemavu wenye matatizo ya akili, wanakabiliwa na tishio la ubakaji huku wakiwa walengwa wakubwa kwa sababu ushahidi wao haukubaliki mahakamani,” alisema.
Aidha, alisema moja ya kikwazo kikubwa ambacho kinahitaji kufanyiwa marekebisho ni Sheria ya Ushahidi ya mwaka 1917, ambayo haitambui ushahidi wa mtu mwenye matatizo ya akili mahakamani.
Alisema wabakaji wengi wanatumia mwanya huo wa kufanya vitendo vya uhalifu, wakijua wazi kwamba hakuna ushahidi utakaokubalika mahakamani kwa mtu aliyebakwa ambaye ni mgonjwa wa akili.
“Sheria hii inakabiliwa na mapungufu mengi ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi ili kuona kwamba watuhumiwa wa makosa ya ubakaji, wanachukuliwa hatua za kisheria na kukomesha vitendo hivyo moja kwa moja,” alisema.
Mkuu wa Hospitali ya Wagonjwa wa Akili Kidongo Chekundu mjini hapa, Vuai Kombo Haji alilipongeza Jeshi la Polisi Kitengo cha Dawati la Jinsia kwa kujitolea na kufanya usafi katika hospitali hiyo.
Alikiri kuwa wagonjwa wa akili katika hospitali ya Kidongo Chekundu, wanakabiliwa na tishio kubwa la vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia ikiwemo kubakwa.
Mtandao wa Polisi wa kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa kijiinsia ukiwajumuisha zaidi ya polisi 30, walikuwa katika zoezi la kufanya usafi katika eneo la hospitali ya wagonjwa wa akili Kidongo Chekundu.
Chanzo:Habari Leo
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa