Home » » WANASIASA WETU NA WOGA WA MABADILIKO

WANASIASA WETU NA WOGA WA MABADILIKO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kitabu cha Cycles of American kilichotungwa na Arthum Schelesinger Jr kinasema kutokufungwa na mawazo ya kale katika mazingira yanayobadilika kunampa kiongozi wa kidemokrasia nafasi ya kutengeneza vionjo vitamu ili apendwe na kufurahiwa na wengi.
Wanasiasa wetu wengi wao ni watu wenye woga wa mabadiliko, wanavyochukia mabadiliko ya kifikra ni kama vile mtoto achukiavyo kuchomwa sindano na daktari. Hawapendi fikra mbadala na wala kubadilika.
Namchukulia kiongozi wa zamani katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mzee Hassan Nassor Moyo kuwa ni miongoni mwa viongozi wasiofungwa na mawazo ya kale na aliyekuwa tayari kukabili changamoto za mawazo kinzani kwa hoja.
Ijapokuwa kwa wakati huu hayupo tena katika ulingo wa kisiasa, lakini Mzee huyu anabaki kuwa mtumishi wa wananchi aliejipa wajibu wa kuisadia jamii kuondokana na mazonge ya fikra za ukale hasa wanapokabili jambo lenye kugusa masilahi ya nchi na wananchi kwa ujumla.
Mchakato wa katiba mpya umemkuta Mwanasiasa huyo mkongwe mahiri, shupavu na hodari akiwa mwenye afya na siha njema ambaye kwa sababu ya ari ya kupenda nchi yake hana kago ya kukaa pembezoni.
Hapendi awe nje ya uwanja kubaki mtazamaji katika jambo ambalo angeweza kushiriki na kusaidia hususan jamii ya vijana ambayo kwa namna moja au nyingine si mashuhuda wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Alivyokuwa kila Mtanzania kuwa na ari ya kutaka mabadiliko ya muundo wa Muungano, ndivyo alivyo Mzee Hassan Nassor Moyo. Mara kadhaa nilipokutana na kubadilisha mawazo, alinieleza kuwa yeye si mtu wa kufungika kimawazo.
Bila shaka anaungana na Sheikh Shaaban Robert katika kitabu chake cha Kusadikika alipoandika “Nashikilia ukale kama ni lazima na huuacha vilevile ikiwa haunifai. Nitaendeleza kubadili mambo kwa sababu siwezi kuwa mtumwa wa kutenda hayo kwa hayo nikazuia bidii yangu. Ukale huniletea mashaka nikajidai kuwa ni wajibu wangu”.
Mzee Moyo hashikilii ukale akazuia mabadiliko ya leo na ya miaka hamsini ijayo. Amekuwa miongoni mwa wanasiasa walioweka wazi misimamo yao kuhusu ulazima wa mabadiliko katika Muungano.
Viunga vya Zanzibar na Tanzania Bara kwa jumla vinatokota kwa hoja ya Muungano, hakuna asiyejuwa jambo hilo, kila kona, lakini mbona kila nikitafakari sauti hizi nahisi kama vile wasemaji wake wanaotaka mabadiliko katika mfumo wa muundo wa Muungano hoja zao ni zenye mantiki na zisizotakiwa kukejeliwa?
Hivi unawazaje kukataa ukweli kwamba mfumo wa muundo wa Muungano una matatizo na tunalazimika kubadili? Kutoa hoja ya kutaka mabadiliko imekuwa nongwa kiasi cha watu kuchukiana, kuhasimiana au kuvunjiana heshima hadharani?
Ikiwa mtu anaamini kuwa ana nguvu ya watu inayomuunga mkono katika hoja yake, ya nini kuweweseka? Tusubiri kura ya maoni itakuja na kila mwenye haki atapiga kura na kuamua, hapo ndipo itajulikana wazi kuwa wale waliokuwa wakipiga porojo na wale waliokuwa wakitoa hoja zenye mantiki.
Baadhi ya watu hawana hesabu nzuri, pungufu kwao kamili, wana macho hayaoni, wana masikio hayasikii, wana akili hawazitumii.
Watu shupavu na wenye misimamo, mara zote hawaogopi kuadhibiwa kwa misimamo yao au mitazamo ya fikra zao.
Unawazaje kubeza mawazo ya Mzee Moyo ambaye Baraza la Kwanza la Mawaziri katika Jamhuri ya Watu wa Zanzibar mwaka 1964 alikuwa Waziri mdogo na baadye kuwa Waziri kamili katika SMZ na SMT.
Uzoefu wake serikalini na katika Chama cha Mapinduzi kabla ya hapo Afro Shiraz Party unatosha kuyapa uzito yale anayoyashauri kuhusu katiba mpya kwani ni yeye akiwa na wajumbe wengine kutoka ASP na TANU waliofanikisha kuunganishwa kwa vyama hivyo na kuzaliwa kwa CCM.
Tukumbuke kuwa wanachama wengi wa ASP walipinga wazo la kuunganisha vyama. Lakini kwa sababu ya dhamira ya umoja, Mzee Moyo, marehemu Sheikh Thabit Kombo Jecha na mwenyewe Rais wa pili wa Zanzibar na Mweyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mzee Aboud Jumbe Mwinyi walifanikisha lengo hilo. Kadi ya CCM ya Mzee Moyo haipindukii namba kumi.
“Vijana wangu nataka kuwaeleza kuwa suala kubwa ni nchi, chama lilikuwa jambo la pili na kama viongozi wetu wa chama wanataka kutupeleka huko tukaeleze msimamo wa Chama, mimi nasema Muungano umekuja kwanza na hivyo ndiyo ninavyojua mimi na huo ndio msimamo wangu” Anasema Mzee Moyo.
Maelezo haya ya Mzee Moyo hayakuwa ni maneno ya porojo au mazungumzo ya “Alfu Lela Ulela bali anatumia uwezo na uzoefu wake kuelezea kero za Muungano, faida yake na wapi Wazanzibari waelekee katika kupata mfumo wa muundo wa Muungano wenye usawa kupitia Katiba Mpya
 Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa