Home » » TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA IKULU YA ZANZIBAR

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA IKULU YA ZANZIBAR

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



SERIKALI ya Japan kupitia Shirika lake la Kimataifa la Maendeleo (JICA) limeahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa diko na soko la kisasa la samaki linalotarajiwa kujengwa Malindi mjini Zanzibar.

Makamo wa Rais wa Shirika hilo la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA), Yasushi Kanzaki aliyasema hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya  mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

Katika maelezo yake, Makamo huyo wa Rais wa (JICA) ambaye aliongozana na uongozi wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, alimueleza Dk. Shein kuwa Shirika hilo liko tayari kuanza ujenzi huo mapema mwakani na hivi sasa limo katika hatua za mwisho za matayarisho.

Makamo huyo alisema kuwa mradi wa ujenzi wa soko hilo utakuwa ni wa kisasa na wa kuvutia kutokana na kukidhi mahitaji yote yanayopaswa kuwepo kwa ajili ya diko na soko la samaki la kisasa.

Alisema kuwa soko hilo litakuwa la pekee katika ukanda wa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara ambapo ujenzi wake unatarajiwa kufanyika ndani ya muda wa miaka miwili kuanzia muda utakaoanza ujenzi huo.

Aidha, Bwana Yasushi Kanzaki aliahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi mengine muhimu ya maendeleo ukiwemo mradi wa kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji, uvuvi na kuendeleza mradi wa usambazaji maji kupitia Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA).

Katika mazungumzo yake kiongozi huyo, alieleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Shirika hilo katika kuimarisha mradi wa maji utakaokwenda sambamba na teknolojia mpya ya kisasa ili kurahisisha usambazaji na upatikanaji wa maji safi na salama hapa nchini.

Sambamba na hayo, Makamu huyo wa Rais wa Shirika la (JICA), alimueleza Dk. Shein matayarisho yanayoendelezwa na Shirika lake na hatua zilizofikiwa katika kuimarisha mradi wa kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji kwa mabonde maalum yaliotengwa hapa Zanzibar.

Nae, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alitoa pongezi na shukurani kwa Serikali ya Japan kupitia shirika lake la (JICA) na kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake wanathamini sana misaada na ushirikiano na uhusiano uliopo kati yake na (JICA).

Alisema kuwa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA) ni  mshirika muhimu wa maendeleo hapa Zanzibar kwani limeweza kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo ya kilimo, maji, afya, elimu, uvuvi na mengineyo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kupongeza azma ya ujenzi wa soko hilo ambapo alisema kuwa utasaidia kuendeleza malengo ya serikali katika kuimarisha sekta ya uvuvi na kusisitiza kuwa tayari miundombinu ya eneo linalotarajiwa kujengwa soko ikiwemo umeme na maji lipo katika hatua za mwisho za matayarisho pamoja na kueleza kuwa tayari ruhusa kutoka UNESCO nayo imeshatolewa.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka lengo la kuanzisha programu ya uvuvi wa bahari kuu ambayo pia, itawasaidia wavuvi kuvua katika kina kirefu cha maji ili kuongeza kiwango cha samaki wanaovuliwa na kuongeza fursa za ajira, biashara na kuchangia ukuaji wa uchumi.

Kwa upande wa kilimo cha mpunga wa umwagiliaji maji, Dk. Shein alisema kuwa tayari Serikali imo katika juhudi za kuweka miundombinu kwa kuimarisha eneo la hekta 2,200 katika mabonde ya mpunga  huku akieleza huku akilipongeza Shirika la  JICA kwa kuuunga mkono mradi huo.

Alisema kuwa lengo la Serikali katika kuimarisha kilimo hicho ni kupunguza ama kuondosha kabisa uagiziaji wa mchele kutoka nje ya nchi unaofanyika hivi sasa kwani matumizi ya mchele hapa nchini ni tani 80 elfu kwa mwaka ambapo kati ya hizo tani 64 elfu huagizwa na zinazozalishwa nchini ni tani elfu 16 tu.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Shirika hilo kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza mradi wa maji safi na salama, kwa awamu zote huku akieleza hatua inayofuata ya kuimarisha mradi huo kwa utaalamu zaidi utasaidia upatikanaji wa huduma hiyo kwa ufanisi zaidi.

Madhumuni makubwa ya mradi wa ujenzi wa diko na soko la kisasa huko Malindi ni kuwawezesha wavuvi wanaotumia soko hilo kuuza na kununua samaki wao wakiwa salama kiafya pamoja na kuwepo mazingira mazuri ya kuweka vyombo vya uvuvi na biashara kwa wavuvu, wachuuzi, madalali, wauzaji wadodgo wadogo na wanunuzi.

Tsh. Bilioni 14 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi wa soko hilo ambalo litakuwa na maeneo sita ya kuendesha mnada, meza ndogo 141 za wauzaji wadogo wadogo, sehemu 13 za kuchakatia samaki, linatarajiwa kwa siku litakuwa kuegesha vyombo vya uvuvi wa kienyeji 392 na wafanyakazi 1,400 watakaoshusha na kupakia samaki ambapo pia, wafanyabiashara 6,500 watatumia eneo hilo salama.
 
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa