Home » » MAMA WA KAMBO AMTESA MTOTO ZANZIBAR

MAMA WA KAMBO AMTESA MTOTO ZANZIBAR

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

MTOTO Milembe Matius mwenye umri wa miaka sita, mkazi wa Mwera Mabonde ya Mpunga visiwani Zanzibar ameshambuliwa kwa kupigwa pamoja na kuchanjwachanjwa vidole vyake viwili vya mkono wa kulia na mama yake wakambo.

Mtoto huyo ambaye anasoma darasa la tatu katika Shule ya Maandalizi alipatwa na mkasa huo juzi huko nyumbani kwao Mwera Mabonde ya Mpunga majira ya asubuhi.

Akizungumza na waandishi wa habari huko katika Hospitali ya Mnazi mmoja alipokuwa akipatiwa matibabu mtoto huyo alisema kuwa, mama yake huyo alimpiga pasipo kosa lolote.

Alisema kuwa, pamoja na kumpiga kwa siku hiyo pia mama huyo alikuwa na kawaida ya kumpiga kila siku na kumtishia asimwambie baba yake mzazi kwa madai kuwa atampiga.

"Kila siku amekuwa ananipiga na juzi alinichinja kwa kisu wakati namenya chungwa, lakini aliniambia nisimwambie baba na nikisema atanipiga," alisema.

Hata hivyo, kwa upande wake baba wa mtoto huyo, Shija alisema kuwa ameanza kuona afya ya mtoto wake ikibadilika, lakini kila anapojaribu kumwambia mke wake huyo huwa haelezi ukweli wowote.

Alisema kuwa, kikawaida yeye huondoka wakati wa asubuhi na kwenda katika shughuli zake za kila siku na kurejea jioni, lakini juzi wakati anarudi alikuta nyumbani hakuna mtu na alipojaribu kufuatilia aliambiwa na majirani kuwa mtoto wake amepigwa na kuhifadhiwa kwa majirani.

Alisema kuwa, wakati alipofika huko alimkuta mwanaye akiwa ameumia sehemu za usoni na kupata michubuko na alipomuuliza alimwambia amepigwa na mama yake.

Alifafanua kuwa, wakati anamkuta mwanawe yupo katika hali hiyo mke wake huyo hakuwepo na alirejea nyumbani majira ya saa 2:00 usiku na alipomuuliza ni sababu gani ya kumpiga mtoto kiasi hicho alijibu kuwa yeye hajampiga.

"Mara baada ya kumkuta mtoto wangu katika hali hiyo, hatua niliyochukua ni kupiga ripoti polisi (kupeleka taarifa polisi) na asubuhi tukaenda kituoni na hivi sasa mke wangu huyo yupo kituo cha Polisi," alisema.

Akizungumza kwa masikitiko baba wa mtoto huyo Shija alisema kuwa, kitendo hicho kimemuathiri sana na hakiwezi kuvumilika.

Naye Daktari ambaye anahusika na fomu namba tatu ya polisi (PF3), Salim Omar Mbaruok alisema kuwa amemfanyia uchunguzi mtoto huyo na kusema kuwa, amepata majeraha katika paji la uso na vidole vyake viwili vya mkono wa kulia vimechanjwa na kitu chenye ncha kali.

"Ni majeraha ya kawaida yaliyo sababishwa na kitu chenye ncha kali na hiyo michubuko pamoja na kuumia katika paji lake la uso," alisema.

Hata hivyo alisema kuwa, matatizo ya udhalilishaji yapo kwa kiasi kikubwa na ni ya kutisha hali ambayo wanahitaji watu kupatiwa elimu zaidi ili kuachana nayo.

Alisema kuwa, kitengo chake kimekuwa kikishughulikia masuala yote ya udhalilishaji ambapo kwa siku hupata kesi karibu ya 10, huku Wilaya ya Magharibi ikiongoza kwa matukio hayo.

Naye Ofisa Dawati la Jinsia na Watoto, Sajenti Haji Mohammed Iddi alisema kuwa, juzi alipokea taarifa ya mtoto kupigwa na mama yake wa kufikia na alipojaribu kufuatilia wamefanikiwa kumtia hatiani na hivi sasa wamo katika kufungua jalada ili ikiwezekana mtuhumiwa afikishwe mahakamani.

Hata hivyo, mtoto huyo hali yake inaendelea vizuri na mara baada ya kupatiwa matibabu aliruhusiwa na mama huyo akiwa yupo katika kituo cha polisi mjini hapa

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Blogs za Mikoa Tanzania
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Blogs za Miikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa