Home » » TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA IKULU YA ZANZIBAR

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA IKULU YA ZANZIBAR

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amevitaka Vyuo Vikuu hapa nchini kuwa makini katika usajili wa wanafunzi wanaojiunga vyuoni humo kwa kuhakikisha wanakidhi viwango vinavyohitajika katika ngazi za Taifa na Kimataifa.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika Chuo Kikuu cha Zanzibar University, kilichopo Tunguu, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja katika hotuba yake aliyoitoa katika Mahafali ya 14 ya chuo hicho.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa hivi karibuni kumeibuka baadhi ya vyuo vinavyosajili wanafunzi bila ya kufuata viwango husika jambo ambalo linaharibu sifa ya elimu na maendeleo ya wananchi na nchi kwa jumla hali ambayo itapelekea kupata wataalamu wasiokuwa na sifa hapo baadae.

Alisema kuwa kuwepo kwa ushindani mkubwa wa kutafuta wanafunzi wapya wanaotaka kujiunga katika vyuo vya ndani na nje ya nchi isiwe sababu ya kuharibu ubora wa elimu kwa kusajili wanafunzi wasio na viwango kuingia katika Vyuo Vikuu.

Aidha, Dk. Shein alivitaka Vyuo Vikuu hapa nchini kuhakikisha kuwa kila mafunzo wanayotoa yanakuwa na Wahadhiri na vifaa vya kutosha sambamba na kuwa na uwezo wa kuendesha mafunzo hayo ili kuepuka kutoa elimu isiyokidhi haja.

Alisema kuwa mambo hayo kwa pamoja ni muhimu katika kuimarisha ubora wa elimu inayotolewa hapa Tanzania.

Rais Dk. Shein alisema kuwa ubora wa elimu inayotolewa ni suala la mashirikiano kati ya jamii, vyuo na serikali na kuhimiza haja kwa Vyuo Vikuu vya Zanzibar kufanya kazi karibu zaidi katika kuhakikisha elimu inakidhi mahitaji yaliokusudiwa na wanafunzi nao wanakidhi viwango.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwataka wazee kuendelea na malezi bora ya watoto wao sambamba na kuwa karibu na maendeleo yao ya elimu huku akiwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kutoa elimu bure pamoja na kutoa mikopo kwa wanafunzi wenye sifa ya kujiunga na elimu ya juu.

Aidha, aliwahakikishia kuwa Serikali inafanya mageuzi katika mfuno wa elimu ili uende sambamba na mahitaji ya nchi pamoja na mabadiliko ya Teknolojia yanayotokea duniani kote.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisikitishwa na hali ya udanganyifu iliyofanywa na baadhi ya wanafunzi kwa Bodi za Mikopo hapa nchini ambao walifika hatua ya kutoa taarifa zisizo na ukweli hali ambayo huwanyima fursa wanafunzi wenye sifa na dhamira ya kweli ya kutaka kuendelea na masomo pamoja na kusababisha hasara kwa Serikali.

Kutokana na hali hiyo, Dk. Shein alisema kuwa ilimlazimu kuchukuwa hatau za dharura kusitisha utoaji wa mikopo kwa muda lakini hata hivyo, alisema kuwa baada ya kuridhishwa na kufikia hatua zinazohitajika aliruhusu Bodi ya Mikopo ya Zanzibar iendelee kutoa mikopo kwa mwaka 2016/2017 huku akiitaka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuielimisha jamii juu ya suala zima la mikopo na hatari za udanganyifu.

Hivyo Dk. Shein aliwataka wanafunzi wafahamu kwamba kufanya udanganyifu katika suala la mikopo ni kosa la jinai hivyo aliwataka kujiepusha na  mambo hayo na kuwasihi kuitumia vyema mikopo wanayopewa kwa malengo yaliokusudiwa.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alifurahishwa na taarifa ya kuwepo kwa mashirikiano mazuri kati ya vyuo vya Zanzibar kikiwemoChuo Kikuu cha Zanzibar University, Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Chuo Kikuu cha SUMAIT, hatua ambayo inajumuisha mashirikiano katika ufanyaji tafiti na ubadilishanaji wakufunzi.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema  kuwa hivi karibuni alitia saini hadharani Mswada wa Sheria ya utafiti na uchimbaji wa Mafuta na Gesi Zanzibar, hatua ambayo itaiwezesha Zanzibar kuanza taratibu za kuchimba mafuta na gesi yake wenyewe na kuvitaka vyuo vikuu hapa nchini kuitumia fursa hiyo katika kuunga mkono juhudi hizo za maendeleo kwa kuanzisha programu zitakazo husiana na mafuta na gesi.

Vile vile, Dk Shein alivitaka vyuo vikuu hapa nchini kutilia mkazo elimu ambayo itamuwezesha muhitimu kuweza kujiajiri na kujitegemea mwenyewe badala ya kusubiri ajira kutoka serikalini.

Dk. Shein alitoa pongezi na shukurani kwa uongozi wa chuo hicho kwa kukiimarisha chuo chao kwa kiasi ambacho kimepelekea ongezeko kubwa la wahitimu mwaka huu wapatao  1440 idadi ambayo ni zaidi ya mara mbili ikilinganishwa na ile ya mwaka jana iliyokuwa 667  huku akipongeza kwa kuazishwa programu mpya katika ngazi ya Uzamili na Uzamifu.

Pia, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwasihi wahitimu hao kwa kuwataka wawe makini katika hatua nyengine ya maisha wanayoingia hivi sasa ambapo baadhi ya wakati watalazimika kutafakari na kuchukua maamuzi juu ya masuala muhimu na magumu katika maisha yao bila ya kupata miongozo ya wazazi na walimu wao.

Aliwataka mkuazia sasa wafahamu kwamba elimu waliyonayo ndiyo sialaha muhimu wanayoihitaji kuitumia katika kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha na kufanya maamuzi yanayozingatia busara na hekima ili waweze kufuzu katika maisha yao.

Aidha, aliwataka wahitimu hao kutochagua kazi hasa wakizingatia kuwa soko la ajira limekuwa na ushindani mkubwa  na kuwataka kufikiri namna ambavyo wataweza kuitumia na kunufaika na mifuko mbali mbali iliyoanzishwa na Serikali kwa lengo la kuwasaidia vijana na makundi mbali mbali ili waweze kujiajiri wenyewe na kukuza maendeleo ya ujasiriamali hapa nchini.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki  Pembe Juma alitoa pongezi kwa uongozi wa chuo hicho kutokana na kuendeleza utamaduni mzuri wa kutoa ufadhili kwa wanafuzi wa Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu hatua ambayo imesaidia kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini.

Waziri huyo pia, alitumia fursa hiyo kusisitiza umuhimu wa kurejesha mikopo kwa wanafunzi wanaokopa kupitia Bodi ya Mikopo ya Zanzibar ili fedha hizo ziweze kuwasaidia wanafunzi wengine.

Makamo Mkuu wa Chuo hicho Profesa Mustafa Rashash nae alitumia fursa hiyo kueleza mashirikiano yaliopoa kati ya chuo hicho na Serikali pamoja na vyuo vyengine na kueleza wanavyothamini juhudi za serikali katika kuendeleza sekta ya elimu hapa nchini.

Hata hivyo, Profesa Rashash alieleza namna ya chuo hicho kilivyojipanga katika kuimarisha programu zake mbali mbali chuoni hapo zikiwemo mpya na zile za zamani kwa lengo la kukuza sekta ya elimu sambamba na kuendelea kukipa hadhi zaidi chuo hicho.

Profesa Saleh Idris ambaye ni Kaimu wa Bodi ya Chuo hicho kwa upande wake alieleza azma ya chuo hicho kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya kwa kuanzisha Digrii ya Uuguzi ambapo wahitimu 53 ni miongoni mwa waliohitimu mahafali ya mwaka huu.

Pamoja na hayo, Profrsa Idris kwa niaba ya chuo walitumia nafasi hiyo kumpongeza Dk. Shein kwa kuchaguliwa kwa kipindi cha Pili kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi huku akieleza mikakati ya chuo hicho katika kuongeza majengo yakiwemo ya daghalia.

Viongozi mbali mbali walihudhuria katika Mahafali hiyo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balaozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Mkuu wa Chuo hicho Profesa Suleiman Bin Nasry Basahal, Wakuu wa Vyuo mbali mbali,Mawaziri na viongozi wengine kadhaa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa