Home » » ZAC KUTOA ELIMU KUPUNGUZA VVU KWA VIJANA

ZAC KUTOA ELIMU KUPUNGUZA VVU KWA VIJANA

MWENYEKITI wa Tume ya Ukimwi (ZAC) Professa Saleh Idris amesema kazi kubwa inayoikabili tume hiyo kwa sasa ni kutoa elimu kwa makundi maalumu kupunguza maambukizi ya ugonjwa huo kwa kundi la vijana.
Professa Idris alisema hayo Chake Chake Pemba wakati akizungumza na wananchi katika maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani ambapo ujumbe ni kufikia maambukizi sifuri 3, kama njia mojawapo ya kupunguza ugonjwa huo.
Alisema makundi ya vijana wanaojidunga sindano, pamoja na wanaume wanaofanya mapenzi ya jinsia moja ni miongoni mwa maeneo ambayo yanachangia maambukizi ya Ukimwi kwa kiwango kikubwa sasa.
Kwa mfano alisema maambukizi yanayotokana na vijana kujidunga sindano kutokana na matumizi ya dawa za kulevya yamefikia asilimia 16, wakati wanaume wanaofanya mapenzi ya jinsia moja yamefikia asilimia 12.
“Tumeweka malengo ya kuyafikia makundi maalumu ambayo ndiyo yanayoongoza kwa maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi kwa sasa ikiwemo vijana wanaotumia dawa za kulevya,” alisema.
Aidha aliitaka jamii kujenga tabia ya kuchunguza afya zao mara kwa mara kuweza kujijua kama wapo salama na aina yoyote ya maradhi kwa ajili ya kupata tiba sahihi.
Akizungumza katika sherehe hizo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Fatma Ahabib Fereji alisema ugonjwa wa Ukimwi bado upo kutokana na kuwepo kwa mabadiliko mbalimbali ikiwemo utandawazi na maendeleo ya Sekta ya Utalii.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Chamzo;Habari Leo

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa