Home » » NYUMBA 150 ‘DUBAI’ YA AFRIKA ZAKAMILISHWA

NYUMBA 150 ‘DUBAI’ YA AFRIKA ZAKAMILISHWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Mwandishi Wetu
BILIONEA wa Tanzania asiye na maneno mengi, zaidi ya vitendo katika uwekezaji, Said Salim Bakhressa anayemiliki mtandao wa biashara za kila aina ndani na nje yaAfrika Mashariki, ameibuka na kitu kipya kinachotarajiwa kuiongezea thamani Tanzania katika sekta ya utalii.
Kitu hicho kipya ni mji wa kisasa wa Fumba wenye hadhi ya kimataifa katika ufukwe wa Fumba nje kidogo ya Mji wa kitalii wa Kisiwa cha Unguja, Zanzibar unaotarajiwa kuwa na nyumba za kisasa 720 zenye thamani ya mabilioni ya shilingi. Hatua ya kwanza ya mradi imetumia Dola za Marekani milioni 20 (Sh bilioni 42). Nyumba hizo zitajengwa katika eneo litakalozungukwa na mtandao wa barabara za lami za kilometa 20 na aina nyingine ya miundombinu ya kisasa.
Aidha mji utakuwa na huduma muhimu za kijamii kuanzia shule, hospitali, masoko, hoteli, maduka makubwa, sehemu za kupumzikia zenye michezo ya kisasa sehemu za ufukweni na baharini. “Utakuwa mji wa kisasa na wa kitalii kwelikweli, mji wa kuigwa na gumzo kwa Afrika Mashariki na nchi nyingine za Afrika,” alisema Mkurugenziwa Mawasiliano na Uhusiano wa Kampuni za Bakhressa, Hussein Sufian aliyezungumza na HabariLEOToleo la Afrika Mashariki.
Alisema tayari awamu ya kwanza ya ujenzi unaohusisha nyumba 150 iko katika hatua za mwisho ikitarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu, na kwamba lengo la mradi huo ni kuchochea na kufungua fursa zaidi za kiuchumi kupitia uuzaji bidhaa za ndani, kukuza sekta ya utalii, kuvutia vituo vya uwekezaji, makazi ya kisasa na kadhalika.
Aliongeza kuwa, pamoja na kutanua wigo wa uwekezaji na utalii utakaoihakikishia Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kuwa na `mafuriko’ ya wageni katika mji huo wa kisasa na vivutio vingine vya utalii, mradi huo utatanua pia wigo wa ajira, mapato ya Serikali huku akisisitiza; “Kama mapato yakiongezeka, uwezo wa Serikali wa kutoa huduma kwa jamii utaongezeka.
“Tunaamini Serikali yoyote imara ni ile inayohudumia vyema watu wake, nasi tunadhani kupitia mradi huu tutachangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa nchi. Kwa mgeni atakayeingia Zanzibar, ataweza kujiona yuko katika sehemu ya hadhi ya juu kama zilivyo sehemu nyingine za kitalii duniani.” FAHARI YA NCHI Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji Zanzibar (ZIPPA), Salum Khamis Nassoro akizungumzia mradi huo aliouita ni fahari ya Zanzibar, alisema ni moja ya miradi takribani saba katika eneo hilo linalotarajiwa kuwa na shughuli za kibiashara za kimataifa.
“Nathubutu kusema ni fahari ya Zanzibar, Bakhressa amefungua njia… kwa hatua hii, ni lazima itafika wakati watu kutoka nchi mbalimbali za Afrika wataona fahari kuja kufuata mahitaji yao Zanzibar badala ya kwenda Dubai, kwani kila wanachokifuata huko kitapatikana Zanzibar.
“Miundombinu itakuwa ya uhakika, mwekezaji atashirikiana na Serikali kujenga barabara ya kilometa nane kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Amaan Karume hapa Zanzibar, kutakuwa na mfumo maalumu wa mawasiliano ya kisasa, hapa hautaona nyaya za umeme, za simu, sijui madishi ya setilaiti juu ya nyumba, kila kitu kitafukiwa ardhini…,” alisema Nassoro.
PATO LA TAIFA Kukamilika kwa miradi hiyo kivutio kwa utalii, watalii na wawekezaji wa ndani nje, si kwamba kutainufaisha Zanzibar pekee ambayo pato lake la taifa linategemea utalii kwa asilimia 27, sekta inayochangia fedha za kigeni kwa asilimia 83, bali hata Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kwa ujumla.
Hii ni kutokana na ukweli kwamba, Tanzania Bara inayotenganishwa na bahari ya Hindi kwa umbali wa kilometa 73 tu, sawa na maili 26, ina utajiri wa vivutio, vikiwemo Mlima Kimanjaro ambao ndyio mrefu zaidi barani Afrika ukiwa na urefu wa meta 5,895 sawa na futi 19,340 kutoka usawa wa bahari.
Aidha, kuna vivutio katika hifadhi za taifa, baadhi zikiwa Serengeti, Tarangire, Manyara, Mkomazi, Arusha, Gombe, Mahale, Katavi, Rubondo, Saanane, Mikumi, Ruaha, Saadani na kadhalika. Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro, moja ya maeneo ya urithi wa dunia ambayo pia ni moja kati ya maajabu saba ya dunia, ni kivutio kingine katika ardhi ya Tanzania.
Eneo hili ni la kipekee, ni mahali ambako wanyama na binadamu wanaishi bila kudhuriana. Ndipo lilipopatikana fuvu la kwanza la binadamu wa kale aliyeishi ndani ya Ngorongoro kipindi cha miaka milioni 1.7 iliyopita na fuvu, eneo la Olduvai. Katika hifadhi hii yenye wanyamapori wakubwa takribani 25,000, wamo vifaru, viboko, nyumbu, pundamilia, nyati, simba, fisi, chui na kadhalika.
Kwa ujumla, pato la taifa la Tanzania linachangiwa kwa asilimia 17 na sekta ya utalii, hivyo kuimarika kwa vivutio zaidi ya utalii, kunatoa fursa zaidi ya ukuaji wa kiuchumi kwa nchi, na bila shaka mwelekeo wa Bakhressa katika kuijenga Zanzibar itafungua milango zaidi ya maendeleo, yakiwemo katika sekta ya utalii.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa