Home » » JAJI MKUU AVIPA VYUO CHANGAMOTO

JAJI MKUU AVIPA VYUO CHANGAMOTO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

JAJI Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, amesema uwapo wa vyuo vya elimu ya juu kutasaidia kupatikana kwa wataalamu wa fani mbalimbali ambao watasaidia katika kuleta maendeleo ya nchi.
Akizungumza na wahitimu wa Kituo cha Mafunzo ya Sheria na Utafiti Zanzibar wakati wa mahafali ya kwanza ya kituo hicho, alisema Zanzibar ina uhaba wa wataalamu, hivyo vyuo vya elimu ya juu vina nafasi nzuri ya kupunguza changamoto hiyo. 

Alisema kila wataalamu wanavyoongezeka ndivyo Zanzibar inavyozidi kusonga mbele kimaendeleo na kufikia malengo ya kujitegemea kutokana na kupata wataalamu wa ndani ambao wanategemewa kuwa na uzalendo mkubwa wa kuitumikia nchi yao.

Jaji Mkuu alisema chuo hicho kina nafasi zuri ya kupunguza uhaba huo wa wataalamu kutokana na jitihada kinachozifanya licha ya mazingira magumu. 

“Serikali imekuwa ikifanya juhudi za makusudi kwa ajili ya kujenga mazingira bora kwa lengo la kuwawezesha wale wote wanaohitimu katika vyuo vya elimu ya juu kuwa na uwezo wa kujiajiri wenyewe pamoja na kuajiriwa katika sekta ya umma pamoja na sekta binafsi,” alisema Jaji Makungu.

Aidha alisema katika kuzingatia mabadiliko ya sera za kiuchumi kitaifa na kimataifa inawalazimu wanafunzi waliohitimu taaluma ya sheria kuelewa kuwa serikali haibebi jukumu la kuajiri badala yake inaweka mazingira mazuri ya kutoa muongozo wa elimu inayotolewa itumike ipasavyo kwa ajili ya wahitimu kupata njia ya kujiajiri wenyewe na kuondokana na dhana ya kutegemea ajira kutoka serikalini.

Alisema kazi ya kujenga uchumi wa nchi ni ngumu na inahitaji bidii na uwezo wa kujitolea kwa kila mwananchi, hivyo kupitia juhudi hizo ni muhimu wakati wowote kwa wananchi hususani vijana wakawa tayari katika kubuni mbinu mpya, ili kukabiliana na changamoto ya ajira.

Aliwataka wahitimu hao kutumia taaluma waliyoipata na kuwa wataalamu bora ambao wataaminiwa na jamii kwa kuwa na uadilifu, uaminifu, bidii na kuzingatia kanuni na nidhamu.
Jaji Makungu aliwataka wahitimu hao wasiridhike elimu waliyoipata badala yake wajiendeleze katika ngazi zingine za juu.
Mwenyekiti wa Baraza la chuo hicho ambae pia ni Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar, Ibrahim Mzee Ibrahim, alisema wanajivunia uwapo wa wataalamu wa ndani ambao wanaweza kutoa elimu kwa vijana.
Mkuu wa Chuo hicho, Walid Mohammed Adam, alisema lengo la kuanzishwa kwake ni kujenga uwezo kwa watendaji wa serikali na taasisi binafsi.
Chanzo:Nipashe

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa